Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, na kwa hakika siyo tu kwa kunipa nafasi, wewe umekuwa ni mwalimu na pia umekuwa ni mlezi. Umekuwa ukituongoza vizuri katika Bunge letu, na kwa kweli unaingia sasa kwenye rekodi ya Maspika wa viwango. Nakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa zawadi ya uhai. Pili, namshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa kweli Wana-Nachingwea wametufanyia vitu vingi sana, siyo tu kwenye sekta hii ya maji, amegusa karibu maeneo yote. Kwa hiyo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, kipekee kwenye jambo hili la maji, wakati nikiwa mwanzoni wa Ubunge wangu, nililalamika sana hapa kuhusu suala la maji na hasa kwenye Vijiji vya Mchangani na Namanga. Leo nasimama nikiwa na furaha kwamba vijiji hivi; Kijiji cha Mchangani sasa maji yanamwagika. Hii ni kazi nzuri ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwenye Kijiji cha Namanga, kwenye huo mradi wa Namanga ambao una zaidi ya Shilingi milioni 700, muda wowote kuanzia sasa mkandarasi yuko site, anaendelea kufunga pump. Kwa hiyo, maji yanaenda kutoka sasa, muda siyo mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hivyo tu, kwenye ukurasa wa 35, Hotuba ya Mheshimiwa Waziri, Serikali inakwenda kutekeleza mradi mkubwa wa maji ambao utanufaisha Wilaya ya Ruangwa na Nachingwea pamoja na Wilaya ya Lindi.

Mheshimiwa Spika, naishukuru sana Serikali kwa mradi huu, kwani unaenda kuwatua ndoo wamama wa Nachingwea, Ruangwa pamoja na Lindi. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na timu yake. Ombi langu kwenye eneo hili, Mheshimiwa Waziri aende kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa wakati. Watu wana matumaini makubwa sana na mradi huu ambao unakwenda kunufaisha vijiji 56. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri alimwagiza Mheshimiwa Naibu Waziri kuja kwenye Jimbo langu la Nachingwea, na kwa kweli alijionea kwa macho namna ambavyo watu wanahainga kwenye suala la maji kwenye Vijiji vya Ngunichile. Alikwenda Namikango, na pia viko vijiji vingine; kuna Mbondo, Kilimarondo na Matekwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili la Ngunichile, hakuna chanzo cha uhakika, na tuliomba visima virefu. Kwenye bajeti hii ambayo imepita, tuliomba visima tisa, lakini vilivyoidhinishwa ni vitano. Mheshimiwa Waziri nakuomba sana, tumalizie tu hivyo vinne, peleka fedha kwenye Jimbo langu la Nachingwea ili wananchi wale waendelee kufaidi matunda ya kazi nzuri ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, uko mradi wa Mbwinji ambao unanufaisha Wilaya ya Masasi na Nachingwea. Kwa sasa wataalam wetu wanakamilisha usanifu wa mradi mpya, mradi pacha kwenye mradi huu wa Mwbinji. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, andiko hili litakapokuwa linafika kwenye Wizara, ajitahidi kuhimiza hizo fedha kufika kwa wakati kwa sababu tunakwenda kunufaisha vijiji zaidi ya 18 kwenye Jimbo la Nachingwea na vijiji sita kwenye Wilaya ya Ruangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, iko changamoto ya wenzetu wa RUWASA, wanafanya kazi nzuri sana, na hasa viongozi wa Mkoa wa Lindi pamoja na timu yake, pia Engineer wa Nachingwea, Engineer Sultan pamoja na timu yake wanafanya kazi nzuri sana. Hata hivyo, wanafanya kazi kwenye mazingira yasiyo rafiki sana, hawana usafiri wa uhakika. Gari waliyonayo ni ya tangu 2010, imechoka. Engineer anaweza kwenda mahali kushuhudia au kufuatilia miradi ya maji, anakwama huko. Pia halina uhakika tena kwa sababu linagharimu matengenezo makubwa ya mara kwa mara.

Mheshimiwa Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, atuletee gari jipya Nachingwea ili vijana wale walio tayari kufanya kazi hii ya kizalendo waendelee kusimamia miradi hii ambayo Mhehsimiwa Rais anatupatia kwenye jimbo letu. Siyo hivyo tu, kwenye eneo hili, hata watumishi ni wachache. Tunao wahandisi wawili, tunaye dereva mmoja, secretary mmoja, pamoja na mwenyewe Engineer. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hali hii, hawa wanafanya kazi kwa muda mwingi kuliko ilivyo kawaida. Kwenye hili sasa, naomba sana, vijana hawa wanaofanya kazi ya kizalendo, Mheshimiwa Waziri apate nafasi ya kututembelea ili tumwonyeshe kwa macho kazi nzuri na kubwa ambazo wanazifanya ili waone namna ya kuwatumia kwa ukubwa wake zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo yote, ni vizuri tuhakikisha hawa wakandarasi ambao wanapewa miradi, wanakamilisha kwa wakati. Huu mradi ambao nimepongeza na kuusifia wa Namanga, ulitakiwa ukamilike kwa muda mrefu uliopita, mwaka 2022 mwezi wa Kumi na Mbili. Baadaye wakasema kwamba kuna ununuzi wa pamoja wa mabomba na kadhalika. Kwa hiyo, akaongezewa tena muda, akasema mwezi wa Nne. Bado ikaendelea kurushwa hiyo, mpaka sasa hivi ambapo wamefikia hatma ya mradi huu.

Mheshimiwa Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, kwenye mipango yetu wakati tunaenda kutekeleza hii miradi, tuhakikishe tunakwenda kutekeleza kwa wakati, na hii itakwenda kuimarisha, hata namna ambavyo wananchi wanaona hii miradi inakwenda. Kuna maeneo mengine ukifika ukawaeleza, kwa sababu tayari wameshashuhudia miradi, wakati wa mwanzo wanaambiwa mradi huu utachukua miezi sita, au miezi 18, baadaye inaongezwa tena. Halafu ile ya kuongezwa kimya kimya, inaleta sintofahamu, na wakati mwingine sisi wawakilishi tunaonekana hatuko sawasawa.

Mheshimiwa Spika, kwa kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake pamoja na wataalam wake, mimi kama Mbunge wa Nachingwea, naridhika sana. Ninaamini hata haya niliyoyasema kwa uchache yanakwenda kufanyiwa kazi. Mheshimiwa Waziri ukipata nafasi tembelea Nachingwea. Sisi hatuna zawadi kubwa kule, hatufugi ng’ombe, ila tutakushikia kuku. Hizo ndiyo mila za watu wa Kusini, na hiyo ndiyo itakuwa zawadi kubwa kabisa kuliko yote.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, na ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)