Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Uwekezaji Viwanda na Biashara. Nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha leo kusimama katika Bunge lako Tukufu. Kwa namna ya pekee sana namshukuru Rais wetu, Mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyopambana kutengeneza mazingira wezeshi kwa wawekezaji wetu wa ndani na nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa na mambo mawili tu ambayo ningependa nichangie asubuhi ya leo. Tunapoiangalia Wizara hii ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara sisi wawakilishi wa vijana tunaziona ajira, tunaona ndiye mkombozi wa changamoto zetu sisi vijana. Nitaongelea kuhusu ubunifu kidogo.

Mheshimiwa Spika, bado tunaona kuna changamoto katika Wizara hii. Bado hatuna mikakati, wala mpango ambao unawezesha vijana wetu wabunifu na wavumbuzi. Nasema haya kwa sababu moja, mbili au tatu. Katikati hapa, miaka miwili, mitatu hii, kumetokea vijana wavumbuzi wengi. Tumeona vijana wamevumbua local radios, wamevumbua magari, matrekta na ubunifu mbali mbali, lakini bado hatujaona mwendelezo wa bunifu zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata Mkoa wetu wa Kigoma kuna kijana amevumbua local radio, lakini hatuoni mwendelezo wa ubunifu wa kijana yule. Hatuoni Serikali inapoingia kumsaidia kijana yule kuendeleza ubunifu wake. Bado Serikali haijaweka mikakati mizuri ya kuwasaidia wabunifu wetu wa ndani. Hapa Waheshimiwa Wabunge wameongea vizuri, kama ambavyo wabunifu wa pombe wameelezwa, na kama ambavyo wabunifu wa magari wameelezwa, lakini bado hatuna mikakati ya kuendeleza bunifu zao.

Mheshimiwa Spika, naongea haya kwa sababu, ilitokea hapa mwaka 2021, kuna kijana mmoja alivumbua radio, lakini cha kushangaza, badala ya kusaidiwa kwenda mbele zaidi, tukasikia kijana yule kapelekwa Form Five na Six. Sasa unajiuliza, kwa kijana mbunifu, kijana ambaye amekaa, ametengeneza wazo, nini kilipaswa kufanyika? Kumwendeleza katika wazo lake, au kumpeleka shule akasome Form Five na Six ambayo haimsadii sana kama wangeendeleza ubunifu wake? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hili napenda kushauri, sisi kama Wizara tuje na mkakati wa incubation centers. Tunaposema incubations centers, hivi viwe vituo vya wavumbuzi na wabunifu. Tukiwachukua hawa wavumbuzi na wabunifu tukawaweka pamoja, kwanza inakuwa rahisi kuwapa elimu, kuwaendeleza na pia hata tukiamua kuwapa uwezeshaji wa kimitaji ni rahisi kuwa- manage na kuwafikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, incubation centers hizi zitatusaidia. Wizara inapokuja kutoa taarifa, inaweza kutuambia, katika miaka miwili hii tumepokea wabunifu sita, tumewaendeleza hivi, wamefikia hapa, na mchango wao kwa Taifa ni huu. Leo Wizara inaweza isiwe hata na database ya wabunifu kwa sababu bado mikakati na mipango hatujaiweka vizuri. Kwa hiyo, nashauri sana Serikali kuhusu suala la incubation centers. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ukisoma ukurasa wa 11 na wa 10 wa Hotuba ya Waziri, ameeleza vizuri namna ambavyo Serikali imejitahidi sana kuwasaidia wazalishaji wa zabibu. Nami nachukua nafasi hii kuwapongeza, kwa ambacho mmekisema mmewasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme jambo moja, ukiangalia wazalishaji wa zabibu, hata kama Serikali inasema imewapatia soko kwenye viwanda vidogo vya hapa Dodoma, bado changamoto ya soko ni kubwa sana. Nasema haya kwa mambo makubwa mawili; sijui kama Mheshimiwa Waziri ana taarifa, viwanda hivi vidogo ambavyo mnasema Serikali imewasaidia wakulima wa zabibu, kwamba bado vinashindwa kuwalipa wakulima wa zabibu kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo mkulima wa zabibu analima mwenyewe, akimaliza kulima anapeleka kiwandani zabibu zake, lakini inamchukua zaidi ya miezi nane mpaka mwaka kuweza kupata pesa yake. Pesa yenyewe anaipata kwa awamu na kidogo kidogo. Leo mkulima huyu amepeleka kiwandani zabibu za shilingi milioni mbili, anaambiwa leo anapewa shilingi 200,000, anaambiwa uje baada ya miezi miwili upewe shilingi 300,000, uje baada ya mwezi upewe shilingi 100,000. Kwa mazingira hayo, wakulima hawawezi kupenda kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nini kifanyike hapa? Pamoja ya kuwa mmewatafutia soko kwa viwanda hivyo, bado viwanda haviwalipi wakulima kwa wakati. Ukiongea na wamiliki wa viwanda, changamoto yao ni uwezo mdogo. Kwa hiyo, kwa sababu changamoto ni uwezo mdogo, hawawezi kuchukua zabibu zote na kuwalipa kwa wakati. Nini kifanyike? Kwanza naishauri Serikali iweze kuwasaidia hawa wamiliki wa hivi viwanda vidogo iweze kuwapatia mikopo ya uwekezaji. Hatuwezi kuwasaidia viwanda hivi kama tutawapa mikopo ya kibiashara, haiwezekani. Kwa sababu mikopo ya kibiashara ina riba kubwa. Kwa hiyo, naiomba Serikali iingilie kati jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuliko kutumia nguvu kubwa kuanzisha mashamba mapya, ni bora kutumia nguvu hiyo kwenda kuwawezesha watu ambao tayari wapo site, wanafanya shughuli hizo. Hii itawasaidia waone umuhimu wa kilimo na kuhamasisha wengine. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali, nguvu kubwa inayotumika kuanzisha mashamba mapya ni bora itumike nguvu hiyo kuwasaidia watu ambao tayari wapo site na wana changamoto ya kukuza mitaja yao ili waweze kufanya vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda sana niongelee SIDO, kwa sababu sisi kama vijana tulitamani na tulifikiria ingeweza kuwa mkombozi wetu, lakini Mheshimiwa Waziri bado una haja ya kupitia hizi SIDO, kwani nyingi hali zao ni tete. Sisi Kigoma pale na Mheshimiwa Waziri Mkuu hivi karibuni alienda pale kuzindua kiwanda cha kuchakata mafuta, lakini ukikiangalia kiwanda kile utaona, bado kiwanda kile hakina level ya kiwanda cha kisasa. Bado mzunguko wake ni mrefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hatutawekeza nguvu kubwa kwa SIDO, kama hatutatoa pesa kuwekeza SIDO, bado tutaendelea kuagiza vitu nje, bado tutaendelea kuagiza mashine nje na SIDO haitakuwa na umuhimu tena. Leo ninavyoongea hivi, Watanzania wengi hawafanyi biashara na SIDO tena, wanaenda zao kuagiza vitu nje. Kuliko niagize kitu SIDO, kitu chenyewe bado ubunifu wake au teknolojia yake ni ya kizamani, bora niagize zangu kitu tu nje kwa haraka na gharama nafuu, lakini pia kinakuwa kiko updated. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali iwekeze nguvu sana katika SIDO ili vijana wengi wapate ubunifu huko na itusaidie kupata mashine nyingi, vijana wengi waweze kujiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, ukiona mtu mzima analia, ujue kuna jambo. Jana nimesikiliza michango ya Wabunge wa Mkoa wa Tanga, na nimesikiliza michango ya Wabunge wengi, nikajiuliza kunani Tanga? Ikabidi nifuatilie. Nimeenda kusoma hukumu ya Fair Competition Tribunal nikabaki najiuliza. Hivi kweli katika nchi inayoongozwa na sheria, nchi inayofuata mifumo ya sheria, nchi kama hii ya kwetu, hivi chombo cha Serikali kinapata wapi ujasiri wa kupingana na maamuzi ya Mahakama? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana atakapokuja Mheshimiwa Waziri atuweke wazi, aondoe hii sintofahamu iliyokuwepo, atuelezee jambo hili ili tuweze kulielewa. Pia kuna haja sana ya sisi kama Watanzania kufuata sheria zetu. Tumeweka za nini kama tuna sheria na bado hatuwezi kuzifuata? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)