Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweke mchango wangu kidogo kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chanda chema huvikwa pete, hapa leo tunaona, toka tumeanza kuchangia Waheshimiwa Wabunge wote wanatoa sifa kubwa na shukurani kubwa nikiwemo mimi kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan, Waziri wetu mwalimu wa misemo mbalimbali ya kutufundisha na kutusaidia katika maisha Jumaa Aweso lakini pia Naibu Waziri wake Engineer Maryprisca pamoja na Katibu Mkuu Engineer Kemikimba lakini kiujumla wake kwakweli wizara hii watumishi wake wote wanajitahidi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo mambo mengi mazuri yameishachangiwa na Waheshimiwa Wabunge lakini kwa umuhimu wa wizara hii nashindwa kutoa jina langu inabidi niendelee kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona kwamba wizara imejitahidi kufanya shughuli mbali mbali za kiuwekezaji wa maji katika maeneo mbalimbali nami kwangu nawashukuru sana kwa mradi wa maji Wangingama, Litui group, Ngumbo group na nikiruka mradi wa Pururu Songa mbele ambao kidogo haujanifurahishwa haujaanza lakini kuna Liuli…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa inatoka wapi? Mheshimiwa Ester Bulaya.

TAARIFA

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nampa taarifa Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya kwa mchango wako mzuri apitie hapo kwamba Taifa linawakilishwa vyema, Young Africans wameshinda goli mbili bila. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Stella Manyanya unaipokea hiyo taarifa?

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mimi naipokea taarifa hii kwa sababu mimi ni Simba, lakini Yanga wamechukua jersey za CCM, kwa hiyo tunawapenda tu hata kama wakifanya vyovyote vile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba nilikuwa naendelea kushukuru kwa ajili ya mradi ambao utaendela pale Kilosa, Nangombo ambao utaenda mpaka Malinyi na Chihulu na miradi mingine michache itakayoendelea. Lakini kama ambavyo mwalimu amesema, ulitufundisha kwamba pilau la sherehe mvua ikinyesha huliwa wima. Sasa kwa mazingira hayo mimi sasa hivi nanyeshewa naomba nipate maji Mtupale, Chinyindi, Ruhangalasi, kata ya Lumeme, kata ya Mipotopoto, yaani eneo la Uhuru na Mipotopoto yenyewe, na Luhindo leo wamenipigia tena simu na kule Mseto Lipalamba, kote huko kuna shida ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiendelea katika masuala mengine yanayotuhusu kitaifa, pamoja na hizi shukrani nyingi nilizozisema. Tunamaliza Dira yetu ya Taifa ya Mwaka 2025. Dira hii ilisisitiza zaidi katika kuhakikisha kwamba Watanzania wanakuwa na Maisha bora, tuwe na jamii ambayo itakuwa na Maisha bora, lakini pia tuwe na amani, utulivu na umoja; utawala bora, jamii iliyoelimika na uchumi wenye ushindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mambo haya pamoja na kwamba tumeshaanza mchakato wa kuandaa dira mpya ya mwaka 2050 bado masuala haya ya msingi siamini kama yatatoka katika mtazamo wa dira hii ambayo tunaiandaa. Mambo hayo yote ili yaweze kutekelezeka kuhakikisha kwamba tunakuwa na uchumi ulio imara na wenye ushindani, kwa vyovyote vile suala la maji haliwezi kuwekwa pembeni. Na ndiyo maana sasa unakuta hata Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia suala la kuwa na Mpango kabambe ambao kwa Kingereza lugha nzuri ni hiyo Water Master Plan.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sana kwa sababu Pamoja na kwamba sasa hivi tunatafuta maji hapa lakini bado kuna haja ya kuangalia utoshelezi endelevu wa suala la maji katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisikiliza hapa watu wanavyoshukuru miradi inayotajwa. Utasikia tumepata bilioni arobaini, bilioni hamsini, bilioni ngapi, lakini kule kwangu mimi sihitaji bilioni kumi, nahitaji milioni milioni kwa sababu vyanzo vya maji viko vingi tunahitaji tu kuvuvta maji kufikisha pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo kama Simanjiro tulikoenda mara ya mwisho kukagua mradi. Mradi ni mkubwa sana lakini ukiangalia mradi ule umekuwa mkubwa kwa sababu ya kuhangaika kutengeneza vituo vikubwa, kusafirisha kwa umbali mrefu kwa sababu ya kutokuwa na vyanzo vya maji vya kutosha katika maeneo yanayohusika. Kwa misingi hiyo kwa nini tunataka kuwa na hiyo mpango kabambe wa kuona kwamba ni namna gani tunaangalia maji yetu kwa mbali lakini vile vile namna gani tunaweza kuunganisha hivyo vyanzo, hasa vyanzo vikubwa

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kuna mikakati mingi ya nchi ambayo yote kila Waziri hapo unaona anakuja anachemka, wa kilimo anachemka anasema anataka mashamba sijui ya aina gani, wa Kifugo anakwambia mimi nachemka anataka sijui ng’ombe wa aina gani. Wote hawa wanagombania maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa humo humo kuna kutumia dawa, humo humo kuna kutumia, kwamba hilo hilo bonde moja mwingine anatafuta maji ya kunywa, mwingine anatafuta maji ya kilimo, mwingine anatafuta maji gani. Matokeo yake tutajikuta kwamba tuna hali ambayo baadaye tutakuja kuanza kupigana sisi. Lakini vile vile tukumbuke kwamba tumeshaingia mkataba na umeanza kufanya kazi wa nchi za Afrika kuweza kufanya biashara pamoja; na ninaamini wengi watakuja kufanyia kazi Tanzania kwa sababu ndiko kwenye amani, kuna furaha na rasilimali nyingi ziko huku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama maji hayataonesha dira ya kuweza kutosha, kama maji hatutayawekea mipango maalumu, kama maji yatakuwa kwamba yoyote yule afanye analojisiskia, hiyo itakuwa ni changamoto kubwa sana. Kwa hiyo tunaona kwamba maadam tumeshtuka mapema, tuwaombe si kwamba walikuwa hawafanyi kitu kabisa, tunaboresha mipango ile ambayo tayari wanayo; tunaomba sasa hata katika mpango huu mkuu wa dira ya Taifa ya 2050 suala la maji lionekane vizuri kinagaubaga ili hata tunapoiangalia dira yetu nyingine pia ya 2063 zote hizo ziweze kuwa pamoja ikihakikisha kwamba Tanzania tunakuwa na usalama wa maji, Tanzania inakuwa ni nchi tuitakayo sawa mabavyo Afrika kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema hayo pia kwa kusisitiza hili suala la mfumo wa grid ya taifa ya maji, hayo yamefanyika. Kwanza Mungu mwenyewe ametuumba kwa mfano ambao hata mishipa ilivyounganishwa ndio hizo grid zenyewe, sivyo? Kwenye umeme tumeshaona, na mambo mengine mengine. Kwa hiyo tunaposisitiza suala la kuchukua maji kwenye maziwa yetu kwenye mito mikubwa na maeneo mengine hatumaanishi kwamba sasa tumpe pressure Waziri, kwamba kesho apate fedha za kufanya mambo yote haya kwa mara moja, tunachohitaji ni kuwa na mipango inayoonesha kabisa kwamba eneo hili nitachukua maji kwa muda fulani, lakini baada ya hapo nitatakiwa nichukue huku na huku. Ikifika muda niwe nimeshajiandaa kwa ajili ya kuingiza maji kutoka katika chanzo fulani, lakini pia kuhakikisha kwamba hata mtumiaji mwingine hajakiharibu kile chanzo. Kwa hiyo hizi Wizara zikae pamoja katika kupanga hiyo mikakati mwisho wa yote tuwe na mapango wa maji endelevu ambao utatuongoza huko katika dira kuu ya mwaka 2050 na maisha yetu yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hiyo, nilikuwa napenda pia kuwaomba wenzetu wa Wizara ya Maji kuangalia suala la upatikanaji wa maji kwa bei nafuu. Kwa upande kama TANESCO kuna umeme unapataikana wa gesi, kuna umeme unapatikana wa maji, kuna umeme unaptikana wa diesel ukijumlisha pamoja unakuta bei ya umeme inapungua, kwa hiyo wananchi wote wanapata bei ambayo inafanana. Sasa kitendo hiki cha kuwa na sehemu za upatikanaji wa maji kila eneo kivyake, na system ya mapato imekuwa kila watu kivyao matokeo yake kuna maeneo kunakuwa na bei kubwa sana za maji wakati maeneo mengine wana – enjoy maji kwa bei nafuu zaidi. Kwa hiyo iko haja ya kuangalia mfumo wetu wa ukusanyaji mapato iili uweze kutoa unafuu katika baadhi ya maeneo ambayo yanapata maji kwa gharama kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Stella Manyanya ulikuwa unataka kumalizia, muda wako kengele ya pili imelia.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Basi nizidi kushukuru na ninaunga mkono hoja.