Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anazozifanya hata wananchi kule Ludewa wanaziona na leo wamefurahi kuona kuna Wananchi wa Ludewa walipewa mwaliko wa Mheshimiwa Waziri kwa ajili ya mikopo ya maboti. Hili ni jambo la kumpongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumpongeze pia Mheshimiwa Waziri, Naibu wake na Katibu Mkuu Professor Shemdoe, hongereni sana kwa kazi nzuri. Sisi Ludewa tuna kata nane ambazo zimezunguka Ziwa Nyasa, kuna Kata ya Lumbila, Kilondo, Lifuma, Lupingu, Iwela, Manda na Ruhuhu. Kwa hiyo, kuna idadi kubwa sana ya wananchi ambao ajira yao inategemea maji, inategemea kwenye uvuvi. Kwa hiyo, bajeti hii ni muhimu sana ndiyo maana nimesimama niweze kuwasemea wale wavuvi wa jimboni kwangu na wa maeneo mengine hapa nchini Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikisoma ile Hotuba ya Bajeti ya Mheshimiwa Waziri nimeona amezungumzia mwaka 2021, Sekta ya Mifugo ilikua kwa 5% na kuchangia 7% ya Pato la Taifa. Hii ipo kwenye ukurasa wa 69 wa Hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Vilevile ameonesha kwamba Sekta ya Uvuvi kwa mwaka 2022 ilikua kwa 2.5% na ilichangia 1.8% kwenye Pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane na Wabunge wenzangu waliozungumzia Sekta hizi mbili kwa maana ya Uvuvi na Mifugo kwamba sekta hizi zinazo nafasi na uwezo mkubwa wa kuchangia zaidi kwenye Pato la Taifa iwapo zile changamoto ambazo zinaikabili Wizara hii kama ambavyo Mheshimiwa Waziri ameainisha na kamati imeainisha zikafanyiwa kazi na kuongezewa fedha kama ambavyo Wajumbe wengine wamependekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake amezungumzia ana upungufu mkubwa wa wafanyakazi. Hili hata kule Ziwa Nyasa Jimboni kwangu tuna watumishi wawili tu ambao ni wataalamu wa uvuvi katika kata nane. Kwa hiyo kutegemea hapa tutapata tija ni changamoto sana. Kwa hiyo, ningeiomba sana Serikali iweze kuongeza watumishi kwenye Sekta ya Uvuvi ili waende kusimamia tija kule kwa wananchi ambako wanafuga samaki na wanavua kutegemea asili kwenye Ziwa Nyasa na maziwa mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia hata vyuo ambavyo vinatoa mfaunzo ya uvuvi ni vichache sana hapa nchini hasa hizi kada za kati. Ukienda pale Sokoine utaona wana kitengo wanafanya vizuri lakini hizi kada za kati wale ndiyo hasa ukimwambia nenda Lumbila ukahudumie wananchi wa kule atakwenda na atafanya kazi yake kwa uaminifu mkubwa. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Serikali kuongeza hizi kozi za kati ngazi ya cheti, ngazi ya diploma ili tupate wataalamu wengi zaidi na hii itasaidia sana kuongeza mchango wa Sekta ya Uvuvi kwenye Pato la Taifa vilevile kuongeza ajira kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile imebainika kwamba Watanzania milioni 4.5 wanategemea Sekta ya Uvuvi. Hii ni idadi kubwa ya Watanzania ambao tunatakiwa tulinde ajira zao kwa nguvu zote. Kwa hiyo, tukiwaongezea wataalam tukawapa vitendeakazi, sekta hii kwa kweli inaweza ikakua kwa kasi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine ambalo ningependa kulizungumzia ambalo Wabunge wengi pia wamezungumzia ni eneo la kuanzisha kwa mamlaka ambayo itasimamia Sekta ya Uvuvi, itasimamia Sekta ya Mifugo. Tukiangalia upande wa maliasili, samaki ni maliasili, misitu ni maliasili. Kwa hiyo, misitu, wanyamapori wana mamlaka ambazo zinasimamia kwa sababu kule kunakuwa na wataalam ambao wao kazi yao wakilala wakiamka wanafanya mambo kwa utaalamu kwa kuzingatia tafiti tukamwacha Mheshimiwa Ulega anahusika na sheria na mambo ya sera. Hii mamlaka sasa ndiyo itasimamia kule kwenye uvuvi kwa sababu samaki nao tumesema ni maliasili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, watapewa mafunzo kwa sababu shughuli ya kwenye maji inahitaji ukakamavu kidogo. Kwa hiyo, ni muhimu wakapata pia mafunzo kama ambavyo imefanyika kwenye Sekta ya Misitu. Kwa hiyo, tukiangalia mwaka ule 2009 katika Gazeti la Serikali Na. 135 ilianzisha hiyo Mamlaka ya TAWA kwa hiyo nimshauri sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana na Sekta hii ya Mifugo na yeye nimeona kwenye ukurasa wa 106 wa hotuba yake amezungumzia dhamira yake ya kuanzisha hii mamlaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, jambo hili ni muhimu sana ambalo Serikali ningeishauri iweze kutoa msukumo wa dhati kuhakikisha mamlaka hii inaanzishwa ili Sekta hii ya Mifugo, Sekta ya Uvuvi iweze kuajiri Watanzania wengi zaidi ambao vijana wetu sahizi wanahangaika ajira lakini vilevile itoe mchango mkubwa kwenye Pato la Taifa letu. Hii 7% bado tuko chini sana ukizingatia takwimu zinaonesha kwamba nchi yetu ni nchi ya tatu kwa wingi wa mifugo barani Afrika. Kwa hiyo, nadhani tulipaswa tunufaike sana na idadi hii kubwa ya mifugo ambayo tunayo hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ambalo ningependa kushauri Serikali ni eneo la uhifadhi wa mazingira kwenye maziwa yetu haya ili kuweza kuhifadhi maeneo ya kuzalia kwa samaki, mazalia. Kwa sababu wananchi wengi bado wanategemea ule uvuvi wa asili (nature). Kwa hiyo, ningeishauri Serikali kupitia Wizara hii ya Mifugo ishirikiane na Wizara inayohusika na mazingira waweze kuhifadhi vizuri yale mazalia ya samaki kwenye maziwa yetu ili kuweza kufanya samaki wawe wengi zaidi na wakati ule mpango mwingine wa ufugaji wa samaki nao unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo maeneo yote ambayo yanafaa kwa ajili ya ufugaji wa samaki kwenye vizimba labda kama watatumia njia ya kufuga nchi kavu. Kwa mfano kama Ziwa Nyasa lina mawimbi makali sana kwa hiyo kuna maeneo ambayo yanahitaji Wizara iende ikayafanyie utafiti zaidi iweze kuongeza nguvu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tulisema hizi sheria za uvuvi ndizo zinazosimamia ufugaji wa samaki. Hii ni changamoto kubwa sana, kwa hiyo ningeshauri Serikali iweze kufanyia marekebisho tuwe na Sera, kanuni na sheria zinazosimamia eneo la ufugaji wa samaki kwa sababu utaangalia kuna nyavu ambazo zinatumika kutengeneza vizimba. Ukija kuangalia kwenye Sheria ya Uvuvi ni nyavu haramu. Kwa hiyo, tunakuwa tunajichanganya na hapa nchini hazipatikani kwa hiyo wananchi wanahangaika kwenda kununua nchi jirani kwa njia za magendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana tunaona hapa kuna umuhimu mkubwa sana kwa Serikali kufanyia kazi hizi kanuni licha ya kuwa walifanyia mabadiliko mwaka 2020 lakini hili eneo sasa la ufugaji wa samaki ni vyema lilkawa na sheria zake mahususi na kanuni zake ikiwezekana na sera yake ambayo itaenda kuangalia.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru naunga mkono hoja. (Makofi)