Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na mimi kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu kwa maendeleo ya Nchi yetu. Kwanza kabisa nianze kwa kuipongeza Serikali hii ya Awamu ya Sita kwa kazi nzuri inayofanya katika kuwekeza viwanda ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunafahamu namna Mheshimiwa Rais anavyopambana kuifungua nchi, kukaribisha wawekezaji lakini pia ku-promote vitu vyetu vya ndani. Kwa hiyo niipongeze sana sana sana Serikali hii ya Awamu ya Sita.

Mheshimiwa Spika, kipekee nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake na watendaji. Wamejipanga vizuri, sasa hivi husikii makelele makelele mengi ya kuongezeka kwa bei za bidhaa, nchi imetulia na kazi inaendelea. Hongereni sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi hiyo nzuri. Kipekee niishukuru Serikali na nimshukuru pia Mheshimiwa Waziri. Mwaka jana nilienda kumwona pamoja na wadau kuhusiana na viwanda vya ukoboaji wa kahawa pale katika jimbo langu. Kulikuwa na malalamiko yanajitokeza mara kwa mara kuhusiana na curing loss. Kwamba wakati kahawa inakobolewa, kuna taarifa za upotevu wa kahawa, inaitwa curing loss.

Mheshimiwa Spika, sasa ilikuwa inatofautiana kati ya kiwanda kimoja na kiwanda kingine. Kahawa hiyo hiyo imetoka kwenye chama kimoja ikipelekwa kwenye kiwanda hiki curing loss inakuwa kubwa lakini ikipelekwa kiwanda kingine inakuwa ya kawaida. Nilikuja na wadau kumwona Mheshimiwa Waziri tatizo lile limeshughulikiwa sasa hivi pako shwari. Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya ameunda tume juzi imefanya kazi nzuri, imehoji baadhi ya AMCOS, zimejibu kwamba sasa hivi kelele ile sasa imekwisha. Kwa hiyo nishukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kulishughulikia hilo. Niombe usiishie hapo endelea kuchunguza chunguza, maana hawa watu wajanja wanaweza wakawa wamefanya leo vizuri kesho wakafanya tofauti ili wakulima wetu wanufaike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili nimpongeze pia Waziri katika kipindi hiki ndipo tunaposhuhudia ulipwaji wa fidia wa Mchuchuma na Liganga, mradi ambao kwa kweli una historia kubwa na ndefu kweli kweli. Sisi wengine hata tulizaliwa suala la Mchuchuma na Liganga lilikuwa inazungumzwa. Leo watu wamekufa masuala haya yalikuwa yanazungumzwa; lakini leo kipekee tunashuhudia watu wanalipwa fidia. Ni hatua ya kupongeza sana kwamba tunatoka hatua moja kwenda hatua nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu, sasa tukilipa fidia tusikae, tusikae tuanze kutekeleza ule mradi. Nimeambiwa aliyeshinda hii tender hayupo tena duniani lakini watu wapo wa kuendeleza hii kazi. Nikuombe sana Waziri simama kama ulivyosimama, sasa hizi fidia zinalipwa, mradi huu uanze kutekelezwa.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi duniani ndiko kwenye malighafi ya makaa inahitajika. Watu sasa hivi wanavuna makaa pamoja na chuma kwa nguvu na kwa speed kubwa sana. Kwa hiyo nimuombe sana Mheshimiwa Waziri kipindi hiki ndicho cha kunufaika na huu mradi. Tusikae tena tunalipa fidia halafu tunaenda kutulia. Hatutai tendea haki nchi yetu, hatutawatendea Watanzania hawa haki. Mimi nina uhakika na Mheshimiwa Waziri suala hili ataenda nalo kwa speed kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine niishukuru pia Serikali. Pale kwangu kulikuwa na Mgodi wa TANCOAL kwa muda mrefu ulifanya kazi lakini ukasimama kwa muda pia mrefu sana kwa sababu tu ya migogoro ambayo pengine ilikuwa haina hata manufaa kwa nchi yetu lakini kwa Watanzania ambao walikuwa wanafanya kazi pale. Kulikuwa na mgogoro kati ya NBC, Milambo na Taifa Mine. Taarifa njema sasa hivi kupitia watu wetu wa FCC mambo haya yamezungumzwa vizuri na muda si mrefu kwa maelezo niliyopewa kuna muwekezaji mpya anakabidhiwa huu mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu ni kwamba suala hili nalo liende kwa speed ile ile, lisije likakawia tuakona tena kizungumkuti. Kwa sababu limeshaisha linakaribia sasa huyu muwekezaji mpya ku-take off pale; na wamesema baada ya kukabidhiwa, pale tu mkataba utakapo sainiwa basi wale watumishi, wafanyakazi waliokuwepo pale wataanza kunufaika na mafao yao ya huko nyuma kwa sababu kulikuwa na kelele nyingi sana za malipo yao ya huko nyuma, lakini pia kulikuwa na madai tofauti tofauti pale. Mara kadhaa ilikuwa nikienda pale unasikia kelele za wafanyakazi, kelele za waliowekeza pale kwa maana ya kwa sababu migodi hii ya makaa ya mawe inakuwa na wawekezaji wengi wengi. Kwa hiyo kila mtu alikuwa anadai kupitia kwenye hii Kampuni ya TANCOAL.

Mheshimiwa Spika, sasa nina uhakika Mheshimiwa Waziri baada ya kusainiwa huu mkataba hawa wote watalipwa na sasa hatutapata tena kelele. Lakini shughuli ya uchimbaji ya makaa ya mawe ambayo sasa yanahitajika sana sana duniani itaanza kwa kasi sana. Kwa hiyo nikuombe sana Mheshimiwa Waziri hili lishughulikiwe. Lakini nikupongeze kwa hatua hii ya awali ambayo imefikiwa, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine nitoe ombi. Kwa sababu wakati tunaambiwa tumegundua makaa ya mawe katika jimbo letu, wananchi hawa waliaminishwa kwamba sasa viwanda vitakuwepo, maendeleo yatakuwepo. Hata hivyo mpaka leo hatujapata kiwanda hata hiki, kimoja. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, kwa sababu tuna malighafi zetu pale, naomba sasa na sisi tupate kiwanda ili sasa wananchi wale waone manufaa ya kuwa na haya makaa ya mawe pale na malighafi nyingine. Niombe sana hilo Mheshimiwa Waziri; najua pengine utalitolea ufafanuzi hapo baadaye.

Mheshimiwa Spika, lingine ni suala la kulinda viwanda vyetu. Nilisikiliza baadhi ya michango hapa jana ya namna tunavyo- promote viwanda vilivyopo ndani ya nchi yetu. Tuna viwanda vingi, mimi hapa niwe specific kuzungumzia Kiwanda cha Magari cha GF Motors Limited. Kwanza tumshukuru sana huyu mtu mzawa huyu kwa kuwa na wazo hili la kiwanda ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunafahamu watu kadhaa walijaribu kuanzisha viwanda hapa Tanzania wakashindwa, lakini huyu ndugu yetu kaanza muda si mrefu na sasa hivi progress yake ni nzuri sana. Ameshafikia kuzalisha magari mpaka 700 na malengo yake mwaka huu anaenda kuzalisha magari 1,200. Kwa kweli watu wa namna hii wanapaswa kupongezwa lakini cha ziada wanapaswa kulindwa ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu sasa hivi ninavyokwambia mimi nilipata nafasi ya kutembelea pale. Tayari anawafanyakazi 115 wako pale wanafanya kaziā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde 30 malizia.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ombi langu watu wa namna hii wanapaswa kulindwa kwa sababu wanai-promote nchi yetu, wanakuza uchumi wa nchi yetu na wanatoa ajira kwa nchi yetu. Kwa hiyo tuombe sana Mheshimiwa Waziri watu hawa walindwe kwa nguvu zote.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)