Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi ya kuchangia. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu ambae amenijalia afya na nguvu za kuendelea kuwatumikia mabosi wangu wananchi wa Jimbo la Kyerwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, kuona ile ndoto yake ya kuwatua wakinamama ndoo kichwani inatimia. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Aweso, Mdogo wangu pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu, kwa kazi kubwa mnayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa najaribu wakati mwingine unapopata nafasi watu hawa wanaofanya kazi vizuri unaenda mbele ya Mungu kuwaombea. Wakati ninaomba kwa ajili ya Mheshimiwa Aweso pamoja na timu yake nikawa najaribu kumuuliza Mungu, hawa watu yaani ukija kuwangalia nia yao, kusudio lao ni moja yaani wamejipanga vizuri. Ukienda kwa Mheshimiwa Aweso, ni mnyenyekevu mpole, ukienda kwa Naibu Waziri hivyo hivyo, ukienda kwa Katibu Mkuu, hivyo hivyo, ukienda kwa Ndugu yangu Bwire, hivyo hivyo lakini hatujaishia hapo hata hawa watumishi mliowaweka mikoani ndugu yangu Warioba anafanya kazi nzuri pamoja na Tungaraze wanafanya kazi vizuri sana ndio maana mnaona haya mafanikio makubwa tunayoyasema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine tunapokuwa tunasifia, tunasifia kwa sababu vitu vimefanyika. Ninataka nieleze kwa upande wa Kyerwa. Miradi inayoendelea upande wa Kyerwa baada ya kukaa na Mheshimiwa Aweso na Katibu Mkuu pamoja na wasaidizi wake nikawaomba sana na ninakumbuka maneno uliyoniambia Mheshimiwa Aweso, ukaniambia hutakuwa kikwazo kutupatia maji wananchi wa Jimbo la Kyerwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye kata ya Murongo, kuna mradi wa milioni 589 mradi huu umekamilika, ukienda kwenye Kata ya Mabira, tuna mradi wa bilioni 768 mradi huu tenda imetangazwa na wiki ijayo mkandarasi anakabidhiwa Mradi. Ukienda kwenye Mradi wa Kata ya Nkwenda, Iteera mpka Rwabwere, Mradi wa bilioni 4 na milioni 600, mradi huu unaendelea vizuri na uko kwenye asilimia 75. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye kata ya Kimuli, mradi wa bilioni 2 milioni 116 unaendelea vizuri. Ukienda kwenye Kata ya Kaisho, Isingiro na Rutunguru, mradi wa bilioni 1 na milioni 900 mradi unaendelea vizuri, tukienda kwenye Kata ya Rwabwere, mradi wa milioni 738 umekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Aweso, ninakushukuru sana maana nilikusumbua sana lakini ukasema hautakuwa kikwazo ni hakika maneno yako nimeanza kuyaona. Mungu akubariki na ninasema kama mtumishi wa Mungu kama Mungu wangu aishivyo hatakuacha wala kukupungukia wewe pamoja na timu yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru, pamoja na kupongeza hawa watu namna walivyojipanga, ukiangalia hata wakandarasi wanaowaleta ni wakandarasi ambao wako makini. Mkandarasi mliyempa mradi kule Kyerwa anaitwa JAMTA, mkandarasi huyu ameanza kufanya kazi hata kabla hajaanza kulipwa. Ukiangalia miradi yote inayoendelea yuko karibu asilimia 80 lakini angalia alipolipwa ni kwenye kama asilimia 40 au asilimia 50. Wakandarasi wa namna hii tuwalinde na tuendelee kuwaunga mkono na kuwapa miradi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, tumekaa tena na wewe, Katibu Mkuu lakini pia Waziri wa Fedha. Tunao mradi ambao unakwenda kuhudumia Kata ya Kyerwa, Kata ya Nyaruzumbura, Kata ya Nyakatuntu, Kata ya Kitwe, Kata ya Bugara, Kata ya Kikukuru, Kata ya Kitwechenkura. Mradi huu unahitaji fedha nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekuomba na tumekaa sana na Mheshimiwa Waziri wa Fedha, mmenihakikishia mradi huu unakwenda kuanza na nimeuona kwenye bajeti mmeuweka. Niombe sana kama ambavyo umekuwa msaada, umekuwa mtu wa karibu kwa wana Kyerwa wewe pamoja na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na wasaidizi wako. Nikuombe mradi huu tunapomaliza bajeti uweze kuanza ili wananchi wa Kata hizi ambazo nimezitaja na wao waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu Kyerwa mnaweza mkaona ni miradi mingi. Kyerwa tulikuwa mbali sana hatukuwa na miradi, miradi mingi ambayo walikuwa wanapigia mahesabu ile miradi ya zamani. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri, miradi hii iweze kukamilika ili wananchi wangu, mabosi wangu wa Jimbo la Kyerwa na wao waweze kupatiwa maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, kitu kingine ambacho nilikuwa nataka nishauri Serikali, ukija kuangalia Mkoa wa Dodoma ni Mkoa ambao tunatumia maji ya kuchimba. Lakini maji haya ni maji ya chumvi, ni maji kiasi gani tunayoyapoteza? Maeneo mengi Mkoa wa Dodoma mafutiko ni mengi. Mheshimiwa Aweso, sisi tunakuamini pamoja na timu yako, hebu angalia ni namna gani tunaweza tukavuna maji yanayopotea ili wananchi wa Mkoa wa Dodoma waweze kupata maji, yanaitwa maji safi, maji laini? Yale maji ambayo sio maji chumvi. Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo, niombe sana hili uliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine wameeleza hapa Wabunge, Wizara ya Maji madeni ni mengi mnayodai. Kwa nini msije na mfumo wa mtu kulipia kama tunavyolipia umeme akalipia maji ili kuondoa hii adha ambayo mnaipata ya madeni kuwa mengi? Lazima tuje na ubunifu, mwananchi anakwenda analipia akishamaliza kulipia ndio anapata huduma ya maji. Vinginevyo, Mheshimiwa Aweso, hawa watu wataendelea kukukwamisha pamoja na Waziri wa Fedha. Tunataka tupate pesa hii ili pesa hii iende kuwasaidia wananchi wengine maeneo mengine ambayo bado hawajapata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, nikushukuru tena na nikutakie kila la heri. Lakini ndugu zangu niwaombe, pamoja na hawa watendaji kufanya kazi nzuri hebu tumkumbuke Rais wetu ambae kwa kweli anafanya maajabu katika nchi hii. Tumuombee kwa Mungu ili Mungu aendelee kumlinda, aendelee kumpa afya njema ili aendelee kuwatumikia watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)