Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Wizara ya Maji. Hii ni Wizara muhimu sana kama walivyotangulia kusema, uhai wa Taifa letu unategemea Wizara hii pia ya Maji kwa sababu ni muhimu katika kila sekta. Tukisema Ujenzi unagusa maji, tukisema nini kila kitu kinagusa maji, tukisema usafi, afya kila kitu kinagusa maji. Kwa hiyo ni Wizara muhimu sana kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchukua nafasi hii kuipongeza Wizara kwa namna ambavyo bajeti yake inatekelezeka. Tukiangalia katika suala zima la bajeti ya miradi ya maendeleo katika fedha zilizokuwa zimetengwa shilingi bilioni 657.899 fedha zilizotoka kufikia Aprili 2023 zilikuwa ni shilingi bilioni mia sita ishirini na tatu na milioni saba Hamsini na tatu na point. Kiukweli hii inatia moyo hata Wabunge tunapokaa hapa kupitisha bajeti kiuhalisia inatia moyo mpaka kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutia moyo huku bado kuna changamoto kubwa kwenye suala zima la usimamizi na ufuatiliaji wa miradi inayotekelezwa, hili ni tatizo kubwa sana kwenye maeneo yetu. Bajeti inapita huku inatekelezeka lakini ukienda kwenye suala la usimamizi na ufuatiliaji wa miradi inayotekelezwa kumekuwa kunasuasua sana. Hii imepelekea miradi mingi kutokamilika kwa wakati na wakati mwingine kutokwenda kwenye lengo sawa sawa na vile inavyokuwa imekusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Mji wa Tunduma pale sasa hivi utakuta kuna ma-tank ambayo yamepakwa rangi za kila aina, lakini hakuna maji. Utaona kuna miundombinu kila maeneo, ukifika utasema Mji wa Tunduma una maji, lakini ukienda kwenye uhalisia, wananchi wa Mji wa Tunduma asilimia kubwa hawapati maji safi na salama. Hii ni hatari sana. Wananchi wetu wanataka wanapoona yale ma- tank, wanavyoona miundombinu ya maji imetembea kila mahali, kitu kikubwa wanachokitaka siyo yale matenki, siyo mabomba yaliyopitishwa kila maeneo, wanachotaka ni uhalisia wa maji. Sasa tunataka tuone maji, tusione tu yale matenki ambayo yanabadilishwa rangi. Tunataka tuone uhalisia wa maji kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiuhalisia kama walivyosema Wabunge wengine wa Mkoa wa Songwe, Mheshimiwa Waziri kuna hatari ya sisi Mkoa wa Songwe kukimbia na Shilingi yako. Kiukweli. Kwa sababu uhalisia hakuna kata hata moja ndani ya Mkoa wa Songwe ambayo ina uhakika wa kupata maji safi na salama kwa uhakika, hakuna. Katika taarifa yako unasema kwamba hali ya upatikanaji wa maji vijijini ni asilimia 77, lakini ukienda Wilaya ya Momba, ukienda Halmashauri ya Mji wa Momba kuna vijiji 72. Kati ya vijiji 72, vijiji 28 tu ndiyo vyenye uhakika wa kupata maji. Kwa hiyo, napata shaka na hii asilimia 77, ni wapi? Ni wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapata shida. Karne hii ya leo watu wana-share maji na mifugo. Ukienda Momba…

MHE. CONDESTER M. SICHWALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wana-share maji na mifugo, ni kitu cha hatari sana.

MHE. CONDESTER M. SICHWALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

TAARIFA

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwongezee taarifa Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wetu wa Songwe, kwamba katika Jimbo la Momba kati ya vijiji 72, ni vijiji 22 tu ndiyo vinapata maji safi na salama ya kwenye bomba. Vijiji 50 havina maji. Kwa upatikanaji wa Jimbo la Momba ni sawasawa na asilimia 30 tu, lakini vijiji vilivyobaki 50 tunakunywa maji na nguruwe, punda, mbuzi na ng’ombe. Vijiji 50, na jambo hili linaendelea kushamiri.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Stella Fiyao unaipokea taarifa.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza taarifa naipokea kwa mikono miwili kwa sababu huo ndiyo uhalisia wa Jimbo la Momba. Ni hatari! Kwa karne hii, leo wananchi wana-share maji na mifugo! Ni jambo la hatari. Ndiyo maana typhoid kwenye Mkoa wa Songwe haziishi, maana ni hatari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri atakapokuja hapa, atuambie mkakati wake katika Mkoa wa Songwe ni upi, kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, tunataka tujue, tumeendelea kusema hapa, kila inapofika Wizara ya Maji tunachangia na tunasema. Mmeendelea kutuahidi kipindi kirefu kwamba maji yatatoka kwenye Mto Songwe huko Ileje, yatakuja Tunduma, yataenda Vwawa, yataenda Mbozi, leo hii mmetubadilishia mpango, mnasema maji yanakwenda kutoka Momba. Tunataka mtuambie, kwa sababu tangu mwaka 2019 mlisema tayari mmeshafuatilia na mmejua gharama za mradi, mradi utagharimu kiasi gani. Leo hii mmetubalishia mpango, mnasema maji yanakwenda kutoka Momba, yanaenda Tunduma, yanaenda Vwawa, yanaenda Mbozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Waziri atakapokuwa anakuja hapa atuambie, ni lini mradi huo utatekelezeka? Ni lini mradi huo utatekelezwa? Kwa sababu tumechoka kuimba humu, tumechoka kusema, tumechoka kuzungumza. Tuambieni ni lini mradi huo mkubwa utatekelezeka kwa ajili ya kukomesha tatizo la maji katika Halmashauri ya Mji wa Tunduma, Mbozi na Vwawa? Lini mradi utatekelezeka? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, bado tumeendelea kuimba, kuna mradi ambao unahudumia Kata ya Mpemba na Kata ya Katete. Mradi huu unatoka Ukwire Wilaya ya Mbozi kuja Halmashauri ya Mji wa Tunduma na unahudumia Kata hizo mbili, miundombinu yake ni mibovu. Miundombinu ilitengenezwa tangu mwaka 1971, mpaka leo kuna tatizo kubwa. Mradi huu ulikuwa unawakomboa sana wananchi wa Kata ya Mpemba na Kata ya Katete. Mheshimiwa Waziri utakapokuwa unakuja hapa, utuambie ni lini mtafanya ukarabati mkubwa kwenye mradi huo ili wananchi wa Kata ya Mpemba na Kata ya Katete waweze kunufaika na maji? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba, sisi watu wa Songwe tuangaliwe kwa jicho lingine. Tunachangia asilimia kubwa sana kwenye pato la Taifa, hebu tuangalieni kwenye suala la maji, tuondoleeni hizi changamoto. Ninaamini changamoto hizi zinatibika kama Mheshimiwa Waziri utaamua. Tusaidie wananchi wa Mkoa wa Songwe tuepushieni changamoto kubwa ya maji ambayo inaleta athari mpaka kwenye ndoa. Tusaidieni! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)