Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu katika Wizara ya Maji, Wizara ambayo ni muhimu katika ustawi wa maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuhakikisha kwamba, huduma ya maji inaendelea kuboreka nchini, lakini nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Sisi Wabunge tumekuwa mashuhuda nadhani kwamba, kila Mbunge anaponyanyuka anampongeza Mheshimiwa Aweso na wasaidizi wake na watendaji wote katika Wizara yake, nami nifanye hivyo.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii, cha kwanza nieleze Bunge lako tukufu kwamba, chanzo cha maji katika Mto Ruvu ambao ndio juzi katika semina tulielezwa pale na Mheshimiwa Waziri kwamba, asilimia 76 ya uchumi wa viwanda katika Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani unategemea Bonde la Mto Ruvu. Mto Ruvu unaanzia katika Mto unaoitwa Mbezi unaanzia katika Kata ya Kibogwa, lakini vilevile kuna Mto Mfizigo ambao unatoka kwenye Kata ya Kibungo Juu, kuna Mto Mvuha unatoka Kata ya Bungu, kuna Mto Dutumi unatoka Kata ya Kolelo, lakini kuna Mto Mngazi unatoka Singisa na kuna Mto Mgeta Kafa unaotokea huko huko Singisa. Mtiririko wa maji hayo ndio unaofanya kwamba, ustawi wa Mto Ruvu ukamilike na wenzetu wa Dar es Salaam waendelee kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina simanzi kidogo, sisi ambao ndio tunatunza vyanzo vya maji, lakini sisi tunashindwa kupata maji. Sisi tunaotunza vyanzo hivyo vya maji, sisi ndio hatupati maji, tunaendelea kupata miradi midogo midogo ya milioni mia tatu, mia nne, mia tano, mia sita, lakini unakuja kuangalia wenzetu ambao wanafaidika kwa sisi ambao tumewatunzia wanatengewa miradi mikubwa. Mheshimiwa Waziri nakumbuka alikuja jimboni nilimweleza, tuna mradi unaoitwa Kibana Group Water Project ambao ulikuwa unahitaji bilioni 7.8, aliniahidi kwa kujua umuhimu kwamba, sisi ndio tunaomtunzia maji, aliniahidi kwamba, kama tutashindwa kufanya kwa wakati mmoja, basi atanifanyia walau kwa awamu mbili, angenipa bilioni nne baadaye angenipa bilioni tatu mradi huo ukamilike.

Mheshimiwa Spika, katika kitu cha kushangaza na kuumiza sana kwa wananchi wa Morogoro Kusini, Halmashauri ya Morogoro, ndani ya bajeti tukaonekana kwamba, mradi huo haufanyiki. Nilienda ofisini kwake na watendaji wangu akaniahidi kwamba, tutaufanya na akasema twende tukaweke fedha, walau token, ili mradi ukamilike. Imewekwa milioni 200, nimwombe Mheshimiwa Waziri, tafadhali sana sana tunauhitaji Mradi wa Kibana ili wananchi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi huu ukikamilika unahitaji fedha ndogo, kama tunaweza kupeleka Dar es Salaam mabilioni kwa billions of money, juzi kwenye semina unaangalia kuna mahali kuna watu wanapata bilioni 90, kwa nini sisi watu wa Morogoro Kusini? Kwa nini sisi watu wa Halmashauri ya Morogoro tusipate mradi wetu huo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sitaki kusema kwamba, nitakamata shilingi, lakini naamini Waziri ni mtu mwenye hekima, ana busara. Tumekaa na watendaji wake, lile jambo ambalo ameliahidi wakati ana-wind up naomba aje athibitishe ndani ya Bunge kwamba, tutapata maji au hatupati kupitia mradi wetu wa Kibana ili wananchi wangu wa kata nne, vijiji 12 wakapate huduma hiyo ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine kuna Mradi wa E-Water, kuna wadau wamekubali kuweka bilioni 1.5 ili Vijiji vya Mirengwerengwe, Kijiji cha Mngazi na Dakawa waweze kupata huduma ya maji. Watu hawa wanachotaka ni commitment ya Serikali na kutupa kibali, ili watumbukize fedha hiyo, wananchi wapate maji na mradi huu ni mradi ambao utakuwa unarudisha fedha. Katika makubaliano na vijiji hivi ninavyovitaja na wananchi tumekubaliana kwamba, ndoo itauzwa kwa shilingi 100. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, watupe hicho kibali, hawa wadau wakatumbukize fedha za maendeleo, wananchi wapate huduma hiyo, lakini kama wanadhani kwamba, kwa mujibu wa Sera inapingana, basi tunaomba watupatie hiyo bilioni 1.5, wananchi wangu hawa wakapate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine nizungumzie Bwawa la Kidunda. Niipongeze Serikali kwa ujenzi wa Bwawa la Kidunda kwa sababu, ujenzi wa Bwawa la Kidunda ndio itakuwa suluhisho la uhakika wa upatikanaji wa maji safi na salama Dar es Salaam. Naomba nitoe angalizo kwa Wizara, tunaenda kutumbukiza fedha nyingi kwenye mradi huu, ni vizuri tukaangalia uhifadhi wa mazingira. Mkoa wa Morogoro una bahati ya malisho, una bahati ya maji. Matokeo yake kipindi cha kiangazi wafugaji wanavamia vyanzo hivi nilivyovitaja vya Mto Ruvu na kuweza kukausha maji katika Mto Ruvu.

Mheshimiwa Spika, sasa nimwombe Waziri kupitia DAWASA, kupitia Bonde, tukaangalie jinsi gani tunaisaidia Halmashauri ya Morogoro Vijijini na Ofisi ya DC katika kutunza vyanzo hivi vya maji. Haiwezekani tunatoa hela sisi kama Halmashauri za own source kwa ajili ya kutunza maji ambayo yanakwenda kupata uhifadhi Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna Mradi wa Umwagiliaji wa Kongwa Turo. Mwaka jana, mwaka juzi, ulifungwa wakati water right users wanalipia, lakini unafungwa kwa ajili watu wa Dar es Salaam wapate maji. Kwa hivyo, nimwombe Waziri nahitaji watu wangu wapate nao kutumia maji hayo ambayo wanayatunza, lakini vilevile tunaomba uhifadhi wa mazingira ufanyike ili kuweza kulitunza hilo Bwawa la Kidunda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine, watu wa DAWASA, mwaka jana wakati tunachangia bajeti, kuna mambo ambayo ni ya msingi kwa wananchi wangu wa Kata ya Serembala, bado hawajapata toka tumekubaliana wakati tunakubali kuhama ili kupisha ujenzi wa bwawa. Kuna makaburi yao hawajalipwa, kuna Kituo cha Polisi hakijajengwa, kuna maji hayajakwenda; nimwombe Mheshimiwa Waziri wakati ana- wind awaambie watu wa DAWASA, tunataka tumalizane kwa pamoja. Nilimwona Mtendaji wa DAWASA akaniambia kwamba, anasubiri tutakwenda.

Mheshimiwa Spika, tarehe 15 tunakabidhi Mwenge, kama Mkoa wa Morogoro. Mheshimiwa DC wangu yuko tayari, mimi Mbunge na mdogo wangu Mheshimiwa Tale tuko tayari, tunataka twende tukamalizane, ili kusudi mradi huo uanze. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nimwombe Mheshimiwa Waziri, jana hapa mdogo wangu Mheshimiwa Tale alisema, sisi tunatengeneza hilo bwawa kwa wenzetu wa Pwani na Dar-es-Salaam wafaidike. Tunataka na sisi bwawa hili litusaidie kwa vijiji jirani, lakini maji ikiwezekana yafike Mvuha kwenye Makao Makuu ya Halmashauri yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)