Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye hotuba hii ya Wizara ya Kilimo. Nianze kwa kukupongeza wewe kwa jinsi ambavyo unatuongoza vizuri siku ya leo pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri Bashe, Naibu Waziri Mavunde, Katibu Mkuu Gerald na watumishi wote wa Wizara ya Kilimo kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kumsaidia Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Kilimo tumewapa watu makini ambao tunaamini watatuvusha kwa rasilimali ambayo kwa kweli Mama amewapatia. Changamoto kubwa kwenye upande wa kilimo ni suala la kutegemea mvua ya Mwenyezi Mungu, Waziri kwenye hotuba yake ametueleza vizuri jinsi alivyoweka mkakati mzuri wa kutengeneza maeneo ya umwagiliaji. Mimi niombe tu kwenye eneo hili Jimbo langu la Hanang’ kuna maeneo mengi ambayo tukiweka skimu za umwagiliaji na Hanang’ ardhi yake ina rutuba ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Bonde la Duru iko Kata ya Masakta ina maji mengi sana, yale maji hayatumiki weka skimu pale. Tuna Bwawa la Gidahabaiek ambayo inakusanya maji yote ya Mlima Hanang. Wizara ya Maji wamefanya tathmini na usanifu wa kina tayari, shirikiana nao weka skimu ya umwagiliaji eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Bonde la Getasam Kata ya Masqaroda eneo zuri sana na ardhi pale ina rutuba sana. Tuna eneo tunaliita Endasak Matindigani skimu inafaa. Tuna Bonde la Nyamura ambako vijiji vitatu vingeweza kunufaika tukiwekeza hapo. Kijiji cha Basutuqang, Hidek na Mara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Balang’dalalu na Gidabanja pale mpakani maji ni mengi sana, tukiweka skimu pale itasaidia vijiji hivyo viwili. Tuna Bwawa la Endesh litaisaidia Kata nzima ya Ishponga. Tuna ziwa kubwa Ziwa Basutu. Wananchi wanalitumia kwenye kilimo cha umwagiliaji, wakati mwingine wanagombana na Serikali kwa sababu wao wanafanya kienyeji wanahitaji kusaidiwa tutengenenze mfumo wa umwagiliaji wa kisasa ili wale wakulima wa eneo la Basutu waweze kutengeneza tija na hiyo itawezesha wakulima wa Wilaya ya Hanang’ kuzalisha kwa mwaka mara mbili au mara tatu na kwa sababu ardhi ile ina rutuba ya kutosha na tukaboresha eneo la usimamizi tutapata mavuno ya kutosha. Ninaamini umelipokea Mheshimiwa Waziri wewe ni msikivu tunashirikiana vizuri, naamini kwenye eneo hilo hutaniangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kwenye tija. Hatuna muujiza wowote ili tuendeleze kilimo bila kuwekeza kwenye sayansi. Eneo hili lazima tuweke fedha za kutosha kwenye eneo la utafiti. Utafiti wa mbegu, mbolea na viuatilifu ambavyo vinaendana na mazingira yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri miaka ya nyuma wakati tunakua unachukua tu mbegu ghalani unaenda kupanda na unavuna. Sasa hivi mbegu tulizonazo ukishatumia mwaka mmoja, mwaka mwingine hamna. Tuna mbegu zetu za asili, tumieni sayansi pale tuone namna ya kuboresha badala ya kwamba tunatengeneza biashara za watu kwenye mbegu, tuone namna ambavyo tunaweza kuwapunguzia wakulima wetu gharama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kakunda ameongea hapa, mfuko mmoja wa kilo mbili shilingi 12,000 wakati ukivuna tu sisi mahindi hayana bei. Kwa hiyo, eneo hilo tuliangalie kwa makini tufanye utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikukumbushe Mheshimiwa Waziri mwaka 2020 Desemba wewe na timu nzima ya Wizara ya Kilimo mlikuja Hanang’. Tulitembea kwenye mashamba ya ngano na hii ilikuwa inaenda kutibu hotuba aliyotoa Mheshimiwa Rais wakati anazindua Bunge la 12 kwamba tuna nakisi ya ngano ya karibu tani milioni moja. Hanang’ kihistoria ni wazalishaji wakubwa wa ngano. Nimepitia kwenye hotuba yako ukurasa wa 90 umeelezea masuala ya uzalishaji wa ngano. Mwaka 2017/2018 tani 57,000 lakini mwaka 2021/2022 tani 62,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mashamba makubwa Hanang naomba weka jicho kule, yale mashamba hayatumiki vizuri. Tunalo shamba la Basutu plantation ambalo linasimamiwa na Halmashauri, lile shamba wanakodishwa wananchi fedha zile zinakusanywa na Halmashauri inaisaidia sana halmashauri lakini lile shamba limerudiswa kwako, utakapolipokea naomba usitafute wawekezaji wa nje, Hanang ni wakulima wazuri, kilimo ndiyo maisha yetu. Badala ya kutafuta watu waje wawekeze halafu baadaye uzalishaji uwe hafifu kama sasa hivi wawekezaji tulionao. Nikupe tu taarifa, wawekezaji ambao tunao sasa hivi, wanazalisha wastani wa 0.3 to 0.5 tons kwa eka moja. Wakulima wangu wa kawaida wanazalisha 1.2 mpaka 1.5 kwa eka moja. Sasa utahangaika kutafuta wawekezaji wa nini? Watanzania wapo tayari kufanya kazi. Tuwasaidie wale ambao tayari wanafanya kazi yao, tusije tukaleta watu ambao watakuja kutukwamisha kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tu niseme tukiwapa Watanzania hawa wa kawaida ile ardhi ya mashamba makubwa ya sasa hivi, karibu ekari 66,000 tukazalisha kwa wastani wa 1.5 ton, tutapata kwa mwaka mmoja metric ton 99,000. Hiyo ni Hanang’ tu na hayo mashamba makubwa. Nikwambie tu kwa sasa hali ilivyo siyo nzuri, mapori ni mengi. Uliniahidi hapa Bungeni kwamba utatwaa ekari 30,000 tuwarudishie wakulima wazuri wa Hanang’ ili waweze kuzalisha kwa tija. Ninaomba hiyo kazi uifanye wale jamaa zako wanakuja kwako wanakupa na maneno mazuri, hakuna chochote kinachofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa ninavyoongea kuna zaidi ya ekari 20,000 ni pori, wananchi wangu wanakodi mashamba. Heka moja kwa wastani wa shilingi 200,000. Mfano mzuri tunalo shamba la Halmashauri ambalo mwananchi amelikodi, eka moja shilingi 165,000 lakini kuna mashamba mabingwa tu wa kuweka mipaka lakini hawalimi. Ninaomba angalia eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tuna ardhi wananchi wanataka kuzalisha lakini kuna mtu ameshikilia ameweka vigingi kila siku ni kukamata mifugo ya wananchi, ukiigusa tu kidogo anaenda anaharibu mazao yako, sasa tumeleta wawekezaji ili walinde ardhi yetu? Hatuwezi kulinda sisi wenyewe? Tafuta watu ambao watawekeza na Wanahanang’ wako tayari wanataka ardhi ya kulima. Hatuna ardhi ya kulima utusaidie kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie Mheshimiwa Waziri mimi nakuamini sana unafanya kazi nzuri angalia maeneo hayo niliyoyataja. Baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)