Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Bajeti hii ya Kilimo. Awali ya yote naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na tumekutana katika Bajeti hii ya Mwaka 2023/2024. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Bashe, Naibu Waziri Mheshimiwa Mavunde, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa jinsi walivyoandaa vizuri randama lakini na Hotuba ya Waziri. Pia niwashukuru sana na kuwapongeza jinsi wanavyomuunga mkono Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ili aweze kutekeleza majukumu yake katika kusaidia shughuli nyingi anazozifanya za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa nafasi ya pekee nimpongeze sana Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kukubali kuongeza bajeti ya Wizara ya Kilimo kutoka kwenye shilingi milioni zaidi ya 200 mpaka shilingi milioni 954. Pia nimpongeze kwa kutoa shilingi bilioni 150 kama ruzuku ya pembejeo. Nampongeza sana kwa sababu kwa matendo haya ambayo ameyafanya ni matendo ya kiungwana ya kiuzalendo ambayo yamewasaidia sana wakulima na maeneo mengi tumepata neema kutokana na hayo yaliyofanywa na Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika malengo mkakati ya Wizara ya Kilimo, moja ya malengo haya ni kuboresha uratibu katika shughuli za kilimo. Kwa ujumla ukiangalia shughuli za kilimo zinavyoratibiwa ukianzia kwenye ngazi ya Wizara mpaka kule kwa wakulima hapo katikati panakuwa na pengo ambalo halisimamiwi na matokeo yake tunashindwa kufikia malengo. Kwa sababu Wizara inaweza ikatoa maelekezo au ikatoa namna mfumo unavyotakiwa ufanye kazi lakini unakuta kule chini Wizara nyingine pia inakabidhiwa majukumu ambayo pengine inakuwa na vipaumbele vingi bila kuzingatia sana suala la kilimo. Kwa hiyo nikuombe sana nishauri Serikali kuhakikisha kwamba wanatengeneza mfumo wa usimamizi katika Wizara ya Kilimo kuanzia ngazi ya Wizara mpaka kule chini kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimkumbushe Mheshimiwa Waziri kwamba kwenye suala la uzalishaji kwa mwaka 2020/2021 kwenye mazao mkakati tulizalisha tani 898,967. Mwaka 2021/2022 tulizalisha tani 1,004,470 na mwaka 2022/2023 ni tani 950. Kwa hiyo unaona kabisa kwamba hatufikii malengo, tunakwenda mbele tunarudi nyuma. Suala la kwanza kama Wizara itasimamia kwa ujumla kwenye suala la kilimo kuanzia kwenye Wizara mpaka kule chini, nina uhakika yale malengo yatakayokuwa yamepangwa yatasimamiwa vizuri na wakati mwingine tunaweza tukafikia hayo malengo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe mfano, mkakati wa miaka mitano kwenye zao la kahawa katika uzalishaji, tulipanga kuzalisha tani 300,000 lakini mwaka huu ambao tunao tumezalisha tani 62, bajeti inayokuja hiyo tumepanga kuzalisha tani 75. Kwa hiyo unaona kabisa ni namna gani bila kuwa na mikakati madhubuti hatutaweza kufikia yale malengo ambayo tumeyapanga. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Waziri kusimamia na kuona kwamba yale tunayopanga tuwe tunafikia angalau zaidi hata ya asilimia 50 kwenye utekelezaji wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitoka hapo kwenye uzalishaji kuna mambo mengine mbalimbali ambayo tuliyajadili huko nyuma, tungetegemea leo tungepata maelekezo ambayo yangetuonesha kabisa kwamba tunapiga hatua. Katika bajeti zetu za nyuma tuliwahi kujadili kwa kina sana kwenye suala la upimaji wa udongo, lakini ukiangalia kwenye taarifa ya Wizara ni kwamba yalitengwa mashamba makubwa makubwa yenye ukubwa wa ekari 162,000 lakini tulitegemea kwamba yapimwe yale mashamba ya wakulima wadogo wadogo, na nina uhakika kabisa kama yale mashamba yangepimwa leo tungepata taarifa ya kutushauri kwamba tunatakiwa tuagize mbolea kiasi gani na tupeleke maeneo yapi na mbolea ya aina gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina uhakika kabisa kama ukipima udongo na ukaona hali udongo umepimwa vizuri wakati mwingine unapunguza hata matumizi ya mbolea. Kwa hiyo niiombe Serikali kusimamia kwenye suala hili la upimaji wa udongo ili baadaye tuweze kuwashauri wakulima ni mbolea ya aina gani watumie katika kuongeza uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ukiangalia kwenye huduma ya ugani tumegawa pikipiki 5,889, lakini mimi natoka kule kwa wakulima sijaona manufaa ya zile pikipiki kwa sababu wale Maafisa Ugani hawawezeshwi, hawapewi mafuta na hawana uwezo wa kwenda kuwahudumia wakulima. Kwa hiyo niombe Serikali iangalie uwezekano wa kuhakikisha kwamba Maafisa Ugani wale wanawezeshwa na wanasimamiwa na waende wakawasaidie wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la pembejeo kama nilivyoshukuru kwa Mheshimiwa Rais kutoa ruzuku ya shilingi bilioni 150, tulipata changamoto kwenye ugawaji wa zile pembejeo. Mwanzoni kabisa wakulima walikuwa wanahangaika sana namna ya kupata pembejeo lakini baadaye hali ile ilipungua. Sasa kwa upande wa Mbinga nilikuwa naomba sana kuishauri Serikali, kuna vyama vya msingi ambavyo bado viko vizuri tofauti na wenzetu wa Mbozi. Tuishauri Serikali vyama vile vipewe uwakala kwa ajili ya kugawa hizi pembejeo lakini vitakuwa na uwezo tu wa kugawa pembejeo kama vitaongezewa ukomo wa madeni ili viwe na wigo wa kuchukua mikopo kwenye mabenki na kuhakikisha kwamba wanapeleka pembejeo kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nataka nizungumzie ni kwenye suala la elimu. Ukiangalia Wizara wamesema kwamba elimu inatolewa kupitia Sekretariet za Mikoa, Serikali za Mitaa na Sekta Binafsi, hawa wanatoa kwenye maonesho, kwa mwaka yanafanyika mara moja lakini kumbe tunatakiwa tuhakikishe kwamba wakulima wale wanapata elimu ya pembejeo lakini pia wanapata elimu ya viuatilifu na vitu vingine ambavyo vinahitajika ili kuongeza uzalishaji.

Suala la mwisho kabisa nichangie kwenye suala la masoko. Katika taarifa ya Wizara sijaona kama wameweka umuhimu sana kuzingatia masoko ya ndani. Soko la kwanza la ndani ni sisi wenyewe tuwe wanywaji wa kahawa. Tunatakiwa tuzingatie tuhakikishe kwamba wananchi wanakunywa kahawa kwa wingi na ukiangalia wenzetu nchi ya Ethiopia zaidi ya asilimia 50 kahawa ile inanywewa na wananchi wenyewe. Kwa hiyo niwaombe Wizara waweke mikakati ya kuhamasisha kuhakikisha kwamba wananchi wanakunywa kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili kwenye taarifa ya Wizara wamesema kwamba tutaimarisha masoko ya nje kupitia Balozi zetu, lakini ukiangalia zile Balozi wataalam waliopo kule kwenye Balozi nyingi siyo wataalamu wa kilimo na siyo wataalam wa biashara hizo. Kwa hiyo, nimuombe Waziri katika Wizara yake waunde Kitengo cha Baraza la Biashara ili iweze kuwasaidia kuwa-lead wale wananchi na wafanyabiashara kuhakikisha kwamba wanapata masoko katika Balozi zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa minada kwa upande wa Mbinga na Mbozi mwaka huu kulikuwa na changamoto kubwa sana bei za kahawa zilishuka, wananchi wale wamehangaika wamekaa muda mrefu bila kuuza kahawa yao, wamekuja kuuza baadaye sana wakati bei zimeanza kushuka. Pia kwenye makato ya shilingi 200 kama alivyosema Mheshimiwa Mwenisongole kwamba wananchi wale wanapata adha kubwa sana kwa makato yale ya shilingi 200, ni vizuri kama makato yoyote haya yanafanyika kwenye zao la mkulima yatolewe elimu mkulima aelewe na akubali kukatwa zile fedha bila kushurutishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa ninaunga mkono hoja. (Makofi)