Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Spika, ahsante na mimi kunipa fursa ya kuchangia katika Wizara hii ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana, Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Kwa sababu tangu aingie madarakani kati ya vitu ambavyo ameviweka kama maeneo yake ya vipaumbele ni katika kuhakikisha kwamba anaifungua Nchi yetu kwa wawekezaji wa nje, kuhakikisha anakuza uwekezaji wa ndani na kuhakikisha anakuza diplomasia ya uchumi katika Nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia naomba nitumie fursa hii kuipongeza Wizara, Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara. Kwa sababu kazi inayofanyika ni kubwa na matokeo yake tunayaona, hotuba iliyosomwa ya bajeti ya Wizara hii inatia matumaini.

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kuchangia nilivyokuwa nimepanga kuchangia, nimevutiwa sana na mchango alioutoa Mheshimiwa Mtenga juu ya changamoto ya viwanda vya chumvi katika Mkoa wake wa Mtwara na Lindi na ningependa tu wakati Mheshimiwa Waziri anakuja kutujibu hapa atueleze nini mkakati wa Serikali au Serikali ina mpango gani katika ku–control vibali vya uingizaji wa chumvi nchini, kwa sababu tukiacha hili eneo wazi hatuhatarishi tu viwanda hivi lakini tunahatarisha ajira nyingi sana za vijana…

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Ng’wasi Kamani kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. Biteko.

TAARIFA

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, pamoja na mchango mzuri wa Mheshimiwa Mbunge ninaomba tu kutoa taarifa kwa msemaji na kwa Bunge, kwamba vibali vya kuingiza chumvi nchini vilisimamishwa na Waziri wa Viwanda na sisi Wizara ya Madini tunaotoa vibali toka tumekubaliana na Wizara ya Viwanda kusitisha uingizaji wa chumvi ili tukubaliane namna gani tutumie chumvi ya ndani kabla ya kuagiza ya nje, hatujawahi kutoa kibali chochote na hakuna kibali kinachotolewa hadi sasa. Kwa hiyo, nilitaka tu wakati anachangia awe na comfort hiyo na Bunge liwe na comfort kwamba Serikali inafanyia kazi hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

SPIKA: Mheshimiwa Dotto Biteko, nilimsikia Mheshimiwa Nyongo akisema asilimia 70 ya chumvi inaagizwa. Amesema asilimia 70, wewe unasema haiagizwi kabisa, yaani mmesitisha uagizaji ama mimi ndio nimechanganya? Si unazungumzia chumvi. Mheshimiwa Nyongo taarifa uliokua unampa Mheshimiwa Mtenga ilikuwa inasema, tunaagiza asilimia ngapi?

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Spika, ni kwamba mahitaji ya chumvi kwa mwaka Tanzania ni tani 250,000. Tunaingiza asilimia 70 ya mahitaji hayo na wakati nchi ina uwezo wa kuzalisha chumvi tani zaidi ya 300,000 kwa kutumia source zote tulizonazo. (Makofi)

SPIKA: Haya, ahsante sana. Mheshimiwa Doto Biteko, hiyo taarifa sasa iko sahihi ili nimuulize sasa yule anapokea taarifa yako, kwamba vibali havitolewi na yule anasema asilimia 70 inaingia. Au ilikuwa inaingia kabla hamjaweka hilo katazo.

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, kama Mheshimiwa Nyongo nimemuelewa ni kwamba mahitaji ya chumvi ni tani 250,000 ambayo namba imepanda kidogo. Lakini sisi tunaagiza chumvi asilimia 70 wakati tuna uwezo wa kuzalisha zaidi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Nyongo ana justify kwamba hatuna sababu ya kuagiza kwa sababu uwezo wa kuzalisha uwezo wa kuzalisha chumvi ndani ni mkubwa kuliko kuagiza nje na ndicho nilichokuwa natoa taarifa kwa Mheshimiwa Kamani.

SPIKA: Swali langu ni kwamba hiyo asilimia 70 tunaingiza ama hatuingizi?

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, hiyo asilimia 70 ndio tunayo import kwa ajili ya kuja ku-blend chumvi ambayo tunayo ndani wakati tunayo ndani inayozidi kiwango hicho.

SPIKA: Haya pengine mwenye hoja ameelewa, Mheshimiwa Ng’wasi Kamani unaipokea taarifa hiyo?

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo naipokea, lakini nitumie fursa hii kutoa rai kwa Serikali kama tayari takwimu zinaonesha kwamba tuna uwezo wa kuzalisha chumvi ya ndani kwa kiwango kikubwa hata kuliko kile tunachohitaji katika mahitaji yetu. Naiomba sana Serikali utaratibu huu wa kufuta vibali hivi basi utiliwe mkazo ili viwanda vya ndani vya chumvi vipate kuzalisha na ajira za vijana na wakina mama wa Tanzania tuendelee kuzilinda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ya kwanza itakuja kwenye suala la chuma; Imekua miaka mingi sana na Wabunge wengi sana wamechangia suala la Mradi wa Liganga na Mchuchuma. Silengi kuujadili mradi huo kwa sababu naamini Serikali imesikia inaendelea kulifanyia kazi kwa sababu imekua ni jambo la muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, lakini nataka tu Serikali itueleza katika nchi yetu Mungu ameibariki na chuma inapatikana sehemu nyingi sana na katika taarifa ya Mheshimiwa Waziri ametuonesha kwamba katika mwaka huu wa fedha wanampango wa ku-deal na Liganga na Mchuchuma na Chuma kilichoko Maganga Matitu. Lakini kuna chuma kipi Handeni Tanga, kuna chuma kipo Mayamaya Dodoma, kuna chuma kiko maeneo Hondusi Morogoro lakini Wizara haizungumzii mambo haya. Tunaona kila leo kuna magari ya Dangote yanatoka katika maeneo yale ambako wachimbaji wadogo wadogo wanachimba chuma zinasafirishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali nitaomba ije itupe majibu, je, imekwishafanya tathmnini ya viwango vya chuma vilivyoko katika maeneo haya? lakini wachimbaji wadogo wadogo wanachimba hii chuma na kupakia na zinaenda nje. Je Serikali inafanya tathmini ya kiasi gani cha chuma kinatoka? Lakini Serikali inapokea mapato au maduhuri kiasi gani kutoka kwa wachimbaji wale? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitatoa mfano katika Wizara ya Madini, miaka ya nyuma Wizara ya Madini ilikuwa imetoa kipaumbele kikubwa sana na guidance kubwa kwa makampuni makubwa ya wachimbaji, ikasahau wachimbaji wadogo. Leo hii Wizara ya Madini imeamua kuwa incorporate wachimbaji wadogo na tuona ni namna gani mapato kutoka Wizara ya Madini yameongezeka.

Mheshimiwa Spika, ninaomba pia Wizara hii iangalie mfano huu kutoka katika Wizara ya Madini. Tuna wachimbaji wadogo wa chuma wanaochimba na chuma hii inatoka, itueleze ni kwa nini chuma hii inatoka bila kuchakatwa. Ni kwa nini hatujaja na mpango mkakati wa kuwa guide hawa wachimbaji wadogo ili na wao waweze kutuongezea pato na Mheshimiwa Waziri katika taarifa yake ametuonesha mahitaji ya chuma yalikuwa kutoka tani 200,000 na sasa tunaenda kwenye tani 1,000,000 na tuna project kubwa sana za Serikali zinazofanyika za kimkakati zinazohitaji chuma.

Mheshimiwa Spika, ninaamini kila chuma iliyoko katika nchi hii tukiiutumia ivilivyo na Serikali ikaangalia. Kuacha tu katika hii project moja ya Liganga na Mchuchuma ambayo nayo inatakiwa iendelee kufanyiwa kazi lakini tuangalie na chuma zingine zilizoko katika maeneo mengine ili tusipoteze mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakuja pia katika suala la NDC, NDC imeanzishwa zaidi ya miaka 60 sasa katika Nchi yetu. Ningependa pia katika majibu ya Serikali Mheshimiwa Waziri aje atuambie NDC mpaka sasa ina leseni ngapi? Na leseni ngapi zinazofanya kazi na ngapi hazifanyi kazi, wapi tumefeli na wapi tunatakiwa kurekebisha. Ili kusudi tuweze kuisaidia NDC kufanya kazi yake vizuri na iendelee kulipa maduhuri inayotakiwa kulipa katika Serikali.

Mheshimiwa Spika, ningependa pia Mheshimiwa Waziri katika majibu yake aje atueleze, tumeona mikakati mingi na kwa hilo nawapongeza ya kuweza kuwakuwa wawekezaji wadogo ndani ya Nchi yetu. Kwa namna moja ama nyingine naweza nikasema bado Wizara hii haina wivu na wafanyabiashara wake wa ndani, Wizara hii haina wivu na wawekezaji wadogo wa ndani kwa sababu wawekezaji hao na wafanyabiashara wanapitia changamoto nyingi na mara nyingi Wizara hii imekuwa ikirudi nyuma kuwaachia Wizara zingine ziweze kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii wafanyabiashara kule nje hata wakipata usumbufu kutoka TRA bado Wizara hii itasema hapana hayo ni mambo ya Wizara ya Fedha sisi tunakaa pembeni. Leo hii wafanyabiashara wetu wanachajiwa hela ya kodi kabla ya miezi sita ambayo ndio takwa la sheria. Wizara hii itakuambia inakaa nyuma haya ni mambo ya TRA, mambo ya Wizara ya Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaomba Wizara hii ianze kuwa na wivu na wafanyabiashara wake ianze kuwa na wivu na wawekezaji wa ndani. Wawekezaji wa nje tunawapenda, wanatupa fursa za ajira, wanatupa mapato kama nchi lakini fimbo ya mbali haiui nyoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunahitaji Wizara hii ije mkakati kama tunavyolinda wawekezaji wa nje, kama tunavyopambana kuhakikisha wanakuja kwa wingi, tuendelee kuwalinda wa ndani ili waweze ku-maintain ushindani. Tuwape nafuu za kikodi tuwajengee mazingira yaliyo salama ili kesho na keshokutwa mfanyabiashara katika eneo lake la kazi akiona Afisa wa Serikali anakuja kumtembelea wasitishike kama wanavyotishika sasa hivi. Waone hawa ni marafiki zao wanataka kuwanyanyua wanataka kuwasaidia katika hili Mheshimiwa Waziri tunaomba utusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kingine nilitaka kuishauri Serikali sasa hivi zaidi ya asilimia 70 ya viwanda vilivyoko katika nchi yetu viko maeneo ya Dar es Salaam na Pwani. Je, Serikali haioni haja ya kuja na mpango wa kutoa incentive kwa wawekezaji wa ndani na nje ili kuweza kuanzisha viwanda vingi zaidi katika maeneo mengine ya nchi? Baba wa Taifa aliona umuhimu wa jambo hili na ndio maana walianzisha viwanda vingi sana katika maeneo mbalimbali ya nchi, mikoa mbalimbali kulingana na mazao au vitu vinavyozalishwa katika mikoa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii viwanda hivyo vingi vimekufa kwa sababu ya ubinafsishaji na wale waliobinfsisha viwanda hivi, wamekiri wenyewe hata wengine wameandika vitabu kwamba kuna sehemu walikosea. Sasa Serikali inajifunza nini ili kutusaidia kwanza kufufua viwanda hivi turudishe viwanda katika mikoa mingine ili tuweze ku-balance maendeleo lakini mimi naamini pia ni hatari sana kwa Taifa letu kama tukifanya viwanda vyote viwepo Dar es Salaam na Pwani tu. Hiyo ni ngumu sana tunatishia kwanza migration watu wote wa Nchi nzima wahamie Dar es Salaam na Pwani lakini pili maendeleo yatakuwepo kule kuliko sehemu zingine zozote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia Mheshimiwa Waziri atatuambia hapa kwamba pamoja na kwamba Nchi yetu ni consumers wakubwa sana wa vitu vingi sana kutoka nchi za wenzetu. Ni kwa nini makampuni haya makubwa ya manufacturing yanaanzisha franchise na branches zake katika nchi za wenzetu zinazotuzunguka na hawaji hapa kwetu.

Mheshimiwa Spika, pia tulikuwa na sehemu za ku-assemble scania katika Nchi zetu na matreka. Viwanda hivyo vimefungwa, vimepelekwa katika nchi za wenzetu. Kuna shida gani katika nchi yetu inayofanya wawekezaji wakubwa badala ya kuleta makampuni haya ku-assemble mali zao hapa inapeleka katika nchi jirani na sisi tunakosa fursa hizo.

Mheshimiwa Spika, nilishawahi kuishauri Serikali, tuna uhitaji mkubwa sana wa kuiwezesha TiRDO na SIDO zetu kama tunahitaji kwenda katika uchumi wa viwanda. Leo hii SIDO katika bajeti iliyopita ilitengewa 1.9 bilion lakini mpaka tunavyozungumza imepewa milioni 400 tu. Hatuwezi tukafika katika uchumi wa viwanda kama TiRDO na SIDO tusipoziwezesha inavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)