Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa; na nianze moja kwa moja kwa kumpongeza sana Waziri wetu wa Maji Mheshimiwa Engineer Jumaa Aweso, Mheshimiwa Engineer Mahundi, Katibu Mkuu Kemikimba na nisiwasahau wale watendaji wetu kule mkoani Engineer Munishi, Kija Limbe, Mussa Msangi wa Wilaya, na kwa namna ya pekee Engineer Mussa wa Mfuko wa Maji. Ninawashukuru sana kwa jinsi ambavyo mnatusaidia kule Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Spika, pongezi zangu za pili kwa Rais wetu. Mama ana nia thabiti ya kuwatua akina mama wenzake ndoo kichwani. Nasema hivyo kwa sababu tunaona bajeti ya Wizara ya maji imeongezeka kutoka shilingi bilioni 705 kwenda shilingi bilioni 756 kwenye bajeti inayokuja. Na ile ya maendeleo imeongezeka kutoka bilioni 657 mpaka 695. Hizi zote ni Juhudi za Mama, juhudi nzuri, moyo mzuri, nia njema ya kuwasaidia akina mama.

Mheshimiwa Spika, katika miradi ambayo Wizara ya Maji itatekeleza, nitachangia zaidi kwenye mradi ya maji vijijini. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu wametenga pesa ya kutosha kabisa. Asilimia 72 ya fedha zote za maenedeleo ambazo ni shilingi bilioni mia tano na, zinakwenda kujenga miradi 1,546 vijijini, kuhudumia zaidi ya wananchi milioni 13. Hili ni jambo zuri kusema ukweli. Sasa baada ya kusema hayo, katika bajeti hii, ukienda kwenye ukurasa wa 262, kule moshi vijijini Mheshimiwa Waziri na timu yake wametukumbuka vizuri. Tunakwenda kujengewa chanzo cha maji na kuweka mitandao ya bomba kwenye mradi wa Kilema-Okaoni ambapo wametenga shilingi bilioni 204, tunashukuru. Mnakwenda kupanua mradi wa Tema, Shishamaro na Uru Shimbe ambako mmetenga shilingi milioni 699. Mnakwenda kuboresha mfumo wa mradi wa maji katika chanzo cha Urunduma ambao utapeleka maji katika Kata za Okaoni na Kibosho Kati, mmetenga shilingi milioni 300, tunashukuru; na mmetenga shilingi 69,000,000 kwa ajili ya kufanya usanifu na kugundua vyanzo vipya vya maji katika maeneo ya Tema, Shishamaro na Uru Shimbwe, tunashukuru kwa hili.

Mheshimiwa Spika, sasa, ili tufikie ile azma na sisi watu wa Moshi Vijijini tuwe na asilimia 85 naiomba Wizara inisikilize na inisaidie kwenye mambo yafuatayo. Katika kata ya Uru Kusini kuna wakazi 31,000, na kuna miradi mitatu ya maji ambayo ni mradi wa Mang’ana, Kisimeni na Mbora. Kwenye kata hii zipo taasisi nyingi za Serikali ikiwemo Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Mwenge. Katika miradi hii niliyoitaja maji ni kidogo na mabomba mara nyingi yako tupu. Tunamuomba Mheshimiwa Waziri na timu yake watuletee mradi wa kuongeza maji kwenye hii miradi mitatu ili hii kata ambayo ina watu wengi sana kule kwenye jimbo langu wapate maji ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, kata ya pili ni Kata ya Arusha Chini ambako ina wakazi kama 13,900 hivi, na kwenye kata hii Vijiji vya Mikocheni na Chemchem hakuna maji, badala yake wanahudumiwa na mradi wa Kirua Kahe ambapo watu wanapeleka maji kwa punda, kwa trekta kusaidia hivi vijiji. Ni kweli hawa watu wa Chemchem na Mikocheni wana shida. Kutokana na uhaba huu kuna mito inapita pale karibu, tunamuomba Waziri ikiwezekana mtujengee miradi hata kutoa kule mtoni tuje tutibu yale maji tuwape watu wa hii kata wapate maji kama Watanzania wengine.

Mheshimiwa Spika, kata ya Old Moshi Magharibi kuna mradi mkubwa wa Tellamande ambao namshukuru Waziri mkuu alikuja akaufungua. Maji ni mengi na yanapasua mabomba. Lakini eneo la Old Moshi Magharibi katika vijiji vya Mandaka Munono na vitongoji vya Sanindo hakuna maji. Tunaomba tu MUWSA wapeleke maji kwa kutumia chanzo hiki hiki au RUWASA watusaidie kutumia chanzo hiki ili hawa watu na wao wapate maji ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, katika kata ya Uru Kaskazini ambako kuna watu elfu kumi mia nane naa kuna chanzo kizuri cha maji ambacho kinatoa maji Uru Kaskazini kuyapeleka Uru Kusini na Kata ya Pasua kwenye Manispaa ya Moshi Mjini. Lakini wale watu wa Uru Kusini Vijijni vya Njari na Msumi hawajaunganishwa kwenye huu mfumo wa maji na maji yanataoka kwao. Nikuombe chonde chonde Mheshimiwa Waziri tuangalie hawa watu kwa sababu maji yanatoka kwao, watakuwa walinzi wazuri wa hii miradi, na wao waunganishwe katika huu maradi.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Kimochi, ina watu 16,000. Tunaishukuru Serikali ilitupa milioni 500 na MUWASA bado wametupa ili kuboresha mfumo wa maji katika maeneo haya. Lakini bado vijiji vya Sango, Shiha na Kisaseni havijapata maji. Tunaomba Mheshimiwa Waziri utusaidie katika hili.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa ni Kata ya Mabogini ambayo ina watu kama 56,000, na ndiyo kata kubwa kabisa na yenye watu wengi kuliko zote katika Mkoa wa Kilimanjaro. Niombe sana, nashukuru Serikali mlitupa shiling milioni 500 tukawajengea miradi ya maji, maana kuna vijiji vilikuwa havijapata maji tangu tupate uhuru. Niombe, kwenye Viijiji vya Mabogini kwenye Kitongoji cha Sanya Line D, Vijiji vya Muungano, Vitongoji vya Mwamko, Umoja, Uru, Relini, Kijiji cha Chekereni, Kitongoji cha Chekereni, Kijiji cha Maendeleo, Kitongoji cha Uarushani na Kijiji cha Mtakuja kitongoji cha Upareni, Kijiji cha Mserekia, Kitongoji cha Remiti, wanahitaji maji.

Mheshimiwa Spika, namuomba sana Mheshimiwa Waziri ni kijana mchapakazi Pamoja na timu yako. Mimi ukinitendea haya utakuwa umewatendea watu wa Jimbo la Moshi Vijijini haki, na tutaendelea kuwaombea daima.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo machache naomba kuunga mkono hoja.