Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Abdulhafar Idrissa Juma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtoni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hoja hii tuliyo nayo mezani. Kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali na Waziri mwenye dhamana, lakini kwa nafasi hiyo pia nimpongeze Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake ya kuhakikisha kuwa wawekezaji wanakuja Tanzania na matokeo ya uwekezaji yanatokea, tunaanza kuyaona. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kuhakikisha anasimamia maono ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii tumeelezwa hapa na Waziri wakati anasoma bajeti yake kwamba mpaka sasa mpaka mwezi wa pili bajeti, fedha alizopokea kutoka Wizara ya Fedha hazijafika 60%, lakini Wizara hii ndio ambayo inaleta wawekezaji ambao ndio wanaolipa kodi na kulisaidia Taifa katika masuala mbalimbali. Nitumie nafasi hii basi kuiomba Wizara ya Fedha kwa sababu maziwa wanayoyakamua sehemu kubwa yanasababishwa na Wizara hii, basi Wizara hii waipe fedha kwa wakati hasa fedha za maendeleo ili waendelee kutoa yale ambayo yanategemewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najiuliza pia ipi dhamira ya uwekezaji katika Taifa letu. Michango mingi tumezungumza mambo mengi mazuri kwa ajili ya wananchi wetu, lakini naamini dhamira ya uwekezaji ni kuhakikisha tunakuza ajira katika Taifa letu, ni kuhakikisha tunaiongezea Serikali kipato kwa kodi, lakini ni kuhakikisha bidhaa zinapatikana bila usumbufu kwa wananchi wetu tena kwa gharama nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najiuliza, bajeti ya Waziri imesema bidhaa ya cement au saruji tunazalisha kwa kiwango kikubwa kuliko mahitaji yaliyopo ndani ya nchi, hivyo tunauza nje ya nchi, lakini kwa nini bado bei ya cement kwa mujibu wa taarifa ya Waziri ni Sh.17,600. Hii Sh.17,600 sio fedha ndogo kwa wananchi wetu wanyonge. Najiuliza kama material ya cement yanapatikana ndani ya nchi, wanafanya kila kitu ndani ya nchi, kwa nini bado bei yake haijafika kama bei ambazo tukinunua cement nje ya nchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako baadhi ya marafiki zangu ni wafanyabiashara wa cement, wanaagiza bidhaa ya cement kutoka Iran. Bei ya bidhaa ya cement wanayonunua Iran mpaka wakija kuuza katika soko la Zanzibar, bado bei ni nafuu kuliko bei hii ya cement inayozalishwa ndani ya Tanzania na tunauza nje ya Tanzania. Sasa nini dhamira ya uwekezaji kwa wananchi maskini katika Taifa hili? Kama dhamira ya uwekezaji ni kuhakikisha wanapata bidhaa kwa bei nafuu, nataka Mheshimiwa Waziri aje aniambie, kwa nini pamoja na cement kuuzwa nje ya nchi kutokana na uzalishaji kuwa mkubwa, lakini bado bei yake ni kubwa kuliko cement ambayo inazalishwa kutoka nchi nyingine za na ikafika Tanzania na ikaweza kufanana bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri atueleze kwa nini bei yake isiwe ndogo? Kwa nini bei ambayo mfanyabiashara ataenda kununua Iran asiwe ananunua ndani ya Taifa letu na huyu anasafirisha, analipa kodi na bado mambo mbalimbali yanaendelea kuyafanya. Kwa hiyo nataka kuona dhamira ya uwekezaji itoe matunda kwa wananchi maskini, sio tu peke yake kwa kutoa matunda katika ajira na Serikali kupata kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kidogo nizungumzie suala la ununuzi wa Tanga Cement kama ambavyo baadhi ya wenzangu wamezungumzia na ndio wajibu wetu kwa sababu tumechaguliwa tuje tuishauri Serikali na tusipoishauri tutakuwa hatujatenda wajibu wetu wa kuwawakilisha wananchi wa Jimbo la Mtoni na majimbo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hofu ya baadhi ya Wabunge ambao wameendelea kusimamia ama kuishauri Serikali iangalie mchakato wa Twiga Cement kuinunua Tanga Cement ni hofu ya kibiashara na ni hofu wazi kabisa. Hofu hiyo msingi wake ni sheria tuliyoitunga ndani ya Bunge hili, kama sheria tumeitunga ndani ya Bunge letu kwa dhamira ya kulinda hofu kama hiyo kitu gani kinatufanya Serikali ishindwe kusimamia sheria iliyotungwa na Bunge hili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria imesema wazi katika masuala ya kuingia sokoni kama wakati wanafanya merge haitakiwi uzidi 35%. Mwenye mamlaka ya kusimamia hiyo sheria, watendaji kupitia Wizara hii FCC walikiri kwamba hili jambo likifanyika litazidi 35%, sasa leo kitu gani kilichotokea tena nyuma wakajisahaulisha yale waliyoyasema, tena hata wakajisahaulisha hukumu iliyotolewa na Mahakama ambayo haijatoa kwa kupenda, ni sisi wawakilishi wa wananchi ndio tulitunga sheria hii. Ni sisi wawakilishi wa wananchi ndio tulihakikisha panakuwepo na Mahakama, tulihakikisha panakuwepo na FCC kwa sababu tulijua yatatokea mambo ambayo tunataka kulinda maslahi ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sio dhambi mtu kuuza kitu chake, hata mimi naweza kuuza vitu vyangu, lakini katika Taifa hili kuna sheria, vipo vitu Mwenyezi Mungu amekutunuku wewe mwenyewe, ukivifanya katika Taifa letu ama ukivitumia katika Taifa letu ni makosa kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo kuuza kitu chake mtu sio dhambi, lakini utaratibu wa sheria zetu ufuatwe. Utaratibu uko wazi, wanunuzi wapo, kama vipi itangazwe, mbona tumeona makampuni mengi yaliyo-merge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilijaribu kuanza kufuatilia masuala ya merging ya kampuni wakati Millicom anauza hisa zake kuelekea iliponunuliwa sasa hivi na kampuni ya Axian na nilifuatilia sana kwa maslahi ya kampuni ambayo Serikali ya Zanzibar ina hisa Kampuni ya Zantel. Pale ndipo wakati nafuatilia nikalikuta suala hili pia, nikasema acha nilifuatilie kwa maslahi ya Taifa letu. Nikafuatilia tangu mchakato ulivyoanza, nikajua taarifa za watu na wadau mbalimbali waliokwenda Mahakamani, nikajua hukumu iliyotoka ambayo ilishauri kwamba suala hili lisifanyike kwa maslahi ya Watanzania. Ni Mtanzania gani mwingine huko nyuma ambaye ana maslahi tofauti na maslahi ya Watanzania ambaye anaruhusu suala hili lifanyike tena? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kampuni hii ikachukua ikamiliki soko zaidi ya 42%, wakiamua kuangusha bei ya saruji, wataua viwanda vingine vidogo vya Watanzania na watu wengine mbalimbali, hapo tutakuwa tunasaidia uwekezaji au tunaua uwekezaji? Je, jambo hili likifanyika bei ya saruji ikapanda zaidi kuliko ilivyo sasa hivi, tunawasaidia Watanzania au tumewaua Watanzania?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa inawezekana sheria hii kwa maono ya hawa imeshapitwa na wakati, lakini ndio iliyopo, tufuate sheria iliyopo. Pia niishauri Serikali kupitia Wizara hii na Serikali nzima, suala hili la Tanga Cement kuuza hisa zake na interest ya Twiga kununua tulitumie kama visibility study ama kama maono basi, pana sheria nyingi sana ambazo haziko sahihi kwa mujibu wa mwenendo wa masuala ya kibiashara katika Taifa letu. Kuna sheria za manunuzi nyingi haziko sahihi kwa wakati huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo hili tulitumie kama mfano kwamba Serikali ilete mabadiliko ya sheria mbalimbali ambazo wanadhani yanaweza yakasaidia masuala ya kibiashara. Katika hatua ya sasa, kile ambacho kipo kwa mujibu wa sheria kiheshimiwe ili wafanyabiashara waendelee kuiheshimu Serikali, wawekezaji waiheshimu Serikali, lakini wananchi watambue yale tunayoyashauri na kupitisha katika Bunge ni kwa maslahi ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)