Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni hii ili na mimi nichangie katika Wizara hii ya kilimo. Nita-base sana kwenye suala la pembejeo za korosho pamoja na mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Rais wetu Jemedari wetu kwa kuwapa wakulima wetu pembejeo kwa njia ya ruzuku, tunashukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lakini Mheshimiwa Waziri nikusifu na nikupongeze kwa bajeti yako nzuri. Mashaka yangu ni yaleyale, kwamba Serikali iendelee kukupa pesa ili ndoto zako ziweze kufikisha vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri aende ukurasa wa 51 na 52 unaozungumzia suala la ruzuku la mbolea. Katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri amesema wakulima waliosajiriwa nchi nzima ni 3,050621 na walionufaika ni 801,776; kwa maana hiyo zaidi ya wakulima 2,200,000 hawakunufaika, Nadhani ilitakiwa atoe sababu ili wananchi wazijue lakini hakuzisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nikuambie ni kwa nini? kwa sababu jimbo langu ni asilimia 100 ni la vijijini. Jambo la kwanza uandikishaji ulitumia vitabu vya kawaida. Wanajiandikisha kupitia ofisi za vijiji anaandika na namba ya simu. Sasa, wakulima wetu ni masikini, hawana simu, anatumia simu ya mtoto anatumia ya binamu anatumia ya kaka. Wanakusanya vitabu wanapeleka halmashauri, halmashauri ndio wanasajiri. Matokeo yake unavyosajiri feedback kwa mkulima inakwenda kwa namba ya simu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walio wengi hawakupata namba hizi za usajiri na matokeo yake sasa hawakuweza kupata zile mbolea za ruzuku; na bahati mbaya zaidi, kwa sababu namba zile zimewajia wale ambao waliwapa namba wale waliopata zile namba ndio wamenufaika na huu mfumo wa ruzuku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tumwombe Mheshimiwa Waziri hili aliangalie; kwa mfumo ujao nilitegemea watabadilisha. Wakati huohuo hizo mbolea zilikuwa zinatolewa kwenye center moja ya makao makuu ya wilaya. Naungana na wenzangu waliosema, tunaomba mbolea hizi ziende zipelekwe kwenye centers, kwa maana ya kata au makao makuu ya tarafa isaidie angalau mkulima anaweza kwenda kwa baiskeli kufuata mbolea pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mtindo utasaidia sana kupunguza kero za wakulima. Lakini nilikuwa nadhani ni busara; TFRA wamefanya kazi nzuri sana ya kusajiri mawakala na wanunuzi 28. Miaka iliyopita tulikuwa tunatumia CPB kununua mbolea kwa pamoja, nadhani CPB ipo chini ya TFRA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini sasa hivi tutumie watu binafsi badala ya kuwapa TFRA kupitia CPB wapate hii mbolea ya ruzuku ili iwe rahisi kusambaza kwa bei ya kawaida? si jambo geni tumelifanya kwenye mafuta Serikali ilikuwa inatoa ruzuku kila mwezi bilioni 100, lakini hatukusikia kelele za mtu wa kupata mafuta kwa sababu amekosa ruzuku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa wakulima wetu kwa mfumo huu ulioutumia wakulima wengi wamekosa mbolea kwa sababu ya kukosa namba ya kusajiriwa kwa ajili ya kupata mbolea. kwa hiyo naomba sana wasomi mko wengi sana kwenye kilimo liangalieni mtindo huu fundisho mnalo; CPB kwenye mafuta wamefanikiwa. Wamefanikiwaje hamisheni mtindo huo kwenye CPB kwa upande wa kilimo ili wakulima waende wakanunue mbolea kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mawakala wale watapelekwa mpaka vijijini, mkulima ataenda na hela yake tayari mbolea ina ruzuku, siyo mnampa namba. Hii inasababisha mtindo fulani unakuwa siyo mzuri matokeo yake output yake itakuwa ni ngumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili la mbolea mwaka jana tumechelewesha sana. Kwa upande wetu sisi imekuja mbolea ya kupandia mwezi wa kwanza; tayari wakulima wameshapanda mahindi yameshafika futi moja, ni changamoto kubwa sana. Kwa hiyo hata hivyo uzalishaji utakuwa umepungua kwa sababu ya jambo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kilimo kule kwetu upande wa korosho miaka ya nyuma ya 2015/2016 Bodi ya Korosho ili jenga maghala matatu. Ghala moja lilijengwa Tunduru walipekeka bilioni moja, lingine Mkuranga bilioni moja na lingine Tanga Kilindi. Yale maghala zile pesa zimekaa tu pale, hayajaisha, tunaomba Serikali mkamalizie kujenga yale maghala. Yako matatu mkataba wao ilikuwa ni bilioni tano, mlipeleka bilioni moja moja, yamebaki yamekaa, hayajamaliziwa. Tunaomba Serikali katika mpango wa kujenga maghala basi mliangalie lile ghala la Tunduru, Mkuranga na Kilindi ili yaweze kumalizika kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo wakazungumzia suala pembejeo la korosho; kwa kweli Mheshimiwa Waziri unafanya kazi kubwa sana, tunakubali wakulima wote wa korosho. Hakuna mwaka ambao wakulima wamepata pembejeo nyingi kama mwaka uliopita; lakini matokeo yake uzalishaji umekuwa mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya sababu ni aina ya pembejeo mlizopeleka, wakulima hawakupata mafunzo ya kutosha ili kuweza kutumia uzalishaji ukae vizuri. Sehemu zingine wanadai kwamba pembejeo zilizokwenda ni fake matokeo yake mikorosho imeungua na uzalishaji umeshuka. Tunduru msimu uliopita kabla ya huu tulikuwa na tani 25,000, safari hii kutokana na changamoto hii tumepata tani 14,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri hao wazabuni ambao wamewapa kazi ya kusambaza pembejeo wakatoe elimu kwenye maeneo yetu wakulima ili watumie hizi pembejeo vizuri. Nimeona kwenye hotuba yako umesema TPHPA imetoa mafunzo kwenye wilaya tofautitofauti lakini Tunduru hawakufika, matokeo yake hizi dawa walizozipitisha zote wakulima wetu hawajui kutumia. Kwa hiyo wameathirika kwa kiasi kikubwa kwa ajili ya kutokujua matumizi halisi ya hizo pembejeo tulizozipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu skimu. Wilaya ya Tunduru tulikuwa na skimu nne, zilitumia zaidi ya bilioni nne. Kuna Skimu ya Madaba, Skimu ya Misyaje, Skimu ya Lolelole iko kwa mwenzangu na Kitanda; hizi zote zilitumia fedha nyingi sana, zaidi ya bilioni nne. Walijenga lakini walipeleka na barababra kwenye maeneo hayo, zaidi ya milioni 800 kutengeneza barabara; zile skimu hazifanyi kazi; hazifanyi kazi kwa sababu zoezi lile halikukamilika. Tunaomba hizi skimu mkafanye chini juu mkazimalizie, pamoja na maeneo mengine ambayo tayari tuna ukanda wa skimu. Kwa mfano kule kwangu kuna sehemu inaitwa Misyaje Kata ya Marumba wapo vizuri sana kwenye jambo la umwagiliaji. Kuna Vijiji vya Mkotamo, Wenje na Madaba. Vyote hiviā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mpakate muda wako umekwisha.

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)