Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie Wizara hii ya Maji, Wizara muhimu kwa mustakabali wa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu, kwa kazi kubwa na nzuri sana anayoifanya ya kuboresha maisha ya Watanzania, mchapakazi, mpenda watu na kwa kweli tunajivunia kuwa nae. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Maji na wasaidizi wake kwa kazi nzuri, kwa wepesi wake na usikivu na kazi inasogea mbele. Kazi kubwa sana inafanywa na huduma za maji safi na salama na ya kutosha inasogezwa kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimboni kwangu miradi mingi ipo mikubwa na midogo na inakwenda vizuri. Mradi mmoja wapo kati ya miradi mikubwa ni ule wa Kemondo wa kata saba. Kata hizo Saba ni Kata ya Kemondo yenyewe, Kata za Katerero, Bujugo, Kanyangereko, Maruku na Kata mbili ziko kwa jirani yangu Mheshimiwa Charles Mwijage Mayondwe na Muhutwe. Mradi umesogea umefika asilimia 80 na zaidi ni kazi nzuri inasonga mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu umekuwa wa zamani una umri wa miaka minne, sasa hivi tuko awamu ya pili inatakiwa shilingi bilioni 4.8 ili awamu ya pili ikamilike. Kata kadhaa zipate maji na ninaomba hizi fedha zitolewe shilingi bilioni nne na milioni mia nane ili maji yasonge kwenye vijiji vya jirani pale ambavyo vinahusika na hiyo awamu ya pili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaambiwa kuna vifaa vinatoka Dar es Salaam, vingine vinatoka Uturuki, pampu za maji, imekuwa ni hadithi ya muda mrefu tunaomba ziletwe ili kazi hiyo isonge mbele na kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vingine miradi ipo lakini Mradi wa Kata ya Karabagaine umekuwa ni kizungumkuti. Pale tumepeleka maji Vijiji vitatu vya Kizuru, Kitwe na Kawa. Serikali ya mama Samia imesogeza maji kwenye vijiji hivyo, na pale ni Bukoba Vijijini lakini ule mradi umekabidhiwa Mamlaka ya Mjini, BUWASA. Kwanza sielewi kwa nini hiki kinafanyika, wajenge RUWASA wakamilishe kazi halafu mradi ukabidhiwe watu wa mjini waendeshe. Watu wa mjini wana bei kubwa. Sasa hivi kuna tatizo la kuunganisha maji kwa wananchi, maji yameshafika vijijini lengo ni kuwatua wanawake ndoo kichwani, lakini wanawake hawawezi kumudu yale maji, wanakwenda na ndoo zao mbali huko walikozoea maji yale hawayafaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ni nini hawa BUWASA wanaweka gharama kubwa sana. Gharama yao ni kuanzia shilingi 200,000 hadi shilingi 1,300,000 ya kuunganisha maji kwenye nyumba ya mtu, 200,000 ndiyo gharama za chini wengine mpaka 1,300,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa lengo la Serikali ya mama Samia ni kwamba watu wapate maji safi na salama na ya kutosha, lakini hawa BUWASA wanaweka gharama kubwa ambayo wananchi wa vijijini hawawezi kuimudu. Niombe hili Mheshimiwa Waziri uliangalie na uingilie kati. Kwa nini mradi uhamie mjini wakati ni wa vijijini?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mtu mmoja ametumiwa bili ya kuunganisha maji kwenye nyumba yake, ngoja noisome, imeandikwa hivi, Ndugu Charles Tibenderwa gharama zako za kuunganishiwa maji ni shilingi 464,396.40 na Kumbukumbu Na. ya malipo ni 994440341104, tafadhali lipa mapema kufuatana na maelezo uliyopewa na mamlaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, huyu bwana yuko mita 80 toka maji yalipofikia, anaambiwa gharama ni shilingi 464,000 na zaidi. Sasa kwa kweli hili ni tatizo kubwa, lazima wananchi wapate maji kama Serikali inavyokusudia. Serikali ya CCM inafanya kazi kubwa sasa kusitokee watu ambao wanataka faida kubwa kuzuia mafanikio ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yanayotokea Karabagaine yametokea tena vijiji vingine kwa mfano Kijiji cha Burugo, Kata ya Nyakato, hivyohivyo. Hii iko vijijini mradi umekabidhiwa kwa watu wa mjini wa BUWASA, matokeo yake gharama inakuwa ni kubwa, hawawezi kuimudu, naomba hii iangaliwe upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, gharama hizi za kuunganisha maji, kushimba mtaro na kulaza mabomba, kwa nini wananchi wasiruhusiwe kuchimba mitaro wenyewe? Mabomba yanajulikana yapo madukani, kwa nini BUWASA isisimamie kama inataka iendelee na huu mradi, isimamie tu uchimbaji wa mtaro wa kutosha, mabomba mazuri class c, bei iwe himilivu wananchi wapate maji kama walivyokusudiwa badala ya kupandisha bei wananchi wakashindwa kupata hayo maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi mwingine uko pale Kata ya Katoma, maji yamekamilika pale katika Kijiji cha Ilogero, Kijiji cha Kashenge na kwingineko. Lakini kuna vita ya chini kwa chini. Huu mradi umejengwa na RUWASA, umekamilika, kazi ni nzuri, maji yako ya kutosha mazuri kwa wananchi. Kuna vita vya ndani kwa ndani, wanataka wauhamishie BUWASA mjini. Mradi uko vijijini kwa nini wanapambana kuupeleka mjini, ili wapandishe bei wananchi washindwe kupata huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nimalizie kwa kuomba, kuna mradi mwingine wa Kata sita za Izimbya, Kaitoke, Mugajwale, Ruhunga, Katoro na Kaibanja. Mradi huu umesemwa siku nyingi sana, miaka mingi unasemwa, tunaambiwa hadithi ileile upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Usanifu huu hauishi? Miaka zaidi ya mitatu, minne, tunaambiwa usanifu wa kina na upembuzi yakinifu. Naomba upembuzi ukamilike, usanifu ukamilike mradi uanze.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale kuna ziwa Ikimba, maji mengi ya kutosha lakini watu hawawezi kupata maji. Katikati ya hizi Kata sita kuna Ziwa Ikimba, kubwa la kutosha lakini maji hayawezi kuwafikia wananchi kwa sababu ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Tunaomba mradi huu ukamilike nao uanze kujengwa wananchi wapate huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)