Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuwa miongoni mwa wachangiaji kwenye Wizara hii. Niishukuru sana Serikali kupitia Mheshimiwa Rais kwa kutoa fedha za miradi ya maendeleo ya maji. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na wasaidizi wake kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuwatendea kazi Watanzania.

Mheshimiwa Spika, nianze na Mradi wa Maji wa Ziwa Tanganyika. Wananchi wa Mikoa ya Kigoma, Katavi, Rukwa, kilio chao kikubwa ni Mradi wa Maji kuyatoa Ziwa Tanganyika, ili yaje tatatue kero ya maji kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Waziri amekuja Mpanda na kwa uungwana alionao aliwashirikisha Wabunge na alibadilisha mfumo wa ziara yake ambayo alikuwa amepangiwa na watendaji. Tukaenda naye kwenye chanzo cha maji Ziwa Tanganyika na yeye aliona umuhimu kabisa. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri mradi ule ndiyo utakaowasaidia wananchi wa mikoa hiyo, tunaomba akautekeleze. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mji wa Mpanda umekua, una mahitaji makubwa sana ya maji na tatizo la maji kwa Mkoa wa Katavi litatatuliwa kwa Mradi wa Maji wa kuyatoa Ziwa Tanganyika. Niombe sana hili alishughulikie Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi mwingine ambao napenda kuuzungumzia ni Mradi wa Mishamo. Mheshimiwa Waziri amenipa miradi mingi ya maendeleo kwenye Wilaya ya Tanganyika, tunayo miradi yenye zaidi ya shilingi bilioni nne ambayo ameitoa na inatusaidia japo ni miradi midogo midogo, lakini ikikamilika tutakuwa na asilimia karibu 80 ya upatikanaji wa maji safi na salama, lakini shida ambayo ipo tuna wakandarasi wabovu wanaotuletea.

Mheshimiwa Spika, tuna Mkandarasi wa Mradi wa Mishamo, HAMWA; mradi huu una thamani ya shilingi milioni 886, toka alipokuja akasaini huo mradi na akapewa fedha za awali shilingi milioni 100 hajafanya uendelezaji wa aina yoyote. Nimwombe Mheshimiwa Waziri wamsimamie huyu mkandarasi ili aweze kukamilisha huu mradi ambao utahudumia Vijiji vya Mishamo, eneo la Ifumbula, Kapemba na Kijiji cha Isenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi mwingine ambao Mheshimiwa Waziri tunaomba akasimamie ni Madi wa Kata ya Katuma. Mradi huu ni mradi wa muda mrefu na Naibu Waziri aliambatana na Makamu wa Rais pale Katuma na Makamu wa Rais alitoa maelekezo ya kuhakikisha Mkandarasi
HERMATEC anakamilisha ule mradi kwa muda uliokuwa umepangwa. Mpaka sasa tunavyoongea, bado huo mradi haujakamilika na inashangaza Makamu wa Rais anatoa amri, lakini mtekelezaji mpaka muda huu hajafanya hivyo. Sasa sijui atamsikiliza nani? Kama Makamu wa Rais anatoa maagizo na hayatekelezwi?

Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, najua kazi anayoifanya na jitihada anazofanya ni kubwa. Sisi Wabunge asilimia kubwa tunamwamini anachapa kazi nzuri, wakamsimamie ili akamilishe huo mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni tatizo la vitendeakazi. Halmashauri yangu ya Wilaya ya Tanganyika Mheshimiwa Waziri anaijua, ametembea, tumeenda kule ukanda wa ziwa na ametembea hadi kwenye eneo tunalopakana na Mkoa wa Kigoma. Hakuna magari ambayo yanaweza yakawasaidia kufanya shughuli za maendeleo na wakati huu tuna miradi mingi ambayo inasimamiwa na hao watendaji wa MURUWASA. Nimwombe Mheshimiwa Waziri kwenye bajeti hii tunahitaji atoe msukumo ili tupate gari ambalo litasaidia utekelezaji wa miradi ambayo inaenda kwenye maeneo ya kwetu. Mheshimiwa Waziri, akiyafanya haya yatatusaidia sana katika utekelezaji wa miradi ile ambayo anaisukuma ili iweze kuwafanyia kazi wananchi.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo napenda nitoe ushauri, ni kuunganishwa kwa Jumuiya za Watumiaji Maji. Ni wazo zuri ambalo wanakuja kuunganisha mfumo wa kuunganisha jumuiya zile za watumiaji maji, lakini kuna kasoro ambazo zinajitokeza. Unaunganisha eneo ambalo wengine wanataka kupewa huduma na wengine ndio wanaotoa gharama za maji. Sasa nimwombe Mheshimiwa Waziri, tusije tukawalazimisha mahali ambapo mifuko inaweza ikajitegemea, tuwaache wafanye hivyo kwa ajili ya ustawi wa miradi endelevu. Kuna maeneo mengine mifuko hiyo imekufa na huduma inakuwa ya shida kwa sababu tunawalazimisha kuwaunganisha ili waweze kubebana wakati wapi wengine uwezo wa kubebana haupo.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, niendelee kumshukuru Mheshimiwa Waziri na watendaji. Naamini yale ambayo ni ya msingi kwetu sisi Mkoa wa Katavi tunahitaji Mradi wa Maji wa Ziwa Tanganyika ambao naamini atatusaidia katika utekelezaji. Mradi ule ukikamilika kuna nafasi ya kuwa zaidi ya asilimia 100 tutakuwa na upatikanaji wa maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)