Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi jioni hii ili kuchangia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu Subhanah Wataala aliyeniwezesha kusimama na kuweza kuongea mbele ya umati huu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, namshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwezesha Wizara hii ya Mifugo kuwa na bajeti nzuri ambayo inaleta matumaini. Naungana na Taarifa ya Kamati, mashaka yao juu ya utekelezaji wa yale yote waliyoandika kutokana na utekelezaji wa mwaka uliopita ambao unaishia sasa ambapo kwenye Miradi ya Maendeleo mpaka sasa umefika asilimia 58, lakini sina mashaka Waziri wa Fedha yupo, Watalam wake wanasikia, wataisaidia hii Wizara kufikisha malengo yale ambayo yamekusudiwa ili jopo la wasomi waliopo kwenye Wizara hii waweze kufikisha kwa wananchi tunaowatarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini katika Wizara ambayo najua ni muhimu sana ambazo zina wasomi wengi Maprofesa, Madaktari leo wameonesha umahiri wao kwa kuleta bajeti nzuri ambayo inahitaji fedha tu kutekeleza ili uvuvi na mifugo ianze kupiga kasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitaongea jambo moja tu, jambo hili ni suala la mifugo. Tunduru Mwaka, 2008 tulianza kupokea mifugo kutokana na Serikali kuwahamisha wafugaji kutoka Bonde la Ihefu. Wengi walikuwa wanapita njia wanaenda Mkoa wa Pwani na wanaenda Mkoa wa Lindi. Kilichojitokeza wafugaji wengi walibaki katika maeneo ya Namtumbo, walibaki katika maeneo ya Tunduru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa Tunduru walivyokuwa waungwana kwa kuona tatizo lipo mwaka 2017/2018 walitenga maeneo ya vitalu. Vitalu ambavyo vilitengwa vilikuwa jumla 279 ambavyo kila kitalu kimoja kilikuwa na hekari 500 kwa jinsi watu wa Tunduru walivyokuwa na uungwana na kuwapenda wafugaji wenzao, wakaruhusu vitalu hivyo vitengwe katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Tunduru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyojitokeza baada ya makubaliano na wafugaji hao na mfahamu kwamba Mkoa wa Ruvuma ni Mkoa wa Kilimo, kwa hiyo Mkuu wa Wilaya ya Tunduru kutoa eneo kwa ajili ya wafugaji ilikuwa ni uungwana ili nao wenzetu waende kuishi vizuri kama wengine. Kilichojitokeza katika vitalu vile tulikubaliana na wafugaji kwamba kila kitalu kimoja watalipia laki moja na nusu kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitegemea kupata milioni 41 katika vitalu vile kwa mwaka, lakini mwaka wa kwanza vitalu vile vilitoa milioni 15, mwaka wa pili vikatoa milioni tisa, mwaka wa tatu ikatoa milioni sita. Mwaka, 2021/2022 ambapo sasa vurugu za wafugaji kuvamia maeneo ya wakulima ikawa kubwa, basi ili mshike mshike ya kuwarudisha wenzetu kwenye maeneo yao tumefanikiwa kukusanya milioni 18.

Mheshimiwa Mwenyekiti, madhara ya hivi vitalu au wafugaji kutokwenda yamekuwa ni makubwa sana katika Halmashauri yetu ya Tunduru, migogoro ya wafugaji na wakulima imekuwa ni mikubwa. Watu wanakufa kwa ajili ya kugombana, mazao ya wananchi yanaliwa na hawa wafugaji. Pamoja na yote na jitihada nzuri za wenzetu wale wa Tunduru kutoa maeneo yale kwa hiyari na kwa makubaliano, lakini bado wale wafugaji wameendelea kukaa maeneo ambayo siyo rasmi ambayo yamesababisha migogoro na wafugaji wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya madhara yake, maeneo makubwa ya Wilaya ya Tunduru sasa yamegeuka jangwa. Ukienda Jimbo la Tunduru Kusini mpakani mwa Ruvuma mwote, sasa hakuna kilimo kinachoendelea na awali nimesema Wilaya ya Tunduru ni eneo la kilimo. Kwa hiyo naiomba Serikali, mgogoro huu kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru, Madiwani walikubaliana kufuta vitalu hivi kutokana na yale matarajio yao ya kupanga vile vitalu, faida yake haikupatikana. Moja, fedha hazikuweza kupatikana ndani ya miaka hiyo mitano tumekusanya milioni 54 tu kati ya milioni 109 ambazo zilitarajiwa kupata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, wafugaji hawa sasa wamesambaa kwenye mashamba ya watu, migogoro imekuwa ni mikubwa, wengine wameenda mpaka maeneo ya hifadhi ambayo sasa wamelazimisha tembo kurudi kwenye maeneo ya makazi ya watu na kusababisha majanga makubwa kwenye mazao ya wakulima hata vifo kwa baadhi ya maeneo ya watu. Juzi tu Waziri wa Maliasili nilimweleza kwenye eneo langu amekufa mtu mmoja kwa ajili ya tembo, lakini changamoto kubwa maeneo ambayo tembo ndiyo anapaswa kukaa basi wako wale ngo’ombe wanakaa kule, matokeo yake sasa wanasababisha madhara hayo tembo kuja kudhuru maeneo ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali, jambo hili liliwekwa kwa nia nzuri, halmashauri iliamua kutenga maeneo ili isaidie wafugaji wetu wakae, hawataki kukaa kwenye maeneo ambayo wananchi na Serikali imewatengea. Kwa hiyo tunaomba sana Serikali ilichukulie hili, Serikali Kuu na namwomba Waziri nilimwambia mara chungu nzima, naomba safari huu tufuatane mguu kwa mguu, akasikilize kero hizi za ng’ombe kwa wakulima, wafugaji wenyewe pamoja na Baraza la Madiwani ambao waliamua kwa hiyari na kwa azimio kufuta vitalu vile kwa sababu havina msaada wowote, wafugaji wale wote hawapo kwenye maeneo yale yaliyokusudiwa. Pia ile faida iliyotakiwa ipatikane kutokana na ada kwenye vitalu vile haipo, ndani ya miaka mitano tumekosa milioni 154 ambazo zingeweza kufanya shughuli za maendeleo katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la mifugo naomba, tumezungumza hapa suala la wafanyakazi. Jimbo la Tunduru Kusini zina kata 15, ni kata mbili tu zina watalam, halmashauri nzima ina kata 39, tuna Maafisa Ugani upande wa mifugo 14, watatu wako pale halmashauri, wawili wako kusini na wengine waliobaki wako kaskakazini. Sasa naomba hili ufanisi mzuri uonekane kwenye kazi hii ya mifugo, basi tuongeze idadi ya Maafisa Ugani kwenye maeneo mbalimbali ya kata zetu ambao watasaidia kuwapa msaada hao wafugaji wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine hawana vitendea kazi. Nashukuru kwenye Hotuba ya Waziri ameongea vizuri kwamba watanunua pikipiki kuwawezesha, lakini siyo pikipiki. Tunduru ni kubwa eneo lake linazidi Mkoa wa Mtwara. Kwa hiyo kumpa Afisa Ugani pikipiki atoke Tunduru Mjini amfuate mkulima zaidi ya kilomita mia ni adhabu kubwa, hasa unaposema Afisa Ugani wa Wilaya. Naomba Waziri ajitahidi kwenye bajeti yake kama hakupanga basi atuchomekee hata angalau kigari moja kisaidie kutoa huduma kwenye maeneo mbalimbali pamoja na hizo pikipiki ambazo zitawasaidia Maafisa Ugani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bajeti, nimeona Waziri ametenga maeneo kwa ajili ya mashamba darasa mia moja. Tunduru tuna shamba pale Masonya, tuna shamba Mowesi, Shamba la Masonya lina zaidi ya ekari 3,200, linafaa kabisa kuweka shamba darasa. Tunaomba katika mpango wa Waziri, basi aliangalie kwa huruma shamba hili, liko idle, mkulima na mfugaji mmoja ana ng’ombe wasiozidi 2,500 tuseme, yuko pale, liko idle kwa hiyo linaweza kufaa kuwa shamba darasa, likawasaidie wakulima wadogo wadogo ambao wako ndani ya Wilaya ya Tunduru ili waweze kujifunza. (MakofI)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nanaunga mkono hoja. (Makofi)