Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa ninampongeza Kaka yangu Mheshimiwa Ulega pamoja na Naibu Waziri, Katibu Mkuu wa Wizara hii na timu yote ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Nimekwenda kwenye mabanda pale nje kumenoga kweli kweli, kwa kweli Mheshimiwa Waziri umetuthibitishia kwamba hii ni Wizara ya vitoweo, hongereni sana kwa ubunifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuchangia kwenye eneo la sekta hii ya maziwa. Jimbo la Lupembe na Mkoani Njombe kwa ujumla wake huko nyuma tulikuwa na kiwanda kizuri sana cha maziwa, kiwanda hiki cha maziwa kilikuwa kinatoa ajira nyingi kwa wananchi wetu, kilikuwa kinatoa kodi kwa Serikali na kadhalika, lakini kiwanda hiki ambacho kilikuwa ni msaada mkubwa kwenye kuchakata mazao ya mifugo leo hii kimefungwa. Mkoa wa Njombe tangu wakati wa Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere kule Makete ranch ya Kitulo kulishakuwa na ranch nzuri kwa ajili ya mifugo na Mheshimiwa Waziri anajua, ranch hii ya Kitulo ilikuwa ni kwa ajili ya kunenepesha ng’ombe tulikuwa na ng’ombe wakitoa maziwa mpaka lita 40 kwa siku, ranch hii imeendelea kushuka imeendelea kuwa haina tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimuombe Mheshimiwa Waziri kwa sababu amekuja kuipa nguvu sekta hii ni vizuri akaenda Mkoani Njombe akasaidie kufufua kiwanda cha maziwa kilichoko Njombe, Serikali kupitia Waziri kwa sababu mnayo nia njema ya kupeleka mbele sekta hii ya mifugo na uvuvi ninaamini kiwanda hiki ambacho kinapigwa danadana, kimejawa na mambo mengi, wataalam wako Mheshimiwa Waziri ukiwauliza wanajua, ukifia Njombe utakuja kukikwamua kiwanda hiki ambacho kipo na mitambo ipo, badala ya kupanga mambo mapya ningeomba bidhaa tulizonazo, vifaa tulivyonavyo tukaboreshe vianze kutoa ajira kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nataka nitumie nafasi hii pia kupitia wewe nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake njema ya kuboresha sekta ya mifugo na uvuvi. Halmashauri ya Njombe kwa mara ya kwanza Halmashauri ya Njombe DC tumepata mradi wa mabwawa manne ya kufuga Samaki, huu ni mpango ambao sekta hii ya uvuvi na mifugo imeamua kwenda mbele na kuboresha maisha ya wananchi wetu. Nikuombe Mheshimiwa Waziri kwa sababu umeanza vizuri, utakapokuja Njombe utembelee mabwawa haya ili uone pia namna ya kuongeza fedha na kuongeza tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la lingine ninataka pia niseme kuhusu mifugo kwamba ni kero. Nakubaliana na Waziri kwamba mifugo ni utajiri, mifugo ni uchumi lakini mifugo pia ni kero. Zipo kero tatu kwenye mifugo, kero ya kwanza hii mifugo imekuwa sababu ya ugomvi kati ya wakulima na wafugaji. Jambo la pili, kero kwenye mifugo ni kwamba mifugo imekuwa ni sababu ya ajali mbalimbali barabarani, Wabunge ninyi mnakumbuka Mheshimiwa Kigwangalla yuko hapa alipata ajali kwa kugongana na mifugo barabarani, Mheshimiwa Waziri ujumbe wangu ni nini, tunakuomba uibadili sekta hii ya mifugo…

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Mwita Getere.

TAARIFA

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba mifugo siyo kero, ila wanaotunza mifugo hiyo ndiyo wana kero, kwa hiyo watu waelimishwe tu kwamba mifugo haina akili watu ndiyo wanaitumia.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Edwin Swalle unaipokea hiyo taarifa?

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa heshima ya Mheshimiwa Getere ninachosema ni kwamba Mheshimiwa Waziri ninakuomba uifanye sekta hii kuwa na utulivu tusiache mifugo iendelee kurandaranda kila mahali, leo hapa Dodoma kwa mfano ukiingia katikati ya mji mchana unaweza kuona ng’ombe, hata ukiingia Dar es Salaam unaweza ukaona mbuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu ni nini? Kwa kuwa Serikali yako maeneo mengi tumepanga maeneo kwa ajili ya majumba ya makazi, yako maeneo kwa ajili ya mahoteli, ninayo imani kwamba Mheshimiwa Waziri mnaweza kupanga vizuri maeneo kwa ajili ya malisho na maeneo kwa ajili ya wakulima. Jambo hili Mheshimiwa Waziri linawezekana kwa dhamira njema ambayo unaweza kuwa nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia jambo lingine kwamba mwaka huu kwenye mbio zetu za Mwenge, kauli mbiu za mbio za Mwenge mwaka huu 2023 zinasema;

“Tutunze mazingira, tuokoe vyanzo vya maji, kwa ustawi wa viumbe hai na uchumi wa Taifa”. Kauli mbiu hii ya kutunza mazingira inaendana na kudhibiti uzuraraji wa mazao ya mifugo, kwa hiyo nikuombe Mheshimiwa Waziri ujitahidi kuweka mpango mzuri ili kusimamia sekta hii ya Mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu na hili ni muhimu sana, nimesoma kwenye taarifa ya Waziri hapa amesema namna sekta ya mifugo na uvuvi inavyochangia uchumi wa Taifa. Mifugo inachangia uchumi kwa asilimia Saba na lengo la Serikali na Waziri na timu yake yote ninaamini tunataka kulikamata soko la Kimataifa, lakini nitoe wito kwenye Wizara hii kwamba soko la Kimataifa lina vigezo vya kuuza bidhaa za wanyama duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya vigezo hivyo ni kuwatambua wanyama hawa kuwasajili na kujua hawa wanyama ni mali ya nani, huwezi kupeleka biashara kwenye soko la Kimataifa bila kujua mmiliki ni nani kwa usajili alionao. Ninakuomba Mheshimiwa Waziri umesema kwenye taarifa kwamba mlikuwa na mpango wa kuwatambua wanyama na mpango huu umesimamishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwako mnaweza kukaa kwenye Wizara yenu kama gharama ni kubwa ya kulipia usajili na utambuziwa wa Wanyama, mnaweza kama Serikali kusaidia kama ambavyo tumefanya kwenye sekta yetu ya kilimo, mkatoa ruzuku kwa kiasi fulani ili mkulima alipe bei kidogo. Kwa hiyo, kama ni 1,500 Serikali mnaweza kutoa ruzuku shilingi 1000 na huyu mfugaji akatoa 500 au 300, lakini ni lazima mifugo yetu itambuliwe, ifanyiwe ufuatiliaji ili soko la Kimataifa liweze kutuelewa kwamba tuna sifa ya kuingia kwenye soko la Dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine nataka niseme kidogo kuhusu mpango wa mbele wa kutoa elimu ya ufugaji. Hivi karibuni kumekuwa kuna mpango wa Serikali wa kujenga vyuo vya VETA nchini, vyuo vya VETA ni kutoa ufundi na ujuzi kwa wananchi, ninataka nimuombe Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi na Wizara yake kwamba washirikiane na Wizara hii ya Elimu na Sayansi vyuo hivi vya VETA kwenye maeneo mengine ni Mikoa ya wakulima, Jimbo la Lupembe kwa mfano tumepata chuo cha VETA kile chuo ni muhimu kikawa chuo pia cha mifugo na uvuvi ili wananchi wetu wasome habari ya umeme, wasome habari ya ujenzi lakini pia wasome na kilimo kwa sababu kilimo ndiyo shughuli yao ya kila siku kwenye maeneo yale, tukifanya hivyo vyuo hivi vitakuwa na tija kwenye kila eneo ambako vipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine pia kwa kumalizia nitumie nafasi hii kumsihi sana Mheshimiwa Waziri wetu wa Mifugo na Uvuvi, kwamba ubunifu alioanza kuufanya leo kwa kutuonesha kwa vitendo uzuri na ubora wa Wizara hii uigwe na Wizara nyingine huko mbele ambako tunakwenda, ubunifi huu Mheshimiwa Waziri ndiyo kitu pekee ambacho kitakupeleka mbele na ktoa tija kwenye sekta hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo nashukuru sana, naunga mkono hoja.(Makofi)