Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa niweze kuchangia machache kwenye Wizara hii pamoja na kutoa ushauri wangu ili kuweza kuboresha huduma hizi za maji safi na maji taka. Naomba nianze kwanza kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kuweza kutekeleza miradi mingi ya maji na kuipa kipaumbele sekta hii muhimu kwa wananchi wetu. Vile vile nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa maono yake na moyo wake dhabiti alioonesha kwa ajili ya kumtua mama ndoo kichwani. Niwapongeze Wizara hapa, maono haya wao ndio wanayatekeleza kwa kiasi kikubwa, niwapongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pongezi hizi ziende sambamba kwenye Serikali ya Mkoa wa Arusha ikiongozwa na Ndugu John Mongela pamoja na viongozi wote wa Chama cha Mapinduzi wa Mkoa wa Arusha, wamekuwa wanaipa miradi hii kipaumbele na wamekuwa wakiifuatilia kwa karibu sana kuhakikisha inatekelezwa kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi, juzi tu hapa Mkoa wangu wa Arusha tumepokea mtambo mkubwa wa kuchimba visima virefu. Kwa ajili ya kuweza kutatua matatizo ya maji hususan kwenye maeneo ambayo yana shida ya vyanzo vya maji kama Wilaya ya Longido, Monduli, Ngorongoro, Karatu na sehemu zingine ambazo zina shida ya changamoto za maji. Shukrani zangu hizi ziende sambamba pia tumekamilisha Miradi 10 ya Maji Vijijini hadi kufikia mwezi Februari. Katika Wilaya ya Monduli kuna Mradi mkubwa wa Maji wa Meserani Bwawani umekamilika mwezi Februari, lakini katika Wilaya ya Arumeru pia kuna miradi takribani nane imekamilika Februari, 2023. Katika Wilaya ya Karatu pia kwenye miradi hii ya maji vijijini, Mradi mmoja wa Gidbasso umekamilika. Vile vile Serikali yetu haijaishia hapo, kuna miradi miwili ya maji katika Wilaya ya Ngorongoro ambayo inatarajia kukamilika mwezi Juni, 2023. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nianze na hali ya upatikanaji wa maji pamoja na takwimu hapa za upatikanaji wa maji alizotupa Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake. Waziri amesema hapa, hali ya upatikanaji wa maji vijijini imeimarika kutoka asilimia 70.1 hadi kufikia asilimia 77, lakini mijini imeimarika kutoka asilimia 84 hadi kufikia asilimia 88. Kama alivyosema Mheshimiwa Waziri huu hapa ni wastani tu na takwimu hizi zimekaa kiujumla mno. Namwomba Mheshimiwa Waziri kama ataweza kutupatia mchanganuo wa takwimu hizi ili tupate kiwilaya ili tujue hali halisi ya upatikanaji wa maji kwenye majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu kuna maeneo mengine ya Mkoani Arusha, ina asilimia sifuri kabisa ya upatikanaji wa maji. Naomba nimweleze tena Mheshimiwa Waziri hapa, anayejua hali ya mgonjwa ni yule anayemuuguza na mimi kama Mwakilishi wa Mkoa wa Arusha, ndiyo nakaa wananchi wangu na najua hali halisi ya upatikanaji wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafahamu vizuri wewe ni mama na una huruma sana, ukienda kwenye baadhi ya vijiji katika Mkoa wa Arusha, kwa mfano Longido, ukienda Noondoto, Kisilya, Mundarara, Wosiwosi, utalia kwa jinsi akinamama wanavyopata shida kutafuta maji. Wanatembea zaidi ya kilometa 30 kwenda kutafuta maji. Sio maji salama tena, kutafuta maji ambayo wakishayapata wana–share na mifugo. Maji hayo wanachangia na punda, wanachangia na ng’ombe na aina nyingine ya mifugo. Binafsi nimetembelea maeneo haya na nimeona hali halisi ya maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, ukienda Monduli Lepurko, Naalarami hali ni hiyo hiyo. Kwa hiyo naomba sana Waziri pamoja na Wizara, basi waweke kipaumbele sehemu zile ambazo zina asilimia chache ya upatikanaji wa maji, basi na wao pia asilimia ziongezeke ili twende nao sambamba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo napenda kuchangia mchana wa leo ni kuhusiana na uvunaji wa maji. Kamati imeshauri vizuri sana. Serikali lazima iongeze juhudi katika kuweka miundombinu ya uvunaji wa maji, lakini iwaelimishe wananchi pia kuhamasisha wananchi wetu kwenye suala zima la uvunaji wa maji. Kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri hapa amesema vizuri kwamba katika mvua zilizonyesha hivi karibuni Kanda ya Kaskazini imeongoza kwenye wastani hadi kufikia milimita 1,350. Mvua hizi zimeleta madhara makubwa sana kwa wananchi wa Mkoa wa Arusha. Zimeharibu miundombinu na vile vile zimeleta mafuriko makubwa na hivyo kupelekea vifo kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nitumie fursa hii pia kuwapa pole wananchi wangu wa Mkoa wa Arusha walioathirika wote na kadhia hii, lakini Mheshimiwa Waziri ataona hapa tungekuwa na miundombinu mizuri ya uvunaji maji, haya yote yasingetokea. Naomba sana niungane na maoni ya Kamati, Serikali iongeze juhudi kuweka miundombinu hii ya uvunaji wa maji ili maji haya yaweze kuwasaidia wananchi wetu pia kipindi cha kiangazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee suala lingine la usambazaji wa maji; katika Mkoa wa Arusha kuna mradi maarufu na mradi mkubwa sana wa bilioni 520. Waziri ametuambia mradi huu umekamilika kwa takribani asilimia 92 hadi sasa, lakini kuna baadhi ya maeneo mradi huu unapita maji hayajasambazwa, Kamati pia imeshauri jambo hili. Mradi huu unapita Wilaya ya Arumeru lakini ukienda Nduruma maji hamna. Kwenye Jiji la Arusha mradi huu upo, lakini kuna sehemu kama Terrat maji hamna. Kwa hiyo, naomba nimalizie, niombe Wizara iweke kipaumbele maeneo yote ya miji na vijijini, sehemu ambayo mradi unapita basi waweze kuwapa kipaumbele wananchi wa pale kwa kuwapa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)