Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo ameifanya katika eneo hili la uwekezaji pamoja na viwanda. Nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake kwa kazi kubwa anayofanya ya kutekeleza maono ya Mheshimiwa Rais katika sekta hii.

Mheshimiwa Spika, mtaweza kuona kwamba uwekezaji ambao umeishaingia ndani ya nchi yetu, pia na performance za viwanda ambapo sisi ni wadau wakubwa sana kwenye masuala ya performance za viwanda na uwekezaji katika eneo la kupata kodi pamoja na kukuza GDP, tunaiona wazi wazi. Hongera sana Mheshimiwa Waziri na hongera sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kuchangia nianzie kwa kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge na kukiri kwamba hoja zile ambazo wamezileta zinazo angukia upande wa Wizara yetu tumezipokea na tutazifanyia kazi na bahati nzuri sana wametoa maoni haya katika kipindi ambacho tunaendelea kukamilisha nyaraka ambazo tutazileta kwa ajili ya mjadala mpana wakati wa Hotuba ya Bajeti ya Serikali lakini pia na katika Finance Bill ambayo itajadiliwa mara tu baada ya bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, nikianza na yale masuala ambayo wameyaongea ya kikodi nitaomba uridhie na Waheshimiwa Wabunge niwaombe waridhie nisipitie kamoja kamoja kwa sababu ndiyo tunaendelea kukamilisha waraka huo. Tumepokea maoni yenu na niwaahidi kwamba tutakuja na hatua za kikodi ambazo ni rafiki kwa sekta binafsi kwa sababu huo ndiyo muelekeo wa nchi yetu na ndiyo muelekeo wa Mheshimiwa Rais kwa kutengeneza sheria za kodi ambazo ni rafiki kwa sekta binafsi na ni rafiki kwa uwekezaji, rafiki kwa mazingira ya biashara ili kuweza kutengeneza ajira na kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja pamoja na uchumi wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, liliongelewa kwa sauti kubwa suala la Kariakoo na lenyewe tumelizingatia tumepokea na yenyewe tutakapo kuja kwenye mjadala tutakuwa tumezingatia maoni yote ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyasema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye masuala mahususi yaliyoongelewa, jambo moja ambalo limeongelewa lilikuwa la ETS yale masuala ya Electronic Tax Stamp.

Mheshimiwa Spika, jambo hili utakumbuka lina maelekezo ya Bunge katika kipindi kilichopita mwaka mmoja ama miwili Bunge lilielekeza Waheshimiwa wabunge kwa kauli moja walielekeza kwamba Serikali iangalie upya jambo hili kwa sababu bei zinazotolewa na mtoa huduma ni kubwa. Serikali ilichukua hatua kwa kutangaza hili jambo hili lifate taratibu za International Tendering ili kuweza kualika wadau wengi wanaofanya kazi hiyo tukiwa tunashirikiana na sekta binafsi kuweza kupata mdau ambaye ataweza kutoa huduma hiyo kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Spika, mchakato uliendelea na wakati mchakato unaendela, nilisikia kauli moja anasema mbona akapewa sasa yule aliyekuwepo. Kwa sababu utaratibu wake unachukua takribani miezi sita na kuendelea, tuliona lazima utaratibu wa makusanyo uendelee katika kipindi hicho cha mpito ambacho ni cha mwaka mmoja, kwa hiyo utaratibu umeenda mpaka mwisho na nitawaomba Waheshimiwa Wabunge kwa umahsusi wa jambo hili katika hatua fulani hivi waridhie kwamba tutalielezea kwa kina katika ngazi ya kamati na kamati inawakilisha Bunge lakini wapokee maelezo haya ninayoyatoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulipofikia katika hatua ya kufanya uchambuzi. Uchambuzi ukafanyika mpaka mwisho na timu iliyokuwa inafanya uchambuzi ilikuwa imekusanya wazoefu wa utaratibu hizi za kimanunuzi kutoka taasisi zetu zote muhimu tunazozifahamu zote za vyombo pamoja na zile ambazo ni za kimanunuzi.

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho wa siku taarifa ile ya mwisho ilionesha kwamba bei zilizokuja hazitofautiani sana na zile zilizokuwepo na wahusika ambao wameenda kwenye hatua hizo wanaeleka kwenye utaratibu ule ambao bei ziko zile zile ambazo zilikuwa zimeamsha hisia hizi za wabunge na kuleta hoja ya kutaka tupate mtoa huduma mpya.

Mheshimiwa Spika, sasa ilivyofika mpaka mwisho pale sifa zile zilizokuwa zinatakiwa zilionekana hazijafuzu kwa sababu kile kilichokuwa kinatafutwa kuanzia maoni ambayo yalitolewa na wabunge ya bei hayakuwa yametimia. Kwa hiyo, kile ambacho kilikuwa kimefikia kwa hatua hii ilikuwa ni mchakato ule ufanyike upya na mchakato wenyewe unafanyika kwa hatua zote ikiwepo ya Window Shopping, ikiwepo ya National Shopping, kwa hiyo timu mbalimbali zimeenda katika maeneo ambako wananweza wakapata teknolojia mpya, teknolojia rafiki, teknolojia ambayo ina gharama nafuu lakini pia ikizingatia uwezekano wa kuihamishia teknolojia hiyo katika mamlaka zetu za usimamizi ili hitimisho wa siku jambo hili liweze kufanywa na watanzania wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ombi langu kwa waheshimiwa wabunge, kama kuna Mbunge ambaye ana mtu ama kampuni, ama taasisi ama teknolojia ama anajua mahali ambako teknolojia tunaweza tukaipata ambayo inaweza ikatoa huduma hiyo hata kwa nusu ya ile ambayo ipo, nimkaribishe aje ofisini aonane na mamlaka yetu inayosimamia jambo hilo Mamlaka ya Mapato Tanzania, halafu aweze kuunganisha timu ile inayofanya hiyo shopping pamoja na hiyo taasisi ambayo inaweza ikatoa huduma hiyo ili tuweze kukamilisha mchakato huo kwa ufanisi na tuweze kupata kile ambacho sekta binafsi yetu itanufaika na Watanzania watanufaika lakini na Serikali iweze kupata kodi katika gharama ambazo zinahilimika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jambo hilo liko hatua hiyo na tunaamini si muda mrefu sana tutaenda kwenye hatua ya mwisho na tutaendelea kulitolea taarifa jambo hili katika Kamati ya Bunge pamoja na Bunge lenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikihamia katika hoja ya pili ambayo ni mahsusi ni jambo lile la kiwanda cha Twiga, jambo hili ni jambo nyeti sana. Moja, sisi kama Serikali tuna interest kubwa sana kwenye jambo hilo kwa sababu kati ya wale wawekezaji kwenye kiwanda hiki ambacho tunakiongelea asilimia takribani sitini na nane ni hawa ndugu zetu wa AfriSam lakini asilimia zinazosalia mnajua kwamba upo mkono wa Serikali kupitia mifuko yetu ya hifadhi ya jamii ambalo ni jambo nyeti sana kwetu sisi kama Serikali. Kwa maana hiyo niwahakikishie Wabunge Serikali inapeleka macho yake yote mawili kuhakikisha kwamba jambo hili halifi bali linaendelea na hiyo ndiyo ambayo imekuwa concern ya wabunge kwamba labda kiwanda hiki kinaweza ikafanyika janja janja kwamba kikanunuliwa halafu kikafungwa. Hakiwezi kufungwa kwa sababu kimebeba maslahi ya nchi, kimebeba maslahi ya Serikali na kimebeba maslahi ya watanzania, hakiwezi kikafungwa. Mbali na habari ya ajira lakini ile tu yenyewe kwamba kwenye umiliki tuna taasisi zetu ambazo zina mkono mle hatuwezi tukaruhusu kikafa na hatuwezi tukaruhusu wale watakaofanya merging wakakipeleka kwenye kufa hilo halitatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili tukiacha utaratibu ukaendela hivi ilivyo sasa mwisho wa siku Serikali itaenda kubeba mzigo ule wote kwa sababu nimewatajia aina ya wamiliki walioko mle. Kiwanda hiki kikifa maana yake wale watu hawawezi wakapata hiyo hasara hii hasara itahamishiwa Serikalini. Kwa maana hiyo kwa hali waliyonayo ya sasa hivi kwa takribani cash flow zao ziko negative zaidi ya bilioni kumi na moja, hivi tunavyo ongea hawawezi wakastahimili kuendelea wao wenyewe tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye upande wa madeni wana deni kubwa ambalo linazidi bilioni mia mbili na tatu. Mnaweza mkaona kwamba hata wa kuwafufua tu anatakiwa awe na muscle kwelikweli. Wana 203 deni na wana overdraft ya zaidi ya bilioni 19 wanapumulia mashine hao walipo hapo wanahitaji wa kuwainua mwenyewe awe very strong. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa taratibu hizo zimeshafanyika zimeenda hatua nyingi. Mheshimiwa Naibu Waziri ameshaelezea vizuri masuala ya kisheria mimi naomba Waheshimiwa Wabunge muiamini kamati yenu Serikali tutaenda kuelezea kwa kina na niwaombe tusije tukalipazia sauti sana hili jambo, kwa sababu ukiondoa uwekezaji huu peke yake masuala ya kiuwekezaji ni very sensitive. Hizi back and forth tunaweza tukashughulika na mwekezaji mmoja lakini tukakimbiza wengine 50 kwa sababu tu ya back and forth ambazo tunazifanya.

Mheshimiwa Spika, ni vizuri tukaenda kwenye hatua kama nchi tukaendelea kupunguza yale ambayo kwenye rating tunakuwa rated chini kwa kuchelewesha uwekezaji na kuwa na milolongo mingi ambayo ina mikono mingi kwenye taratibu ambazo zinahitaji jambo liishe halafu tuweze kuendelea na uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema na nimeshaona kengele ya pili imeshagongwa niwaombe Waheshimiwa Wabunge waiamini Serikali, lakini pia waiamini Wizara, lakini pia waiamini Kamati. Tutaenda kutoa maelezo ya kina Kamati ya Bajeti na tutatoa maelezo ya kina kwenye Kamati ya Viwanda na Biashara kwa niaba ya Bunge zima ili tuweze kuelewana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na naomba kuwasilisha.