Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona na kunipa nafasi ya kuweza kuchangia kwenye hotuba ya bajeti ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuipongeza Serikali yetu ya awamu ya sita kwa kazi kubwa ambayo imekuwa ikiifanya katika kuhakikisha kwamba inamtua mama ndoo kichwani. Pili napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri rafiki yangu bwana Aweso pamoja na Naibu wake kwa kazi kubwa wanayoifanya. Nakumbuka wamepita hadi kwenye jimbo langu mara kadhaa kwa ajili ya kuhimiza na kuisimamia miradi ya maendeleo ya sekta hii ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ningependa kuanza kuchangia kwa kupongeza zaidi Serikali kwa sababu ndani ya miaka mitatu iliyopita imewekeza zaidi ya shilingi bilioni tano katika Wilaya yetu ya Kilwa yenye vijiji tisini, na tayari miradi katika vijiji vinne tayari imekamilika; maji yanamwagika katika Kijiji cha Chapita, Chumo, Likawage pamoja na Somanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ipo miradi ambayo ipo katika hatua za mwisho za utekelezaji ikiwemo uchimbaji wa visima pamoja na kuweka mtandao wa mabomba katika Vijiji vya Marendego, Nasaya, Masaninga, Kisima Mkika Zinga Kibaoni, Matandu, Hoteli Tatu, Mbwemkulu, Nainokwe, Kipimbimbi, Kilwa Masoko, Kikole, Nakiu, Kilwa Kisiwani, Hoteli Tatu pamoja Nakinjumbi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bado kuna maeneo ya vijiji 32 kati ya vijiji 90 bado vina changamoto kubwa ya maji na bado havijafikiwa na mtandao wa maji wa RUWASA. Nitavitaja baadhi ya vijiji; kipo kijji cha sehemu fulani za baadhi ya vitongoji vya Zinga Kibaoni. Pia vipo vijiji Vya Ngalambi; Lienga Kijiji cha Namatewa; Mwengei; Pungutini pamoja na Nandete, Nandembo pamoja na vijiji vingine, kama nilivyosema vijiji 32 kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa hapa napitia ukurasa wa 55, 56 kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, pamoja na majedwali ya miradi ya maendeleo ambayo inakwenda kutekelezwa katika mwaka huu ujao. Nimeona pale katika ukursa huu wa 55, 56 amehimiza kuhusu uwepo wa miradi ambayo itatokana navyanzo vikubwa vya maji ile miradi ya kimkakati ikiwemo mradi wa maji kutoka mto Rufiji. Lakini pia nimeenda mbele zaidi ukurusa wa 111 katika yale majedwali yanayofafanua kuhusu miradi ya maendeleo, nimekuta Kilwa pamoja na Wilaya ya Lindi mkoani Lindi imeeleza kwamba tutapata maji kutoka kwenye Mto Rufiji vijiji viwili tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitanabaishe hapa; kutoka main stream ya Mto Rufiji ni kilometa 52 mnalikuta jimbo langu, yaani ni mpaka wa Mkoa wa Pwani na Mkoa wa Lindi. Lakini pia uipita njia ya mkato kama unataka kwenda Kipatimu unatembea kilometa 47 tu unakuta tayari umeingia katika jimbo langu Mkoani Lindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa inanishangaza kidogo, au sijui kuna typing error kuona mradi huu utatambaa kutoka Mto Rufiji utakwenda mpaka Kilwa mpaka Wilaya ya Lindi lakini utagusa vijiji viwili tu. Nafikiri hii haiko sawasawa. Na kwa mujibu wa maelezo yao kwenye yale majedwali wanasema wananchi wa vijiji viwili wapatao elfu hamsini laki tisa arobaini na nne watanufaika na mradi huu wa maji ya Mto Rufiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napata mashaka kidogo vijiji viwili kuwa na wananchi 50,000 kwa. Kwa hiyo naomba, kwanza hizi takwimu zikapitiwe upya ili kuona accuracy ya hivyo vijiji ambavyo vimezungumzwa hapa. Lakini, vijiji viwili ni vichache kwa umbali ambao bomba litatambaa. Na kwa kutokana na ukubwa wa tatizo nimeshasema hapa ni vijiji 32 bado vya Wilaya ya Kilwa havina maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo ningeomba Mheshimiwa Waziri wakafanye review katika utekelezaji wa mradi kutoka mto Rufiji ili ikiwezekana angalau mkazo hivu vijiji vyetu 32 ambavyo havina uhakika wa maji. Kwa sababu nina hakika chanzo cha uhakika cha kuweza kututoa kwenye tatizo hili la maji ni hiki cha Mto Rufiji. Na kama nilivyosema mwanzo, ni kiasi cha bilioni tano tu zimetengwa, na miradi ya kiasi cha bilioni 1.4 ndiyo ambayo imekamilika kwa miaka hii mitatu. Kwa hiyo tunahitaji sana maji kutoka Mto Rufiji ili yaweze kumaliza changamoto ya maji katika Wilaya ya Kilwa. (Makofi)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

TAARIFA

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji na kumuongezea, kwamba maji ya Mto Rufiji yanahitajika sana kwenye Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Mtwara kwa ujumla, tunahitaji maji kutoka Mto Rufiji.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Francis unapokea hiyo taarifa?

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea kwa asilimia 100. Wiki moja iliyopita tulipewa taarifa hapa na Wizara, kwamba Wizara pamoja na kutekeleza huu mradi kwa vijiji viwili vya Wilaya za Kilwa na Lindi pia watatengeneza mabomba mawili kupitia njia ya Mkuranga na Kisarawe ili yapeleke maji Dar es salaam. Lakini tunaona uwekezaji wa kuelekea Dar es salaam ni mkubwa sana. Ni kwa nini uwekezaji kama huo usifanyike kwa mikoa ya Kusini kama alivyozungumza mwenzangu Mheshimiwa Kuchauka? Kwa hiyo niseme tu kwamba tunahitaji nguvu kubwa ielekezwe katika wilaya za Mkoa wa Lindi za Kilwa, Lindi vijijini, Lindi Mjini pamoja na Liwale kwa kuanzia ili wananchi wetu waweze kupata hii huduma ya maji safi na salama…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Francis Ndulane.

MHE FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti naomba kuunga mkono hoja.