Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa upendo mkubwa kwa wananchi wa Jimbo la Ludewa na Watanzania wote, kazi zake tunaziona. Sambamba na hilo, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maji na Mheshimiwa Dada yangu Naibu Waziri wake, hongera sana, kazi zenu ni nzuri na zinaonekana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Ludewa akifika kiongozi au Mheshimiwa Mbunge akienda kuwatembelea wana kawaida za kuandaa nyimbo zao za utamaduni, kuna nyimbo na ngoma za asili, wanaimba, wanacheza na wanakueleza mambo mazuri ambayo Serikali imefanya kupitia kwako Mbunge na mambo ambayo bado hayajafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilivyokwenda Kijiji cha Kisaula na Kijiji cha Lutala, wananchi walibeba maji machafu kwenye makopo wanacheza ngoma wakawa wanaomba maji, wanaomba sana. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kumuomba sana Mheshimiwa Waziri. Ninakushukuru ulimtuma Naibu Waziri alikwenda kule akawaahidi wale wananchi wa Lutala kwamba ule mradi wa Iwena ambapo Serikali ilifanya kazi nzuri sana, mradi wa bilioni moja na milioni mia mbili, kuna matenki mawili ambapo maji yanamwagika, Mheshimiwa Naibu Waziri aliwaahidi wananchi wa Lutala kwamba ule mradi utakuwa extended kwenda kuwahudumia wale wananchi wa Lutala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuishukuru sana Serikali kwa dhamira hii njema kuwakomboa wale wananchi, kwa kweli wapo kwenye changamoto kubwa sana, ule mradi unaweza pia ukahudumia na pale Kisaula, ni muhimu sana. Kwa sababu Jimbo la Ludewa lina tarafa tano, kuna hii Tarafa ya Masasi kidogo ina changamoto na inahitaji uangalizi wa karibu na msaada. Nilipanga kusema mengi lakini nashukuru Mheshimiwa Waziri nimekaa nae ameniahidi atakuja Ludewa kwa ajili ya kusaini mkataba wa mradi wa maji Ludewa Mjini wenye thamani ya bilioni saba. Kwa hiyo, naamini nitapata muda zaidi wa kuongea naye pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuishukuru sana Serikali kwa miradi mingi ya maji Ludewa. Tulipata bilioni 1.5 kwa ajili ya Mradi wa Maji Mavanga, tulipata bilioni moja kwa ajili ya mradi wa maji Mavala, tulipata bilioni 1.5 kwa ajili ya Mradi wa Kijiji cha Luvuyo, kule ambako na wenzetu wa Njombe wamechukulia maji pale Igongwi, tulipata milioni 900 kwa ajili ya mradi wa Lifua – Manda na miradi mingine mingi sana. Kwa hiyo, nipende kuishukuru sana Serikali. Niombe tu kwamba waendelee kuiangalia Ludewa kwa karibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo yako Mheshimiwa Waziri kwamba wakandarasi waweze kulipwa fedha naomba ulisimamie sana, maana yake pale Mawengi tulipata mradi wa bilioni mbili, umesinzia kidogo Mkandarasi alikuwa anadai fedha, mradi wa Mavala ulikuwa pia umesinzia kidogo. Kwa hiyo, maelezo yako hayo ya kwamba wale wakandarasi waweze kulipwa naamini yatakwenda kutengeneza furaha kubwa sana kwa wananchi wa Mavala. Hata ziara yako utakapokuja Mheshimiwa Waziri itakuwa yenye baraka sana, utakuta ngoma zile za asili za kioda na mganda zina ujumbe wenye furaha na kumpongeza Mheshimiwa Rais na Serikali kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Tarafa ya Mwambao, Kata ya Lumbila, Kata ya Kilondo, Kata ya Makonde, na Kata ya Lifuma. Hawa wananchi bado wanategemea maji kwenye asili (nature), wanakwenda kuteka Ziwa Nyasa. Ndiyo maana nilileta swali kuomba Wizara ifanye usanifu kuona ni jinsi gani wanaweza wakatumia maji ya Ziwa Nyasa kwa baadhi ya kata kuweza kuwahudumia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwamba mradi huu unaweza kuwa na gharama kubwa kwa sababu utahitaji pumping ya maji kwa kutumia umeme, ndipo yaweze kuhudumia wananchi. Tusiangalie gharama kwenye kuokoa uhai wa wananchi, kwa sababu anayepewa kazi ya kumpa mwanadamu maji, anapewa kazi ya kulinda uhai wa mwanandamu huyu. Kwa hiyo, naomba wananchi hawa kama wengine ambao tunashukuru, nao ifike siku waweze kutoa shukrani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna mamlaka ya bonde la Ziwa Nyasa, naomba sana waweze kufanya utafiti kwenye hili Ziwa kuangalia mabadiliko ya tabianchi, kwa sababu mwaka huu maji yameongezeka sana kwenye ziwa. Ukiongea na wale wazee wenye umri mkubwa, wanasema hali hiyo ilionekana mwaka 1976. Kwa hiyo, kwa kuwa wataalam wapo, watusaidie waweze kwenda kufanya utafiti tuweze kujua chanzo. Kwa sababu kuna historia, kuna mwaka nchi jirani iliwahi kufunga mto maji yakaleta shida kidogo. Kwa hiyo, ni vizuri tukajua ili tuweze kuwaeleza wananchi chanzo cha maji kujaa kwa kiwango kile: Je, ni mvua tu au kuna sababu nyingine, ili wananchi waweze kuishi kwa amani kando ya Ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hilo, niangalie huu mradi sasa wa pale Kipingu. Kijiji cha Kipingu kwenye Mto Ruhuhu kumekuwa na matukio ya wananchi kuliwa sana na mamba. Hivi sasa ninavyoongea, tunauguza mwananchi mmoja, na vifo vingi vimetokea kwa wananchi kukosa maji. Namshukuru Mwenyekiti wangu wa Mkoa wa Chama cha Mapinduzi, Mheshimiwa Deo Sanga na Mkuu wa Mkoa, Mheshimiwa Anthony Mtaka, walifanya ziara pale, waliweza kwenda kuwapa pole wananchi na kuwafariji. Kwa hiyo, waliahidi kwamba watashirikiana nami Mbunge, kuhakikisha wale wananchi wa Kipingu wanapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliongea na jirani zetu, Wilaya ya Nyasa, wanaweza wakachukua maji pale, inahitajika kama roll kumi tu, wakavusha kwenye daraja la Mto Ruhuhu tukaweza kuwasaidia wale wananchi wasiende kuteka maji kwenye Mto Ruhuhu. Isitoshe, maji ya Mto Ruhuhu siyo salama sana. Kuna uchimbaji mkubwa wa madini eneo la Amani kule, Ibumi, Nkomang’ombe, Lihugai, wanachimba sana makaa ya mawe na dhahabu. Kwa hiyo, yale maji siyo salama sana. Kwa hiyo, ni vizuri wale wananchi wakatafutiwa chanzo mbadala ili waweze kupata maji ya uhakika ili wajiepushe na magonjwa mbalimbali ambayo yatawagharimu sana uchumi wao. Fedha watakazozipata badala ya kwenda hospitali, basi zitawasaidia kufanya mambo mengine iwapo watapata maji salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba pia lile eneo la Mchuchuma na Liganga ambapo nimetoka kuishukuru sana Serikali kwa kushughulikia suala la fidia ambalo lilikwama, tunatarajia litakuwa na wananchi wengi sana. Pale Amani, Mundindi, namshukuru Mheshimiwa Waziri nimeona kwenye bajei ameweka mradi. Pale Njelela kulikuwa na tenki lita 100,000 ambalo kuna Padre alituletea, ila tulikosa mtaalam wa ku- survey maji na kuyaongoza yakafika kwenye tenki. Nakushukuru umetuletea Engineer mzuri sasa hivi, kwa kweli nakupongeza kijana, wananchi wana matumaini na mategemeo makubwa sana nawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, huu mradi ambao umeupeleka hapa Njelela na Mundindi, utakwenda kusaidia wawekezaji wale wa Mchuchuma na Liganga. Hata hivyo, mradi uliopelekwa bado ni mdogo, hauwezi kutosheleza idadi ya watu ambao tunawatarajia watakwenda eneo lile la Amani pale Mundindi, na eneo la Njelela. Kwa hiyo, kadhalika na kule kwenye makaa ya mawe, Mchuchuma, Makaa ya mawe yana athari. Ukisoma ripoti za kimazingira. Kwa hiyo, wananchi wanatakiwa wapewe maji mbadala. Kwa hiyo, wale wananchi wa Lifua, Liugahi, Nkomang’ombe, Malamba, nao wanahitaji wapewe maji mbadala na tuweze kuangalia idadi ya watu ambao watakwenda kuishi pale kutokana na uwekezaji mkubwa ambao Serikali inakwenda kuufanya pale. Halikadharika kule Liugahi iwapo wananchi wale watatumia maji yale ya kwenye mito ambapo makaa ya mawe yanatiririsha maji, ni hatari sana kwa afya zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja, na nina imani kubwa sana na Mheshimiwa Waziri, kwani ametutoa mbali. Alipotukuta na sasa kuna mabadiliko makubwa. Kule Ludewa tumepata miradi mingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naunga mkono hoja. Ahsante.