Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko Mezani ya Wizara ya Maji. Nianze kwa kumpongeza kidhati Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya kwenye Sekta ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Bwawa la Kidunda shilingi bilioni 329.46 limesainiwa. Bwawa la Kidunda linaenda kuwa Suluhu ya upatikanaji wa maji ya uhakika kwenye Mkoa wa Dar- es-Salaam. Kazi hii ni kazi kubwa, Mheshimiwa Rais anastahili pongezi kubwa sana. Katika miaka yake miwili moja kati ya mambo makubwa aliyoyafanya ni kuhakikisha tunapata chanzo cha uhakika cha maji kwenye Mkoa wa Dar-es-Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kumpongeza kidhati Waziri wa Maji, Mheshimiwa Juma Aweso. Waziri huyu tukianza kutaja sifa zake hapa muda wangu utaniishia, niruhusu nitaje chache. Mheshimiwa Aweso ni mtu mnyenyekevu, Mheshimiwa Aweso ni mtu mpole, Mheshimiwa Aweso anafikika, Mheshimiwa Aweso ni Waziri ambaye ukikutana naye barabarani unaweza ukasema sio Waziri, hajakivaa cheo. Mtu hajapata cheo bali cheo kimempata mtu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo methali ya Kichina kwamba, kiongozi bora uongozi wake unaanzia nyumbani kwenye familia yake. Mheshimiwa Aweso huyu anaongoza familia mbili vizuri sana na ndio maana Wizara hii haimpi tabu. Sisi hatuna kubwa zaidi ya kumwombea dua; “Rabbana aatiina fii dduniya hassana wafil akhirat hassana.” Mwenyezi Mungu ampe neema yote ya hapa duniani na hata akhera, aendelee kufanya kazi ya kumsaidia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, amepata Katibu Mkuu mzuri, Engineer Nadhifa Kemikimba ni mtu aliyekulia kwenye Wizara ya Maji. Kama lile suala la institutional memory hapo ndio mahali pake. Mama mpole, mnyenyekevu ana sifa zote za utumishi wa umma. Tunaona timu hii inaenda kutekeleza ajenda ya kumtua mama ndoo kichwani kwa kiasi kikubwa na Ilani ya Uchaguzi itatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haitoshi pale Dar-es- Salaam tulikuwa na mtu bingwa kabisa, Engineer Cyprian Lwemeja aliyekuwa Mtendaji Mkuu wa DAWASA. Ingekuwa ni usajili labda sisi tungemkatalia kumsajili huku Wizara ya Maji, mtu bingwa, mtu mzuri, anacheza kama Aziz Ki alivyofanya leo pale Uwanja wa Taifa. Naibu Katibu Mkuu huyu naamini ataisaidia Wizara na Taifa hili katika kutekeleza kazi zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji kwenye Mkoa wa Dar-es- Salaam imefika asilimia 95, lakini kwenye Jimbo la Ukonga, jimbo ambalo ndio linaongoza kwa watu kwenye nchi hii, watu 921,957 tuko asilimia 57, lakini Serikali hii ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ziada ya ule mradi uliotoka Ruvu Juu ukapita Kibamba, ukaenda Kisarawe, ukaja pale Pugu, sasa kuna mradi mwingine kule Zingiziwa, Somelo, Ndiole Juu kwenda Msongola, lakini DAWASA wanaenda kutekeleza mradi mkubwa wa thamani ya shilingi bilioni 42, Kata ya Kitunda, Kata ya Kivule, Kata ya Mzinga, Kata ya Kipunguni mpaka kule Chamazi kwa Mheshimiwa Chaurembo na Temeke kwa Mheshimiwa Kilave, wanaenda kupata maji haya na sisi Jimbo la Ukonga tunaenda kufikia hii asilimia 95 ya maji kwenye upatikanaji wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hii kule naomba nichukue fursa hii vilevile kumpongeza Engineer Sirila, Mwanamama huyu Mhandisi, Meneja wa Wilaya ya Ukonga ya maji na Engineer Alex Wandu ambaye anahudumia Wilaya ya Kisarawe, lakini anahudumia maeneo ya Jimbo la Ukonga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme tu kwamba, kazi hii inayofanywa inaenda kuheshimisha Serikali ya Chama Cha Mapinduzi. Serikali hii iliahidi upatikanaji wa maji kwa asilimia 95 mijini, kazi inayofanyika bilioni 42 hizi za mradi mpya, bilioni saba zile za Mradi wa Pugu - Kisarawe, bilioni 11 za ule Mradi wa Somelo, bilioni 60 zinaenda kuwekezwa kwenye Jimbo la Ukonga ni kazi kubwa sana. Sisi watu wa Ukonga tunasema ahsante sana kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na kweli wali wa kushiba unaonekana kwenye sahani, bilioni 60 hili sasa ni sinia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hii ni kubwa, ninachomwomba Mheshimiwa Waziri mwaka 2021, amesoma Pugu kama mimi na amepata shida ya maji, no wonder anafanya kazi ya maji vizuri. Alikuja Mheshimiwa Rais akiwa Makamu wa Rais pale Pugu na alienda pale Pugu Secondary kuona maji yalivyofika kwenye shule ile ya historia ya nchi yetu. Aliahidi mradi ule atakuja kuufungua yeye mwenyewe. Tunaomba Waziri afikishe salamu zetu, tungefurahi kumwona anakuja kuzindua mradi ule wa maji maana ameahidi kufikia Disemba, 2023, Jimbo zima la Ukonga litakuwa limepata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mawili madogo ya mwisho, niwapongeze sana. Kama alivyosema Mheshimiwa Mabula, watendaji wote wa Wizara ya Maji, wako wengi, lakini ninaamini watendaji wengi wamepata unyenyekevu na uchapakazi kutoka kwa Waziri wao. Ukienda RUWASA ingawa haihudumii Dar es Salaam, Clement, Kivugalo Mtendaji Mkuu, ni mtu mwema hata alivyotambulishwa asubuhi niliona Wabunge wengi wakipiga makofi, aendelee na moyo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti wangu, Haji Nandule, CEO wa Mfuko wa Maji, amesema pale anafanya kazi nzuri. Ni watu ambao Mheshimiwa Aweso kwa ukaaji wake kwenye Wizara hii ametengeneza timu nzuri na anafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, itoshe kusema naunga mkono hoja. Naomba sana tupitishe bajeti hii kwa mikono miwili, ili kazi hizi za maji ziende zikamguse Mtanzania na kumtua mama ndoo kichwani, ahsante sana. (Makofi)