Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko na Naibu wake Dkt. Stephen Kiruswa na watendaji wote wa Wizara na taasisi zinazosimamiwa na Wizara na wadau wa sekta ya madini kwa kazi nzuri wanazofanya.

Mheshimiwa Spika, mimi nitachangia kwenye uchimbaji wa mawe ya kutengeneza saruji (gypsum), na bidhaa nyingine huko Makanya, Mkoani Kilimanjaro, na maeneo mengine hapa Tanzania. Madini haya ni muhimu kwani hugusa maisha ya Mtanzania moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, saruji itokanayo na madini haya hutumiwa na idadi kubwa ya Watanzania kwenye ujenzi wa nyumba, miundombinu ya maji ya kunywa na umwagiliaji, barabara na maghala.

Mheshimiwa Spika, mawe ya kutengeneza saruji, chaki, gypsum powder, Plaster of Paris (P.O.P) na mbolea ya kilimo ya kupambana na magadi hupatikana katika eneo la Makanya na maeneo mengine ya Tanzania kama Kilwa (Cement ya Dangote), Dodoma, Tanga, Singida na maeneo mengine. Katika maeneo haya kuna kiasi kikubwa cha rasilimali ya mawe ambayo hutumika kutengeneza saruji (sementi) viwandani. Kwa maoni yangu, bado uchimbaji huu haujawa na tija tarajiwa.

Mheshimiwa Spika, wapo watu wengi ambao wameibukia kuwa matajiri wakubwa kutokana na kujihusisha na kazi hii ya uchimbaji wa mawe haya ya kutengenezea saruji (cement) katika eneo la Makanya na maeneo mengine yaliyotajwa hapo juu. Kwa maoni yangu, madini haya hayajapewa kipaumbele kikubwa, kwani bidhaa zake kama saruji ina mchango mkubwa sana katika maendeleo ya nchi yetu. Idadi ndogo ya wachimbaji wazawa hushiriki katika biashara hii muhimu kutokana na changamoto mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kazi ya kuchimba mawe haya ni ngumu na sasa ni wakati muafaka wa kuwashirikisha wachimbaji wazawa kwa kuwawezesha kushiriki katika shughuli hii ili kujiongezea kipato na kuchangia katika pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, changamoto inayowakabili wachimbaji wazawa ni matumizi ya teknolojia za kizamani, upatikanaji wa zana za kisasa za uchimbaji, na mitaji midogo kwa kundi hili.

Mheshimiwa Spika, bei ya zana za uchimbaji ni kubwa, na vilevile hutozwa kodi kubwa. Hapa nchini Tanzania ni wafanyabiashara wachache wanajihusisha na biashara ya zana za uchimbaji kutokana na kodi nyingi kwenye bidhaa hizi. Kwa hali ilivyo sasa hivi vifaa hivi vikiingizwa nchini wachimbaji wadogo wadogo wazawa hushindwa kumudu gharama.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto nilizotaja hapo juu, naishauri Serikali yafuatayo; kwanza, Serikali ihamasishe wazawa kuwekeza katika uchimbaji wa haya madini ya gypsum; pili, Wizara ya Madini kwa kushirikiana na Waziri wa Fedha washauriane na kuondoa kodi kwa wazawa wanaoagiza na kufanya biashara ya vifaa ili viingie kwa wingi, madini yachimbwe na wengi na kodi iongezeke kutoka kwenye mauzo ya gypsum na cement badala ya ile ya kwenye vifaa.

Tatu, tunazishukuru benki za biashara kwani zimeongeza mikopo kwa wachimbaji wa madini wadogo wadogo kutoka shilingi bilioni 36 mwaka 2022 hadi shilingi bilioni 145 kufikia mwezi Machi, 2023. Hata hivyo, ninaishauri Serikali iendelee kujadiliana na benki za biashara nchini ili ziendelee kutoa mikopo ya mitaji ya kuchimba na ya kununulia vifaa vya kuchimba mawe ya kutengeneza cement kwa wachimbaji wadogo wadogo kwenye maeneo yote husika nchini.

Nne, Serikali ifanye tafiti za kina katika maeneo mengine Mkoani Kilimanjaro na maeneo mengine hapa nchini ili kujua maeneo mengine yenye madini ya gypsum. Utafiti huu uoneshe madini yako maeneo gani ili kurahisisha uchimbaji kwa wachimbaji wazawa. Kwa kufanya hivi, kanzidata hiyo itatumika kurahisisha uwekezaji na uchimbani na kuipatia Serikali kipato cha uhakika.

Mheshimiwa Spika, tano, Serikali ihamasishe wawekezaji wa ndani na nje kujenga viwanda vya kuzalisha vifaa na mitambo ya kutumika migodini hapa nchini; na sita, Serikali ihamasishe wawekezaji wajenge viwanda vya saruji katika maeneo yaliyo karibu na machimbo ili kupunguza gharama za kusafirisha mawe.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.