Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nami niungane na Waheshimiwa Wabunge kumpongeza Mheshimiwa Juma Aweso, Waziri wa Maji kwa uwasilishaji wa Bajeti ya 2023/2024, bajeti ambayo ina mipango mikubwa ya kimaendeleo katika kuleta mapinduzi makubwa nchini Tanzania na kuhakikisha kwamba Watanzania tunaendelea kufurahia huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wanalindi mjini hatuna umasikini wa maji, tuna mradi mkubwa ambao umekamilika uligharimu Shilingi bilioni 33 pale Ng’apa. Mradi ule unazalisha maji kwa siku lita bilioni 7,500,000,000 na matumizi yetu ni bilioni 7,250,000,000. Katika miradi ambayo imekamilika ni mradi wa Tandangongoro, Ncheleweni Ng’apa uliogharimu shilingi 2,800,000,000 na mradi wa Mitoyo, shilingi 3,600,000,000, mradi wa Kiduni wa fedha za Covid-19 shilingi milioni 600, lakini na miradi mbalimbali ambayo bado inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kwetu wanalindi ni mapinduzi makubwa sana katika kuhakikisha kwamba tunaendelea kutekeleza miradi hii ya maji na kuwafanya wanalindi waendelee kupata huduma ya maji safi na salama. Hata hivyo, Lindi Mjini pamoja na fedha nyingi zilizotekeleza miradi ya kujenga matenki ya maji na usambazaji wa mabomba, bado tunayo changamoto. Wananchi wetu wanashindwa kuvuta maji majumbani kwao. Sisi wanalindi tunatamani kuichangia Serikali yetu kwa kulipa bili za maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali, na nimwombe ndugu yangu Juma Aweso, ninaamini kwamba anaumiza kichwa sana juu ya Manispaa ya Lindi kwa sababu hatujakamilisha kusogeza miundombinu ya maji kwenye mitaa yetu ili wananchi wetu waendelee kuvuta maji majumbani na watumie kadri wanavyoweza kutumia waweze kuchangia pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu imechangia fedha nyingi sana, na tunatamani hizi fedha zirudi zikafanye kazi nyingine za kimaendeleo kuhakikisha kwamba tunaendeleza miradi hii ya maji. Hatuwezi kuchangia kama wananchi wetu hawataweza kuingia kwenye mpango wa kuvuta maji majumbani kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana ndugu yangu Mheshimiwa Jumaa Aweso kuitazama Lindi kwa jicho la huruma. Katika miradi mipya ambayo tunategemea kwamba inaendelea kutekelezwa, ni mradi wa Ngaza ambao unagharimu fedha shilingi 1,130,000,000. Pia tuna mradi wa Mkundi upande wa pili wa bahari wa shilingi milioni 800.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Jumaa Aweso, asubuhi hapa ametangaza kutuingizia advance ya fedha na tumeona zimesoma kwenye account za maji. shilingi milioni 100 imekuja Lindi Mjini kuhakikisha kwamba mradi huu Ngaza unaogharimu shilingi 1,130,000,000 unaendelea kutekelezwa. Mheshimiwa Waziri nikushukuru sana kwa huruma yako na kwa mapenzi yako makubwa ya kuhakikisha kwamba sasa wanalindi tunapata mapinduzi makubwa ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mradi mkubwa sasa hivi unaotoka Mitero kuelekea Jimbo jirani la Mchinga. Mradi huu unapita Kata ya Mbanja kwa maana ya Mtaa wa Mbanja, Mtaa wa Kipetu, unapita Masasi ya Leo, unapita Likong’o kwa maana ya Kata ya Mbanja, kata ambayo tunategemea kutekeleza mradi mkubwa wa LNG. Vile vile mradi huu unakwenda Jimbo jirani la Mchinga.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, tuhakikishe kwamba mitaa hii niliyoitaja inapata huduma ya maji, kwa sababu hawa ndio walinzi wa mitaro ile iliyopita bomba kubwa la maji lakini walishiriki kuchimba mitaro ya maji kuhakikisha kwamba mabomba yanalazwa na kuelekea katika Jimbo la Mchinga. Maeneo haya yana changamoto kubwa sana ya maji safi na salama. Nina uhakika na usikivu wake mkubwa Mheshimiwa Waziri atahakikisha wananchi hawa wanaendelea kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri amesema kila Wilaya anatuletea fedha katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ya maji. Ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri, ziko Wilaya zina majimbo zaidi ya mawili. Lindi tuna majimbo matatu; tuna Jimbo la Mtama, tuna Jimbo la Lindi Mjini, na tuna Jimbo la Mchinga kwenye Wilaya moja. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri azingatie majimbo haya ambayo kwenye Wilaya moja yana zaidi ya jimbo moja kuhakikisha kwamba fedha hizi anapeleka kila jimbo na siyo kila Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mradi mpya ambao tunauombea fedha kwa bajeti hii ambayo tunaipitisha hivi leo. Tuna mradi mkubwa wa maji kutoka Ruaha kwenda Mnazi Mmoja utakaogharimu shilingi 1,229,000,000. Ndugu zetu wa Ruaha wamekuwa na changamoto kubwa ya maji kwa muda mrefu. Hawajawahi kuona hata bomba la maji kule kwenye Mtaa wa Ruaha. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri wetu Jumaa Aweso kuhakikisha kwamba fedha hizi zinakuja na tunakwenda kuwatekelezea wananchi wa Ruaha Mnazi Mmoja ili waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado tuna upanuzi wa mradi mkubwa ambao tunao kule Kitumbikwela, upande wa pili wa bahari, wananchi kule wanakosa maji safi na salama. Tunajua kwamba tumetengewa fedha za awali za kujenga matenki, Shilingi milioni 800, lakini tunahitaji kusambaza mabomba katika maeneo mbalimbali kuhakikisha kwamba wananchi wa kule Kitumbikwela, wanaendelea kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, yako maeneo ambayo tunatamani wawe na visima. Wananchi wanaendelea kutaabika kutopata maji safi na salama. Mheshimiwa Naibu Waziri katika safari yake Waziri wa Maji alitoa ahadi ya kutupatia visima vitano Lindi Mjini. Visima hivyo hakuna hata kimoja kilichochimbwa.

(Hapa kengele ililila kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa ahsante, kengele ya pili hiyo.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono, nakushukuru sana, nikutakie kila la kheri katika mapinduzi makubwa tunayoyategemea katika Wizara hii ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)