Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia fursa hii ili niweze kuchangia machache yanayohusiana na masuala ya maji.

Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Kwa kweli, kazi anayoifanya ni kubwa na sisi Watanzania na sisi Wanamtwara na sisi Wananewala tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema sisi Wanamtwara, sisi Wananewala? Ametoka kuongea hapa Mheshimiwa Hokororo akautaja Mradi wa Maji ule wa Makonde ambao ni mradi wa muda mrefu, uliasisiwa na watu wa Finland muda mrefu, ukachoka, ukawa hauhudumii wananchi ipasavyo, mabomba yalishachoka sana. Awamu kwa awamu tukawa tunaomba fedha ili mradi huu ukapate kuboreshwa, lakini ilishindikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Aweso amefika Newala akaliliwa na wazee, yeye mwenyewe ni shahidi, kwa kero ya maji ambayo wananchi wa Newala walikuwa wanaipata, lakini tunashukuru sana Serikali ikatupatia bilioni 84.7 kupitia Mradi wa Miji 28. Kwa kweli, tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa fedha tumezipata. Matarajio ya Wananewala, Wanatandahimba na watu wa Nanyamba ambako mradi huu unapita ni kwamba, wanachotaraji ni kuona mradi unatekelezwa ipasavyo, unatoa maji, ili wananchi wa maeneo niliyoyataja sasa na wenyewe waanze kutumia maji ya bomba, maji yaliyo safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kupeleka fedha hizo tunajua kazi zimeshaanza, maeneo ya kujenga matanki yameshaanza kusafishwa kwa kila eneo. Kwa mfano Newala, Newala Mji, pale Nambunga, Newala Vijijini, Nanda, Tandahimba, lakini pia na kule Nanyamba, tunatakiwa kuweka usimamizi wa dhati pamoja na kupeleka fedha kama usimamizi hautakuwepo, tija ya mradi hatutaipata. Sisi tunategemea kwamba, ifikapo Juni, 2024 wananchi wa maeneo yanayopitiwa na mradi huu waanze kunufaika na mradi huu, lakini tukiacha kusimamia ipasavyo matokeo hatutayaona. Ipo miradi ambayo tunaishuhudia kwa macho haisimamiwi ipasavyo, matokeo yake ni kwamba, huduma kwa wananchi hazifiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba mradi ukasimamiwe, lakini kusimamiwa huko kutategemea wale watu wa Makonde hawana gari la uhakika la kufuatilia huu mradi kwa uhakika. Niiombe Wizara, nilisikia kulikuwa na tetesi ya kupatiwa gari, watu wa Makonde wapatiwe gari ili waweze kusimamia vizuri mradi huo ukalete manufaa kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilikuwa lazima niongee kwa sababu, kupata fedha bilioni 84 kwa mkupuo sio jambo rahisi. Ni kazi kubwa sana ilifanyika mpaka na sisi tukawa wanufaika wa mradi huo. Mradi huu ili ukafanye kazi itakayoonekana vizuri na wananchi wote waweze kupata maji, ukienda kwenye Jimbo la Newala ipo miradi mingine ambayo kama itakamilika na kufanya kazi vizuri, basi tija ya mradi mkubwa huu itaenda kuonekana kwa wepesi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao Mradi wa Mlima Miuyu, upo unatekelezwa katika Jimbo la Newala Vijijini. Mradi huu ni wa muda mrefu. Ulikuwa ni mradi wa miezi tisa kuanzia mwaka 2018/2019, lakini mpaka leo haujakamilika na haujakamilika, inawezekana kuna changamoto za wakandarasi, lakini Wizara pia, hawajawakamilishia fedha. Mradi ulikuwa wa bilioni 1.3 lakini fedha ambazo zimelipwa ni milioni 614 pekee. Niiombe sana Wizara itafute kwa nini fedha hazijaenda, kama shida iko kwa wakandarasi tuwasimamie wakandarasi wetu, kama shida ni ya Wizara, Wizara pelekeni fedha na waje watuambie ni lini fedha zitaenda. Mradi wa miezi tisa wa 2018 mpaka leo tunaongea, hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu pamoja na mimi mwenyewe kwenye maeneo yetu, hatujawahi kuona maji ya bomba. Sasa hii miradi ambayo imeshaanza kwenda angalau basi, ikasimamiwe vizuri. Kwa kiasi fulani nashukuru kwenye huu Mradi wa Miyulu, angalau msimu wa mwaka jana, kaingazi cha mwaka jana, ile pressure kali, fedha ambazo tulikuwa tunalipa kule nyuma kwa ndoo ya lita 20 kulipa kwa shilingi 2,000, msimu wa mwaka jana ilipungua kwa sababu, angalau hii miradi kidogo ilikuwa inaanza kutoa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Mheshimiwa Waziri asimamie, kumbe inawezekana, mambo mengine ni masuala tu ya umeme, mara umekatwa, ukiuliza kwa nini fedha hazikupelekwa umeme ukirejeshwa maji yanatoka. Niombe sana, tusimamie, tuone tija ya miradi ambayo inakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, athari za kutopatikana kwa maji ni nyingi, ukienda leo Jimbo la Newala Vijijini pamoja na Newala Mjini, kuna miradi ambayo haikamiliki kwa wakati kwa sababu tu ya ukosefu wa maji. Mradi unapelekewa fedha, wananchi wako tayari kutoa nguvu zao, wanahangaika kumaliza maji kwenye visima. Kule kwetu kwa sababu ya changamoto ya maji kila nyumba inayojengwa inakua na kisima, tunavuna maji, lakini maji yale kwa bahati mbaya hayatibiwi, tunayatumia hivyohivyo, ni yale maji ya kuokota, ndiyo maji ambayo sasa inapotokea miradi kwenye kijiji wananchi wanajikusanya wanaenda kuchukua maji yao kwenye visima wanaenda kutekeleza miradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine yale maji yanaisha, kwa hiyo miradi unakuta haitekelezeki kwa wakati sahihi kwa sababu ya ukosefu wa maji. Tunakuja tunawalaumu sana Wakurugenzi wetu lakini wakati mwingine wana changamoto hiyo ya maji. Mheshimiwa Waziri tunaomba utusaidie, maji Newala sasa ije ibadilike historia, mmeshaanza kuandika hiyo historia kwa kupeleka fedha nyingi, tunaomba sana wananchi wa Newala nao wanataka kuondokana na kero ya maji, kuondokana na kero ya maji ya kuokota kwa kupatiwa maji ambayo yatatoka kwenye mabomba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo miradi mingine midogomidogo kwenye maeneo yetu. Miradi ambayo ikienda nayo kupelekewa fedha basi changamoto kubwa sana tutakuwa tumeipunguza Mheshimiwa Waziri wetu. Kwa mfano, kuna mradi wa usambazaji wa maji wa vijiji vya Mkudumba – Mnyengachi na Mdimba – Mnyambe – Mnima na Bahati. Pia upo mradi mwingine ambao unajumuisha Vijiji vya Mikumbi, Mkongi, Nyamangudu, Nangujane, Chirende, Mkomato pamoja na Lihanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii ipo kwenye mpango lakini tunaiombea sana ipate fedha. Kukamilika kwa miradi hii kutakuwa na sura nyingine ya Newala, sura ya Newala haitakuwa ile ambayo tumeizoea siku zote. Kuna watu wanarudi Newala wanakataa kufanya kazi kwa sababu ya shida ya maji. Mtu anafika Newala unatumia maji kwenye kile kikopo, kinaitwa kidosho, anapewa kile aoge, hawezi. Atakaa siku ya kwanza, mwezi wa kwanza anaondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji ni afya, maji ni uhai, magonjwa mengi yanatokana na ukosefu wa maji. Tunaipa Wizara ya Afya mzigo mkubwa wa kutibia wagonjwa, magonjwa ambayo kumbe yangeweza kuzuilika kama maji safi na salama yangeweza kupelekwa kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuombe sana Mheshimiwa Waziri, pamoja na mtani wangu Mheshimiwa Mahundi, chondechonde, tunaomba usimamizi na upelekaji wa fedha uende ili wananchi wa Newala wapate maji, tuigeuze Newala, maji Newala ni shida kwelikweli. Kila mtu atashangaa kama watayaona maji Newala kwa hali ya Newala jinsi ilivyo miaka yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi mvua zimeanza kukata tumeshaanza kupata hofu, kwa sababu kuna maeneo mvua hazikunyesha vya kutosha kwenye maeneo hayohayo ya Newala, kwa hiyo hata visima vyao vile vya asili havina maji. Kwa hiyo hapa sasa hivi mvua inavyoanza kukata tunaanza kupata hofu. Hivi sasa hivi mvua imekata tutaishije kwa miezi yote mpaka masika yaje, kwa sababu masika ndiyo mkombozi wetu, lakini kwa dunia ya sasa ilivyo kutegemea masika peke yake hapana Mheshimiwa Waziri. Tunaomba tuondokane na suala la kutumia visima, tuondokane na maji ya kuokota, wakati sasa umefika nasi tufaidi, tuone raha ya kutumia maji ya bomba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi yako, naunga mkono hoja. (Makofi)