Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kutoa mchango wangu kwenye bajeti muhimu sana hii kwa mustakabali wa nchi yetu. Kama muda utaniruhusu, ninayo mambo matatu.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza, tumeipongeza Serikali, inafanya kazi nzuri ya kuitangaza nchi yetu na kuvutia wawekezaji kuja kuwekeza kwenye nchi yetu, lakini ni ukweli usiofichika kwamba hatujafanya kazi nzuri kwenye kufufua viwanda vilivyokufa. Hasa viwanda vilivyokuwa vikimilikiwa na Umma na tukavibinafsisha na viwanda hivi vingi ni viwanda muhimu sana. Bahati mbaya sana kule Korogwe kuna Kiwanda cha Tembo Chipboard, ni kiwanda muhimu sana, na kimetelekezwa muda mrefu. Mheshimiwa Naibu Waziri aliniahidi humu ndani atakuja kukitembelea, mwaka umekwisha sijamwona. Naomba niishauri Wizara tuongeze nguvu kwa kushikana na Msajili wa Hazina na Wizara za Kisekta.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni kuhusu NDC, Shirika letu la maendeleo. NDC lilikuwa ni shirika muhimu sana na nadhani bado ni shirika muhimu. Lilianzishwa kwa Tangazo la Serikali Na. 90 la mwaka 1969, na limeendelea kuwepo chini ya utaratibu wa Sheria ya Mashirika ya Umma. Hata hivyo kuendelea kuwepo kwa NDC leo, mkazo wake hasa ni maamuzi ya Baraza la Mawaziri, Waraka Na. 6 wa Baraza la Mawaziri wa Mwaka 1996.

Mheshimiwa Spika, waraka ule ulieleza kwamba Shirika liendelee kubaki Serikalini, limilikiwe asilimia mia moja na Serikali, liendelee kufanya miradi hii muhimu ya kimkakati ya kusaidia viwanda vingine. Ni ukweli kwamba, hali na utendaji wa NDC bado hauridhishi. Mheshimiwa Waziri baadaye atakapokuwa anafanya majumuisho kesho, nangetamani kujua, kwa sasa NDC in miradi mingapi? Ni mingapi ambayo inafanya kazi? Ninyi kama Wizara mtuambie, hivi kweli mnaridhika na namna NDC inavyofanya kazi zake? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, moja ya njia nzuri ya kuvutia na kushawishi wawekezaji ni kuwahakikishia utulivu kwenye nchi yetu lakini kuwahakikishia kwamba nchi yetu inafuata utawala wa sheria. Hakuna mwekezaji anaweza kuja kuwekeza kwenye nchi ambaye ana wasiwasi na utawala wa sheria unavyotekelezwa kwenye nchi. Nchi yetu inafuata utawala wa sheria, lakini siku za karibuni kumekuwa na matukio ambayo yanafanywa na baadhi ya Taasisi za Serikali yanayopelekea nijaribu kuamini kwamba pengine taasisi hizi zinakoelekea ni kutokutii utawala wa sheria kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, yapo mazingira ambayo ningeweza nikatoa mfano, lakini naomba nitoe mfano kwenye eneo moja tu. Jana wakati namaliza research yangu hii kwa ajili ya kuchangia leo, ndugu yangu Mheshimiwa Shabiby aliniambia, kama unachangia kesho na mimi nimo. Sasa nataka naye pia anisikilize vizuri.

Mheshimiwa Spika, hapa nataka nitolee mfano sakata linaloendelea la Twiga Cement na Tanga Cement. Hapa nataka nioneshe tu madhara ya kisheria ambayo yanaweza kuleta taswira mbaya kwa wawekezaji.

Mheshimiwa Spika, nitalisema kwa kirefu, naomba unisadie, maana muda hautoshi. Mwezi Oktoba, 2021 Kampuni ya Scancem International na Kampuni ya AfriSam. Scancem International ni subsidiary company ya kampuni yenye hisa nyingi kwenye Kiwanda cha Twiga Cement; na AfriSam ni Kampuni yenye hisa nyingi, asilimia 68 kwenye Kiwanda cha Tanga Cement.

Mheshimiwa Spika, mwezi Oktoba, Mwaka 2021 walitoa joint statement kwamba wamemaliza terms na makubaliano ya kuhamisha hisa za AfriSam kwenda Scancem. Tarehe 2 Novemba, Scancem akaiandikia FCC kuomba approval. FCC wakapokea, wakachakata, na FCC wakaridhia kuhamisha hisa hizi kutoka kwa AfriSam kwenda kwa Scancem lakini walitoa masharti. Yapo kadhaa ambayo FCC waliyatoa, na nimeyasoma vizuri kwenye major analysis report ya FCC yenyewe.

Mheshimiwa Spika, wapo wadau ambao hawakuridhika. Wadau watatu wakaenda kufungua shauri kwenye Baraza la Biashara. Mdau wa kwanza ni Scancem yenyewe akifungia shauri kutokuridhishwa na masharti aliyowekewa na FCC. Mdau wa pili ni Kampuni ambayo inafanya biashara kwa jina la Chalinze Cement na mdau wa tatu ni Tanzania Consumers Protection Associations. Wakafungua shauri kwenye Baraza la Ushindani, shauri linasikilizwa. Mwezi Septemba tarehe 23 Mwaka 2022 Baraza la Washindani likatoa uamuzi kwamba baada ya kupima hoja za pande zote, na kwa kutumia major analysis report yenyewe ya FCC, Baraza la Ushindani likazuia kwamba acquisition hii ya shares za AfriSam kwenda kwa Scancem isimame.

Mheshimiwa Spika, cha kushangaza, uamuzi wa Baraza ukishatolewa kuna namna mbili tu, aidha kuomba review warudishe kwenye Baraza lenyewe au kukata rufaa kwenda Mahakama ya Rufaa. Hayakufanyika. Mwezi Desemba, 2022 Scancem wanaandika tena FCC kuomba kupewa approval ya kufanya acquisition ya hizi shares za AfriSam. Tarehe 11 Februari, 2023 FCC anatoa notice watu wapeleke maoni.

Mheshimiwa Spika, cha kushangaza Baraza hili ni la kwetu, tumeliunda kwa sheria. Utaratibu wa ku-challenge uamuzi wa baraza hili upo. Kwanini utaratibu haukufuatwa? Wameacha, wanakuja ku-file application nyingine mpya.

Mheshimiwa Spika, moja ya jambo ambalo Baraza lilizingatia ni measure analysis report ya FCC ambayo ilionesha kwamba Scancem na AfriSam waki-merge watakuwa na 42.27 ya market share kwenye biashara ya cement, kitu ambacho ni hatari na ni kinyume na kifungu cha 11(1) cha Sheria ya Ushindani. Pia hakuna aliyekata rufaa, mwisho wa siku watu wamekuja kivingine.

Mheshimiwa Spika, jambo hili linatia mashaka sana. Kinachotia mashaka zaidi, mwezi Machi mwaka huu, Taasisi nyingine ya Wizara hii, BRELA ikai-deregister Chalinze Cement ambayo ndiyo challenger mkubwa wa hili jambo, wakitoa sababu kwamba haja-file annual returns.

Mheshimiwa Spika, mimi ni kiongozi, najua suala la annual returns ni suala la kisheria, siwezi kulikataa, lakini hivi ni kweli? Mtuambie, makampuni yote tunayo BRELA sasa hivi yamekidhi? Yana-file annual returns kwa wakati? Mheshimiwa Waziri ukija tunataka tujue, maana kunakuwa na harufu ya jambo ambalo siyo zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na uamuzi huu, mimi binafsi sikatai acquisition, sikatai ku- merge, ni mchakato wa kawaida kwenye biashara kwa ajili ya kuyafanya makampuni yaendelee kufanya kazi vizuri, lakini kwenye jambo hili, kuna maswali lazima tujiulize, mbona kuna kulazimisha sana Twiga kuinunua Tanga Cement? Mbona jambo hili halikutangazwa na halikuwa wazi? Walikaa wakakubaliana; Twiga Cement amekuwa registered kwenye stock exchange, akatangaze, watu waje, kuwe na ushindani. Jambo la pili, wakiungana hawa, hii asilimia ambayo kisheria inakataza ya ku-monopolize biashara hii, ninyi mnalionaje kama Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, sisi watu wa Tanga ni wahanga wakubwa sana wa mambo ya namna hii; ni wahanga wa hizi merge, ni wahanga wa hizi acquisition, ni wahanga wa wabinafsishaji, ni wahanga wa uuzaji wa Mashirika na Makampuni, kwa namna ambayo inakuwa haijanyooka vizuri.

Mheshimiwa Spika, hofu yetu sisi tunaotoka Mkoa wa Tanga, Waziri anajua na Serikali inajua, kwamba eneo la Kiwanda cha Tanga Cement ndiyo kiwanda pekee kime-deposit vya kutosha raw materials za kuzalisha cement kuliko sehemu nyingine yoyote kwenye nchi yetu. Tanga ndiyo inaongoza kuwa na deposit kubwa ya clinker ambayo kwenye uzalishaji wa cement huwa kunainahitajika content yake, ni karibu asilimia 95. Huyu Twiga hana deposit ya namna hiyo. Tuna hofu, anapomchukua huyu, usalama utakuwepo? Biashara hii itaendelea? Brand ya Tanga Cement itaendelea kuwepo? Ndiyo hofu yetu. Tunasema haya, hofu hii siyo kufikirika, yametukuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Korogwe tulikuwa na Kiwanda cha Mrwazi Kamba, aka-merge na kiwanda kingine, aliishia kufungua mashine za Mrwazi Kamba, akaenda kufanya shughuli nyingine. Tanga tulikuwa na Kiwanda cha Amboni Plastic, kikanunuliwa na Kampuni nyingine ya Dar es Salaam mnaijua. Kilipoishia, iko wapi ambayo ni plastic yetu leo Tanga? Haipo, imekufa. Hii ndiyo hofu yetu. Lazima Serikali mjiridhishe ili mtutoe sisi wenzenu kwenye hii hofu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu, nini kifanyike kwenye eneo hili? Moja, kama nchi tuiambie Jumuiya ya Kimataifa, tunaheshimu Mfumo wa Utawala wa Sheria. Uamuzi uliotolewa na Baraza la Ushindani, uheshimiwe. Tunaweza kufanya merger au kufanya acquisition kwenye viwanda hivi kwa kutumia taratibu ambazo zitatutoa kwenye eneo la kutokuheshimu uamuzi wa Mahakama zetu, tunaweza kutafuta watu wengine, tunaweza kuangalia mabadiriko kwenye market shares, tunaweza kuangalia mabadiliko kwenye considerations ya hiyo transfer inayotakiwa kufanyika. Tukifanya hivyo, tutakuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile ushauri wa pili kwenye eneo hili, kama Tanga Cement iko registered kwenye stock exchange, kuna public individuals wanayoiyona hisa mle, kuna shida gani kutangaza huu mchakato ukaenda vizuri? Utangazwe, tuondoe usiri na malalamiko ambayo yalikuwepo. Kwa sababu ukitangaza, faida zake, jambo litakuwa wazi, watu watashindana, tutapata mwekezaji anayeweza kutoa fedha nzuri itakayosaidia kuongeza kodi ya Serikali. Pia akitoa hela ya kutosha, ni rahisi kuwa serious na biashara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mauziano yaliyokuwa yamefanyika ambayo FCC iliyabariki na Baraza likayakataa, wanataka kuuza hisa moja kwa shilingi 3,100, jumla kwa hisa zote ni shilingi bilioni 137 na point kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Serikali, tunawaomba sana, vyombo vyetu vya Serikali na taasisi zetu za Serikali, zisitumike kama sehemu ya kuharibu utawala wa sheria kwenye nchi yetu. Kubwa, zingatieni maslahi ya Taifa, zingatieni maslahi ya walio wengi, zingatieni maslahi ya nchi yetu. Tunachohitaji hapa ni kazi hii iende. Sisi hatutaki kuona Tanga Cement inakuja kufikia mahali inafungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)