Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii muhimu kwa wananchi wangu wa Jimbo la Mbozi. Nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunipa nafasi ya kusimama kwenye hili Bunge Tukufu kuchangia bajeti ya Wizara ya Kilimo. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa ruzuku aliyotoa kwa wakulima wa Mbozi na nchi nzima. Kusema ule ukweli isingelikuwa ruzuku ile sijui tungeficha wapi sura zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nimpongeze Mheshimiwa Bashe, Naibu wake na Maafisa wote wa Wizara wakiongozwa na Katibu Mkuu kwa kazi nzuri na utendaji mzuri wa kazi wanaofanya. Kipekee nimpongeze Kaka yangu Bashe kwa maamuzi ya kuwafungia wale mawakala wa mbolea. Kwa kweli vitu alivyofanya ni sahihi ingawa kuna baadhi ya watu wachache wanajaribu kumtikisa, mimi nasema akaze buti. Hatuwezi kuwavumilia mawakala wasio waaminifu, ambao wanashindwa kufuata taratibu na kanuni tulizoweka. Wako mawakala wengi nje ambao wanataka kuwemo katika huo mfumo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze mchango wangu kwa kueleza masikitiko makubwa kwa wakulima wangu wa kahawa wa Mbozi. Hivi tunavyozungumza huu mwezi Mei, kuna baadhi ya wakulima mpaka leo hawajalipwa kahawa waliyopeleka mwaka jana mwezi Julai, ile waliovuna. Shida hii ya wakulima wa kahawa Mheshimiwa Waziri anaifahamu. Amekuja Mbozi, Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuja Mbozi, matatizo yaliyoko kwenye vyama vile vya msingi vya AMCOS ni makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hapa hata malaika ashuke mbinguni aje kuongoza vile vyama bado wataiba tu na sielewi kwa nini Serikali inaona hivi vyama vya ushirika kama vile ni msahafu ambao hauwezi kubadilishwa. Kwani kuna ugumu gani kuleta soko huru, kuwaruhusu wanunuzi binafsi nao wachangie. Kuna ugumu gani kuwaruhusu wanunuzi binafsi kama vile ilivyo kwenye mchele au kwenye mahindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo vyama vya ushirika viwepo, lakini na wanunuzi binafsi wawepo. Kwa sababu ukiangalia, mkulima anapovuna kahawa yake anapeleka kwenye hivi Vyama vya Msingi vya Ushirika kuna makato yasiyo na kichwa wala miguu ambayo yamejaa pale. Sijui kuna makato ya gunia, sijui hela ya viburudisho, sijui hivi, kila aina ya takataka. Ikitoka pale kahawa inachukuliwa na hivi vyama vya AMCOS, inapelekwa kiwandani, bado kule nako kuna makato mengi. Sasa haiingii akilini kwa Serikali kuwalazimisha wakulima wapeleke kahawa yao kwenye hivi vyama vya msingi wakati huko kuna makato mengi yasiyo na kichwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa ambacho kinaumiza viongozi wengi wa vyama vya ushirika ni wezi. Tuna ushahidi wa kila kona, kesi ngapi ziko Mahakamani kuhusu viongozi wa vyama vya ushirika? Mheshimiwa Bashe mwenyewe ameleta timu Mbozi wamekagua, madudu waliyoyakuta yamefika ofisini kwa Waziri. Yanatisha na huo ukaguzi umefanyika kwenye vyama 20 tu vya AMCOS na kwenye kata nane. Sasa je angefanya kata zote 29 na vyama zaidi ya 100 ingekuwaje? Nimwombe Mheshimiwa Waziri sielewi kwa nini Serikali inaogopa kuruhusu soko huru la kahawa, kwa sababu vyama vya ushirika vime-prove failure kila kona. Hakuna justification hata mmoja ya kusema hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio huu ni mfumo mzuri wa wakulima kulinda masoko, lakini una makato mengi na wizi na Serikali imeshindwa kutatua hilo tatizo. Wakati umefika sasa wa kuwepo kwa serious debate ya kuhusu soko huru kwenye kahawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine kuna hii tozo ya shilingi 200 ambayo wakulima wa arabika nchini wanatozwa na Bodi ya Kahawa. Bodi ya Kahawa wanatuambia hii ni kwa ajlili ya kuendeleza zao la kahawa. Nataka niwaulize Bodi ya Kahawa lini wameendeleza Bodi ya Kahawa? Wamemsaidia vipi mkulima wa kahawa Tanzania waseme. Kwenye kata zote za kahawa za Mbozi hawajawahi toa msaada wa aina yoyote wa kusema wanasaidia. Sasa logic ya kuchukua hii shilingi 200 ya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wa robusta wanalipa shilingi 100 na sababu kubwa ni kwamba wameamua Taasisi ya Utafiti wa TaCRI na hii Bodi ijiendeshe yenyewe, iendeshwe na wadau kitu ambacho sio sahihi. Mbona TARI wanawatengea bilioni 40 za utafiti, kwa nini na TaCRI nao basi wasiwatengee fedha au bajeti kubwa. Ndio maana wanakuja na hizi idea ambazo hazina mashiko za kuchukua shilingi 200. Sasa wewe zidisha tani 80,000 zinazozalishwa za kahawa zidisha mara mia shilingi 200 ni shilingi ngapi, sio chini ya bilioni 16, za nini zote hizo? Utafiti gani wanaoufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ni jamaa yangu, lakini nahitaji maelezo ya kutosha kuhusu hii shilingi 200 ambayo wakulima wa arabika wanatozwa nchini bila sababu yoyote ya msingi. Sasa namwomba Mheshimiwa Waziri, kesho atakapokuja kuhitimisha hotuba yake naomba yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza, ili kuondoa kwa wakulima walioko Mbinga na walioko Mbozi ambao wanatulazimisha tupeleke kahawa yetu kwenye hivi vyama vyao vya AMCOS ambako huko kumejaa wezi na makato yasiyo na tija, ninachoomba kahawa inapofikishwa pale kwa AMCOS, mkulima apewe hela yake. Mambo ya kumcheleweshea mkulima aje asubiri sijui miezi, sijui iende huku, kikaenda kikarudi, huko ni kuwaonea wakulima na hakuna tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine hii Taasisi ya TaCRI ambayo inafanya kazi nzuri, lakini wameacha iendeshwe na wadau wa kahawa. Huko ni kumtelekeza mtoto uliyemzaa, kwa sababu TaCRI haina tofauti na TARI, majukumu yake. TARI wanawatengea bilioni 40, TaCRI kwa nini hawataki kuwapa hela na wanategemea watajiendesha vipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine, tuna hili suala la farm gate price ambao Bodi ya Kahawa ilikuwa inapaswa ku- meditate hii farm gate price, lakini kwa kipindi cha miaka mitatu tangu walipo-review hawajatoa hiyo hela. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake mwaka jana Halmashauri ya Mbozi ililazimika kukaa na viongozi wa hivi vyama vya AMCOS kupanga ushuru wa kahawa ambao halmashauri itachukua, kitu ambacho sio sahihi. Hii inafanya Bodi inakwepa majukumu yake. Kwa hiyo imekuwa kwa Mbozi kazi ya Bodi ni kukusanya tu shilingi 200, lakini majukumu mengine inakwepa. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri anapokuja hapa, nataka aje majibu rahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa ile timu ambayo iliituma Mbozi na najua imeleta majibu ya ukweli. Naomba wale wote ambao wametajwa kwenye hiyo ripoti wachukuliwe hatua kali za kisheria.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mwenisongole muda wako umekwisha.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaunga hoja baada ya kupata majibu yangu. Ahsante sana. (Makofi)