Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Christopher Olonyokie Ole-Sendeka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi ya kwanza kukushukuru wewe mwenyewe kwa kuniona na kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuja leo nilikuwa nauguza Muhimbili, lakini nikaona Wizara hii isinipite kwa sababu wananchi wa Simanjiro walinituma niseme maneno, nitakayoyasema. La kwanza, ni kuridhika kwa wananchi wa Wilaya ya Simanjiro kwa kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwamba mradi mkubwa wa maji ambao sijui naweza kusema sijui ni mradi wa kielelezo, wa kimkakati ambao ulibuniwa na Hayati Edward Moringe Sokoine mwaka 1974 alipokuwa akimkaribisha Hayati Rashid Mfaume Kawawa kuzindua Wilaya ya Kiteto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa mmoja wa vijana chipukizi waliokuwepo wakati wilaya ile ilipokuwa inazinduliwa. Hayati Edward Moringe Sokoine alisema pamoja na kwamba Kiteto hakuna maji pale Kibaya ambalo tatizo liko mpaka leo, Makao Makuu ya Wilaya yatajengwa Orkesumet na tutachukua maji kutoka Mto Ruvu, kilometa 45 mpaka 50 kuleta Makao Makuu ya Wilaya ya sasa ya Simanjiro ambayo ni Orkesumet. Mradi huu umetekelezwa na uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa vitendo na umekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri mwenye dhamana ya maji, Mheshimiwa Juma Aweso, wananchi wanamshukuru, wanampongeza kwa kazi nzuri kubwa aliyotufanyia. Wanampongeza kwa sababu yeye mwenyewe kwa kipindi cha Uwaziri wake, mimi nikiwa Mbunge katika kipindi hiki, amekuja pale zaidi ya mara sita, akihakikisha kwamba ule mradi unakamilika. Mara zote alipofika tuliona mabadiliko makubwa ya kukidhi kiu ya wananchi wa Jimbo la Simanjiro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie kwamba kazi inayofanywa na Mheshimiwa Waziri Aweso ni kazi ya kupigiwa mfano, ni kijana mnyenyekevu, kijana muadilifu, kijana mchapakazi na ni kijana anayejishusha. Natamani viongozi wote wa CCM tungeiga mfano wa Mheshimiwa Juma Aweso ambaye hanyanyui mabega, siku zote yuko down. Nalisema hili kwa sababu si sifa njema sana kwa kiongozi kwamba Mungu amekupa madaraka ukiwa na umri mdogo, lakini unasahau kwamba wewe una umri mdogo hata kama una madaraka makubwa, lakini Mheshimiwa Aweso anajua nafasi yake katika jamii hasa akiwakuta waliomzidi umri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati nzuri Mheshimiwa Rais amempa Naibu Waziri mzuri, Mheshimiwa Maryprisca Mahundi, anafanya kazi nzuri sana kwa kushirikana naye. Katibu Mkuu wa kupigiwa mfano, dada yangu Nadhifa Kemikimba, tangu amekulia kwenye Wizara ya Maji, nilimjua akiwa Mkurugenzi, nikamjua akiwa Naibu Katibu Mkuu amekuja kuwa Katibu Mkuu. Leo Wizara ile imekamatwa na viongozi ambao kwa kweli wanajua wajibu wao, wanawajibika vizuri na ni viongozi waadilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nasema leo kwamba, moja kati ya sifa ya kiongozi ni uadilifu na ndio maana huwezi kutenganisha uongozi wa umma na maadili kwa sababu sifa mojawapo ya kiongozi ni uadilifu. Kwa mafanikio haya tunayoyaona yanatokana na kazi nzuri ya uadilifu wa wale waliopewa dhamana katika Wizara husika. Kwa hiyo, nataka niwashukuru kwa mradi huo mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi mkubwa pia wa pili ambao ni wa Mji wa Arusha ambao unasimamiwa na Mamlaka ya Mji wa Arusha chini ya Engineer Rujomba pamoja na Mwenyekiti wake Dkt. Masika na Mheshimiwa Balozi Ole- Njoolay. Mradi ule Mheshimiwa Rais alielekeza maji yale yaletwe Mererani, yapelekwe kwenye Kata ya Endiamtu, yapelekwe kwenye maeneo mengine yanayozunguka Mji wa Mererani ambayo ni Kata ya Shambarai, Kata ya Naisinyai na Kata ya Oljoro Namba 5. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichukue nafasi hii kumwomba Mheshimiwa Waziri na timu yake. Nimesema nawapongeza na ndio hasa furaha yangu iliyopo leo na mengine nitaomba tu kwa unyenyekevu. Maelekezo ya Rais kupeleka maji katika maeneo haya niliyoyataja ni kwa sababu maji yaliyoko pale yana fluoride kubwa na yanapelekea watoto kupinda miguu na wengine meno kuoza, ukiwaona unaona meno ya watu ni mekundu na siyo hapo tu na Kata ya Msitu wa Tembo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuendelea kuwa na maji ambayo watu wetu wanapinda miguu katika kizazi hiki siyo sifa njema kwa Serikali ambayo Rais wake anatafuta fedha nyingi kwa ajili ya maendeleo ya watu. Kwa hiyo niendelee kumwomba sana Mheshimiwa Waziri na timu yake watupie macho yao tena katika maeneo haya. Siyo kwamba sitambui miradi aliyonisaidia ambayo Wizara yake chini ya RUWASA, nampongeza sana Meneja wangu wa RUWASA wa Mkoa, Ndugu yangu Walter Kirita na Ndugu yangu Johanes Engineer wa RUWASA, Simanjiro ambaye kwa kweli nasema amekaa akikaimu nafasi ile kwa muda mrefu na amefanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ningeomba sana amfikirie, apitie tena muda aliokaimu na kazi nzuri aliyoifanya ikimpendeza amthibitishe, amefanya kazi nzuri Johanes, kazi ambayo ni ya mfano. Hakuna Diwani leo ambaye hamsifu kwenye halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekumbuka miradi ambayo Serikali ya Mama Samia imetusaidia sana. Wananchi wa Terrat wana furaha kwa sababu ya Mama Samia, wananchi wa Engonongoi wana furaha kwa sababu ya Mama Samia, wananchi wa Endonyongijape, Naberera, Okutu na Lemeshuko wana matumaini kwamba katika bajeti inayokuja watapelekewa maji. Wananchi wa Losoito na Naiborndet katika bajeti ya mwaka huu watapelekewa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika taarifa ya Mheshimiwa Waziri kwa upande wa, nilikuwa napitia Fungu namba 49 upande wa randama katika ukurasa wa 56 kwamba moja kati ya kazi atakazofanya ni pamoja na ujenzi wa mabwawa ya maji ya ukubwa wa kati hususani katika maeneo makame. Nataka niseme Wilaya ya Simanjiro ni miongoni mwa maeneo ambayo yapo katika nyanda kame na wote wanajua na Waziri juzi ameshuhudia alipokuja na Kamati. Nampongeza sana Mwenyekiti wa Kamati ya Maji walifika, walishangaa walivyofika katika yale maeneo wakasema, kabla ya mradi huu wa Mama Samia wa kupeleka maji Orkesumet, watu hawa walikuwa wanaishije?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Simanjiro ni miongoni mwa maeneo ambayo yapo katika nyanda kame na ninyi nyote mnajua na wewe mwenyewe juzi umeshuhudia ulipokuja na Kamati nampongeza sana Mwenyekiti wa Kamati ya Maji walifika, walishangaa walivyofika katika yale maeneo wakasema kabla ya mradi huu wa Mama Samia wa kupeleka maji Orkesumet, watu hawa walikuwa wanaishije?

Nikawaambia mmeona tu sehemu ndogo ya sehemu ya Wilaya ya Simanjiro ipo haja ya wakati mnagawa rasilimali hizi za nchi muangalie mazingira na jiografia ya maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachimba mpaka mita 200 chini hatupati maji ardhini, tupo katika nyanda kame, Simanjiro iko kwenye nyanda kame, Longido ipo kwenye nyanda kame, Monduli ipo kwenye nyanda kame. Watu wanapeleka maji kwa matrekta kilometa 50 kilometa 20, 30 ni jambo la kawaida kwenda kutafuta maji kilometa 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitoka leo Lerumo ambako leo ndiyo inapelekwa maji katika bajeti ya mwaka huu ni kilometa 30 kwenda Rovuremit lakini wananchi wa Lerumo leo Mkandarasi amepatikana na kazi imekwishaanza na hii kazi ni ya Mama Samia Suluhu Hassan, Waziri wake ni wewe Juma Aweso. Nawapongezeni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini upo mradi….

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Ole-Sendeka.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ooh, ninakushukuru kwa kunipa nafasi hiyo, hauwezi kuniongezea hata dakika hivi au ndiyo muda umeenda?

MWENYEKITI: Malizia dakika moja.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ngoja nimalizie, ahsante nashukuru. Niombe basi ule mradi wa Mirerani, Endiyamtu, Shambarai, Olgora Namba Tano na Isinyai ukamilishwe na wenzetu wa Mamlaka ya Maji wa Mji wa Arusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)