Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa inayofanyika kwa kila sekta katika nchi yetu. Kwa kweli ni kazi nyingi zimefanyika na ina matokeo chanya kutatua matatizo ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze ndugu yangu Mheshimiwa Waziri na timu yake nzima kwa kazi kubwa wanayoifanya, wamejitahidi kufanya kazi kubwa na sekta hii sasa inaelekea pazuri na mafanikio yanaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaona eneo kubwa kwenye eneo hili la hotuba yake pamoja na bajeti aliyoiwasilisha tunao wajibu mkubwa kwanza wa kutazama ikama ya watumishi, hali yetu siyo nzuri kwa Maafisa Ugani, na hatuwezi kufanikiwa bila kuwa na wataalam, rasilimali mbalimbali pia vifaa na vitendea kazi pamoja na fedha kwa ujumla. Kwa hiyo naona kuna umuhimu mkubwa kwa sababu eneo lenyewe kwa mfano, Jimbo la Mbulu Mji lina watumishi Watano tu lakini lina Kata 17, lina Vijiji 34 na mitaa 58. Eneo kubwa la Jimbo langu wengi ni wakulima na wafugaji, wale wafugaji wana mifugo, kwa hiyo tatizo kubwa tulilonalo hatuna wataalam. Pia na najua siyo Idara yake yeye lakini wana jukumu kubwa la kuangalia idadi iliyoko kwa watumishi walioko ili tuone namna gani basi wale wachache wanaweza wakahudumia Watanzania na wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kufanikiwa au kupata mafanikio bila kuwa na wataalam hao, vitendea kazi na rasilimali nyingine pia tuje na mpango kabambe, wafugaji wanahama sana, wanahama sana mifugo wanapata matatizo, mifugo yao wananyang’anywa, wanakamatwa misituni, siyo kwamba wanaingia kwenye misitu kwa nia mbaya ni kutokana na majanga ya ukame yanayoikabili ulimwengu kwa ujumla lakini pia mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili Mheshimiwa Waziri kama hatutakaa chini tutapata tatizo kubwa sana kwa ajili ya wananchi wengi na hasa wafugaji hao wanapopoteza mifugo yao na mwisho wa siku wale wa misitu wanavyowakamata wananauza bila hata kuangalia pande zote mbili na athari zinazotokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuona tunajipangaje kwa hali tuliyoona Afrika Mashariki kwenye majanga yale ya ukame mifugo imekufa sana kutokana na mabadiliko ya tabianchi, kwetu tuna kazi kubwa ya kubadilisha koo za mifugo, kupunguza idadi ya mifugo wengi wa kienyeji, kuja kwenye ufugaji wa tija pia kuangalia ufugaji unakuwa na tija na mifugo wanaopungua wale wanakuwa bora zaidi kulingana na mahitaji ya wakati wa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anafahamu kabisa tatizo hili la wingi wa mifugo litazidi kuongezeka kama taarifa yake ilivyosema leo, kama hatutachukua jukumu la kuwa na mashamba darasa ya kupunguza idadi ya mifugo pia unenepeshaji na namna ya kubadilisha koo za mifugo basi moja kwa moja tatizo hilo litakuwa kubwa kwa nchi yetu na mwisho wa siku umaskini utakuwa unaendela kukabili kundi hili la wafugaji ambao ndiyo kundi kubwa na mifugo hawa tunawategemea kwa namna mbalimbali kama ambavyo tunajua katika maisha yetu ya kila siku na ndiyo uchumi na maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii kumkumbusha Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Rais katika ziara yake Mkoani Manyara, aliagiza maziwa yale ya Babati, Tlawi kule Mbulu na Bassotu aliagiza wataalam waende kuangalia namna ya kunusuru yale mabwawa kwa ajili ya shughuli za uvuvi lakini pia uwepo wa rasilimali hiyo. Timu yako ilikuja tunakupongeza sana, ilifanya kazi nzuri sana, ilitembea na wataalam wa Wilaya zetu lakini taarifa ile nadhani sasa ni karibu miezi Sita hazijaweza kurudi kwetu, nakuomba Mheshimiwa Waziri ile taarifa ifanyiwe kazi ili iweze kurudi na tuweze kujua matokeo ya ile taarifa ili tuweze kufanikiwa kwa jinsi ambavyo tunaweza tukaona ina tija na wananchi wetu wakapata mrejesho, wajibu wa wananchi ni nini kwenye ile taarifa au wajibu wa wataalam ni nini na wajibu wa Wizara ni upi, ili kuweza kulinda hizi rasilimali zilizoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza pia Serikali kwa kupeleka pikipiki, tumepeleka pikipiki kwa Maafisa Ugani wa mifugo, ingawa upelekeaji ule haukuwa mzuri kwa sababu mwenye watumishi Watatu alipelekewa pikipiki Tatu, mwenye watumishi Ishirini alipelekewa pikipiki Ishirini. Hii ilitokana na idadi ya watumishi walioko lakini haijaangalia rasilimali mahitaji yalivyo, ukubwa wa eneo na jinsi ambavyo kundi hili la wafugaji linavyohudumiwa na ni kubwa kiasi gani. Kwa hiyo, nilikuwa nafikiri kuna mambo mawili kwenye zoezi hili, kwanza ni kuendela kuona namna ya kuweza kupeleka pikipiki zaidi kwenye yale maeneo ambayo bado hayajapata pikipiki, kwa mfano, mimi nimepata tatu tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia uwezeshaji wa mafuta, Maafisa wetu tumewapelekea pikipiki Mheshimiwa Waziri hawana uwezo wa kupata hayo mafuta ya kuhudumia wananchi, kwa hiyo tuangalie utaratibu gani tunaweza tukafanya ili tuweze kuona pikikpiki hizo zinakuwa na tija kwa manufaa ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee pia kuishauri Serikali kuona utaratibu wa namna gani tunapoanzisha mizani kwenye masoko. Mheshimiwa Waziri amebainisha kwenye hotuba yake kwamba sasa mifugo watauzwa kwa kilo minadani. Je, ni kwa kiasi gani mazingira hayo ya minada na masoko kwenye maeneo yetu tayari yana miundombinu ya kilo? Ili kusiwe eneo moja tu tunatoa huduma hiyo kwa kilo ama soko linaendeshwa kwa vipimo lakini eneo jingine halina miundombinu, pengine timu ingepita nchi nzima au wangeomba taarifa wao kama Wizara ili waone basi maeneo gani hawana mizani na nini kifanyike ili eneo hili la miundombinu ya mizani liweze kupatikana na kwa wingi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine kwa namna ya pekee ninaiomba Serikali itupatie fedha Milioni 130 niliandika barua Halmashauri ya Mji wa Mbulu kujenga masoko Milioni 130, wakati tunapeleka bajeti ile Milioni 130 wakawa wameiondoa. Mheshimiwa Waziri wewe mwenyewe unakumbuka nimekuja ofisini mara kadhaa, nilipokuomba uliniambia nikuandikie barua, nikakuandikia barua ya hali halisi ya Mji wa Mbulu na Halmashauri ya Mji wa Mbulu kwa sababu tayari tuna Kata Kumi ziko Vijijini na hatuna majosho. Kwenye ile barua ulinijibu kwamba itafanyiwa kazi, kwa hiyo naomba Wizara yako itazame upya uataratibu wa ujenzi wa majosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ule ujenzi uliotumika kipindi kilichopita na ukarabati wa kipindi kilichopita haukuwa na tija sana kwa sababu ilionekana ukarabati wa majosho ulikuwa unasimamiwa na Wizara na fedha nyingi hazikuwa zimetoa matokeo chanya kwa maana ya thamani ya Shilingi, kwa hiyo ni jukumu letu wote kuona kwamba walau fedha zile zilizotengwa kwa ajili ya miundombinu ya majosho zinapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchimbaji wa mabwawa. Sababu kubwa ya mifugo kuhama kwanza ni kuwa wengi halafu hawana tija wingi wao kwa mfugaji, pia ukosefu wa malisho na maji. Sababu hiyo inahitaji miundombinu ya mabwawa, kwa hiyo nafikiri kama inawezekana Mheshimiwa Waziri maeneo maalum yaainishwe kwa ajili ya kuchimba mabwawa pia ufugaji uwe wa kupunguza mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kwenye Halmashauri zetu tuna vituo tumejenga nadhani miaka kumi ya huduma za mifugo na kilimo, vituo hivi kwa sasa havitumiki hasa kwenye Jimbo la Mbulu Mji. Utatumiaje vituo sita wakati wewe huna wataalam lakini pia dhana nzima ya kuanzishwa kwake ilikuwa ni namna pekee ya vituo hivyo vitoe elimu kwa wafugaji na semina kwa wafugaji pia na namna ya uzalishaji na uboreshaji wa wafugaji. Kwa hiyo, mimi nadhani kuna haja ya ile miundombinu kutumika, inazidi kuchakaa kama kwenye Jimbo langu inafika karibu sita haitumiki kwa sasa na tulijenga kwa gharama kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwenye mpango huu kabambe wa sekta yako ya mifugo basi na eneo hili lifanyiwe kazi ili vituo vile vipate wataalam ambao ni wabobezi lakini pia wamesomea hiyo fani, watatoa elimu kwa wafugaji na wakati fulani semina mbalimbali na huduma za mifugo zinapatikana kwenye yale maeneo. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana, Mheshimiwa Zacharia Issaay.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Nakushukuru Mheshimiwa Mwenyekiti, basi mengine nitandika kwa maandishi naunga hoja mkono kwa asilimia 100.