Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi kuwa miongoni mwa watu wanaochangia Wizara ya Kilimo jioni ya leo. Na mimi niungane na wenzangu hasa kwa wanaomshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya kwa ajili ya maendeleo ya Taifa hili. Lakini nitachelewa kidogo kumshukuru au kumsifia Mheshimiwa Waziri kwa sababu kila aliyemsifia ametaja sababu za kumsifia. Mimi bado sijazipata, kwa maana ya Jimbo la Kibaha Vijijini, lakini nitakachokifanya kwa sasa kwake ni kumpa salamu za Jimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema ninaanza kumpa salamu na kwa sababu ni salamu za Jimbo la Kibaha Vijijini na Mkoa wa Pwani nitamuomba Mheshimiwa Waziri akamate peni azipokee salamu kwa sababu maana ya salamu mwisho wa kusalimiwa unamjibu mwenzio salamu aliyokupa na ni imani yangu baada ya kumsalimia leo kesho atasimama na kuzijibu salamu za wana Jimbo la Kibaha Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, salamu ya kwanza, nimepitia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri lakini nimekwenda sana kupitia viambatanisho ambavyo ameviweka juu ya hotuba yake, inayochambua baadhi ya vitu ambavyo vinakwenda kufanywa hasa kwenye baadhi ya miradi. Nimeangalia kwenye maeneo ya mabonde 22.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki moja iliyopita nilisimama hapa hapa niliposimama leo, niliuliza Wizara juu ya mikakati ambayo wanayo ya kutengeneza mabwawa makubwa kwenye Bonde la Ruvu, walinijibu kuwa Bwawa ambalo wanalitengeneza liko kule Morogoro Vijijini.

Hata hivyo, kwenye maswali yangu ya nyongeza nilitaka kujua mkakati wa kwenye Jimbo la Kibaha Vijijini; Naibu Waziri alijibu kwamba, Bonde la Ruvu ni moja kati ya mabonde 22 ambayo wamesaini mikataba na kampuni kwenda kufanya upembuzi yakinifu. Ndio maana nasema nashindwa kumsifia kwa sababu, nimepitia hotuba yake, sijaliona Bonde la Ruvu likitajwa katika hayo mabonde 22.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maneno mengine majibu niliyopewa siku ile ya maswali yangu hayana ukweli kwa sababu, kama yangekuwa yana ukweli maana yake bonde hili lingekuwa ndani ya orodha ya mabonde 22 ambalo Mheshimiwa Waziri alinijibu. Nimesema nampa hii kama salamu, sasa kama huku hakuweka, atakapokuwa anajibu salamu za Pwani na Kibaha, basi atanikumbusha nisome wapi nilione Bonde la Ruvu na mkataba uliosainiwa kwa ajili ya hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali langu pia la nyongeza, nilitaka kujua ile Skimu ya Kwala. Skimu ambayo ilijengwa mwaka 2011 na ilikula bilioni mbili za Serikali, imetelekezwa na nimeieleza maeneo mengi tangu naingia Bungeni, imekuwa sehemu ya kuchungia mifugo. Nikajaribu kuangalia kwenye viambatanisho, nikategemea labda nitaiona kwenye skimu 42 zinazokwenda kujengwa, hakuna. Nimekwenda kuangalia labda nitaona kwenye skimu mpya 35 zinazojengwa, sifuri. Nimekwenda kuangalia kwenye skimu 24 ambazo zinatakiwa kufanyiwa ukarabati, nilijua labda ile ni sehemu ya ukarabati kwa sababu, tayari imeshakula bilioni mbili, hakuna kabisa. Nimekwenda kuangalia labda kwenye mabwawa haya ambayo amezungumza nilipozungungumza masuala ya umwagiliaji wa keni, hakuna kitu. Kuna sababu gani ya mimi kusimama na kuendelea kumwambia Mheshimiwa Waziri nakupongeza sana kwa mazuri? Wa tumbaku wamepongeza kwa sababu kuna mambo yamefanywa kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, hizo nilikuwa nampa salamu na ningependa anaposimama kuja kujibu, basi anijibu hizi salamu za watu wa Jimbo la Kibaha Vijijini ni namna gani haya ambayo niliyauliza na walichonijibu na ambacho sikioni kwenye bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikuishia hapo, wiki mbili zilizopita pia niliandika barua rasmi ya kupeleka Wizarani kujaribu kuitaja baadhi ya miradi, nashukuru wamenijibu kwa maandishi, lakini hayo mandishi waliyonipa na hali halisi ya kwenye hotuba ya bajeti hakuna kitu. Maana yake nilichokuwa nimepata kwenye maswali ya nyongeza na swali la msingi na nilichopata kwenye barua ni sawasawa na hakuna. Kwa hiyo, hizo salamu naomba nipate majibu kesho pale atakapokuwa anakuja kutupatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka nilichangie ni hii Tume ya Umwagiliaji kwenye maeneo mazima ya ukusanyaji wa mapato. Nimeona hapa bajeti yam waka 2022, lengo la Tume ya Umwagiliaji lilikuwa ikusanye bilioni 126.1, lakini mpaka tunafika mwezi Aprili, imekusanya milioni 600 tu. Kwa maneno mengine ni kwamba, wako chini ya makusanyo ya bajeti ya kawaida ambayo wao waliipanga, lakini sasa nimeangalia bajeti mpya ambayo ndio wanaomba, wametoka kwenye bilioni 126 waliyoikusudia mwaka jana sasa wanaomba bilioni 10. Sasa najiuliza nini kiliwafanya mwaka jana waweke bajeti kubwa na nini kinawafanya mwaka huu wapunguze?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia sababu walizozitoa, naona sababu hazina mashiko sana. Unazungumza kwamba, mwaka jana hukukusanya vizuri, bajeti tunaambiwa hukusanyi vizuri kwa sababu hukuwa na watumishi kwenye mikoa; nini kilikupelekea uandae bajeti hiyo, kama unajua watumishi hukuwa nao? Kwa hiyo, naona kuna uwiano hapa ambao tunakwenda kupoteza mapato na tunakwenda kupunguza badala ya kuongeza nguvu za kukusanya ili tuweze kupata mapato ambayo yatakwenda kulijenga Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine la tatu ambalo naomba nilichangie ni huu mradi unaozungumzwa hapa wa BBT. Nimejaribu kuangalia takwimu zao wenyewe kwamba, walituma maombi vijana 20,227, wamefanya upembuzi, maombi ambayo yamekubaliwa ni ya vijana 812, lakini wote tunafahamu humu Bungeni, kama kuna watu wanalima sana wako vijijini, lakini pia akinamama ndio wakulima wakubwa sana. Nimeangalia hawa vijana ambao wanakwenda hapa, wenye jinsia ya kike ambao ndio wanakwenda kwenye huu mradi ni 282 tu, lakini wanaume wanakwenda 530. Hebu tuuangalie uwiano, lakini nakwenda mbali zaidi najaribu kujiuliza, ukiangalia pesa zinazoelekezwa kwenye mradi huu, ukiangalia mikakati inayowekwa na Serikali kwenye watu hawa 800, unajiuliza kwa nini nguvu hii isiwekezwe kwenye wakulima wadogo wa kawaida walio mitaani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tumekiri hapa na tumesikia hotuba ya bajeti, anasema kilimo tumefanikiwa kuandaa chakula mwaka huu kwa asilimia 100. Tujiulize, waliotufanya tuishi kwa asilimia mia moja ya chakula tumewasaidia nini? Kama pesa hizi nyingine zote tunazielekeza kwenye mradi huu na zinakwenda kuwagusa vijana wachache? Wale wengi ambao wametulisha mpaka leo na wataendelea kutulisha, kuna kitu gani kimetengwa kidogo kwa ajili ya kuwasaidia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio wakulima wale tunaowaona wanalalamika mbolea, ndio wakulima wale tunaowaona wanalima kwa jembe la mkono. Ningeishauri Serikali, pamoja na mradi huu una nia njema ya kutengeneza mabilionea kwenye kilimo, hivi unaweza kumtengeneza bilionea kuliko kuanza na yule uliyeanza naye? Kwa nini tusijielekeze kwenye kushughulika na wakulima wetu walio kwenye vijiji vyetu ili tuweze kuwafikia kwa kiasi kikubwa? Ili mabilionea watoke kwenye hao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi wale watatuelewaje? Unatengeneza mabilionea wapya ambao hawakuwa kwenye sekta ya kilimo, unawaacha mabilionea ambao wamelima kwa jembe la mkono kwa miaka mingi? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimwia Mwakamo, malizia mchango wako Mheshimiwa kwa sekunde 30.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi ya kumalizia. Naomba nimkumbushe Waziri kesho, hizi nilizomtangulizia ni salamu, naomba anijibu salamu za watu nilizomfikishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya haya, naunga mkono hoja. (Makofi)