Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na kunifanya nisimame leo mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya na hasa kwenye sekta hii ya maji. Mambo makubwa sana yamefanyika, uwekezaji mkubwa sana umefanyika na changamoto nyingi tulizokuwanazo kwenye sekta ya maji sasa zimepungua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitawapongeza Wizara ya Maji. Mheshimiwa Waziri, Naibu na timu yote ya watendaji, kwa kweli mnafanya kazi kubwa sana. Mimi ni shuhuda kupitia Jimbo langu la Ukerewe, mmefanya kazi kubwa. Pamoja na kwamba kuna changamoto bado, lakini tulipokuwa, na hapa tulipo, kuna kila sababu ya kuwapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tanzania kama Taifa, tuna vyanzo vingi vya maji. Sisi Ukerewe tunazungukwa na Ziwa Victoria. Katika ukubwa wa eneo la Wilaya ya Ukerewe, squire kilometer kama 6,400 ni asilimia 10 tu iliyo nchi kavu. Asilimia 90 yote ni maji. Sasa kwa kusema hivyo, wakati mwingine inaleta shida unapomwambia mtu kwamba Ukerewe tuna shida ya majisafi na salama.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza Wizara, mmefanya kazi kubwa. Mwaka 2022 mmetupa pesa nyingi kwa ajili ya miradi ya maendeleo, tumepiga hatua. Miradi hii ikikamilika, kimsingi tutabakiza eneo dogo sana. Hivi sasa tuna chini ya asilimia 70 ya maeneo ambayo yanapata majisafi na salama, lakini miradi yetu ikikamilika, tutakuwa tumeenda mpaka zaidi ya asilimia 90, ni jambo la kupongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, nampongeza Mheshimiwa Waziri na Wizara kwa ujumla, kwa mwaka huu wa fedha mmetutengea zaidi ya Shilingi bilioni tano kwa ajili ya vijiji vyetu vitano vya maji; Kijiji cha Chabilungo, Kamea, Mkuno, Halwego na Bugorora, jambo ambalo litafanya coverage ya watu watakaokuwa wanapata majisafi na salama, kama miradi hii itakamilika, kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, tuna shida kubwa moja ambayo niliona ni muhimu niiseme hapa ili Mheshimiwa Waziri uone namna gani utaweza kutusaidia. Mwaka 2021 tulikuwa na tatizo kubwa sana kupitia mradi wetu wa maji vijijini, maarufu kama Mradi wa Kazilankanda, ambao unahudumia zaidi ya vijiji 10. Mradi ule unapata umeme kutoka TANESCO lakini bahati mbaya wana-treat mradi huu ambao unatoa huduma kwa wananchi kama mradi wa kibiashara, jambo ambalo limekuwa linafanya kila mwezi kunakuwa na service charge kwenye bili zaidi ya Shilingi milioni tatu.

Mheshimiwa Spika, haingii akilini kwamba inakuja bili ya Shilingi milioni tano, lakini service charge pekee ni zaidi ya Shilingi milioni tatu. Jambo hili lilitufanya tuweze kukaanao na kushauriana. Wakatushauri tutafute pump nyingine ambazo zitaendana na kiwango kile cha matumizi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri nawashukuru, mlinisaidia sana tukaweza kuagiza pump, tukazifunga. Wakatuomba tulipe deni, tumelipa, lakini bado wanakuwa wagumu sana kubadili mita yao, jambo linalopelekea bili iwe kubwa, na inakuwa ni mzigo kwa wananchi. Wanaingia gharama kubwa sana kulipa deni lile. Mwisho wa siku katika mwezi, wananchi wanapata maji wiki moja, wiki tatu hawapati maji.

Mheshimiwa Spika, sasa naiomba Wizara, sioni sababu ni kwa nini TANESCO, Taasisi iliyo chini ya Serikali, RUWASA Taasisi iliyo chini ya Serikali, mnashindwa kukaa na ku-solve tatizo kama hili, mwisho wa siku wanaoteseka ni wananchi.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Ukerewe wanaopata maji kupitia mradi huu wa maji vijijini, Mradi wa Kazilankanda wanapata mateso makubwa sana. Leo kwa mfano ninavyozungumza hapa, wananchi wanaopata maji kupitia mradi huu, wana zaidi ya wiki tatu hawajapata maji, kwa sababu tu ya kukosa muafaka kati ya Wizara ya Maji na Wizara ya Nishati, juu ya nini kifanyike kwenye suala la umeme ili wananchi wapate huduma wanayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru wakati Mheshimiwa Naibu Waziri, amekuja Ukerewe alisaidia angalau ku-solve tatizo hili. Baada ya hapo, atakumbuka tulikubaliana kwamba sasa baada ya ku-clear deni, TANESCO wabadili mita, lakini bado jambo hilo halikufanyika. Kwa hiyo, naiomba Serikali ilichukulie jambo hili kwa uzito. Haiwezekani tunazungukwa na maji halafu bado wananchi wa Ukerewe waendelee kuathirika na maradhi yanayotokana na matumizi ya maji yasiyo safi na salama. Ni jambo lisilokubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana Mheshimiwa Waziri alichukulie jambo hili kwa uzito wa pekee. Nawashukuru, tulileta maombi tusaidiwe angalau kuongeza mtandao wa usambazaji wa maji kwenye eneo la mjini. Kwenye bajeti hii tumekubaliwa, wametupa angalau shilingi milioni 300. Ni jambo jema, lakini bado nitaendelea kuomba, kwa lile ombi la karibu shilingi 1,200,000,000 waendelee kutusaidia.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza Mameneja wa Maji wa eneo la wilaya na mkoa, wanafanya kazi kubwa sana. Mtusaidie kutupa pesa hizi tuongeze mtandao. Wana uwezo wa kujisimamia na kukusanya mapato yatakayowafanya waweze kuongeza mtandao kwa gharama zao, lakini kinachokosekana ni ule mtaji tu wa kuongeza mtandao. Watusaidie kwenye eneo hili, ili mamlaka ya maji pale iweze kujiendesha. Sina mashaka nao. Zaidi ya hilo, nawapongeza, wanatusaidia kwa sehemu kubwa sana ukiachilia mbali eneo hilo la mradi wa maji vijijini, sehemu nyingine tunaenda vizuri na wametusaidia sana.

Mheshimiwa Spika, niwashukuru kwa zaidi ya shilingi bilioni tano walizotutengea kwa mwaka huu kwa ajili ya kuongeza mtandao. Ni jambo jema, lakini bado naomba with a serious note, kwenye hili eneo la Mradi wa Kazilankanda, watusaidie huu mgogoro wa umeme tuondokane nao ili wananchi wa Ukerewe wa-enjoy matunda ya kazi inayofanywa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyedhamiria kuondoa shida ya maji kwenye jamii yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na hayo machache, nashukuru sana kwa nafasi. Mwenyezi Mungu akubariki sana. (Makofi)