Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuweza kunipa nafasi nami ya kupata kuchangia katika bajeti ya Wizara ya Madini 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa namna ambavyo anaendelea kutengeneza mazingira bora ya wawekezaji, lakini na wawekezaji wa ndani na kuendelea kuangalia Wizara ya Madini kama sehemu ya kuongeza kipato ndani ya Taifa letu. Vile vile bila kusahau niendelee kupongeza kazi kubwa ambayo inafanywa na Waziri, Mheshimiwa Dotto Mashaka Biteko pamoja na Naibu wake na timu nzima ya Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, sisi watu wa Manyara tunasema tunamwombea kwa Mungu afya njema lakini kura tulishamaliza kupiga, tunasubiri sanduku tuletewe ili tuweze kuzidumbukiza na ni kura za ndio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulifanya hivyo kwa sababu, tunamshukuru alituletea zaidi ya Shilingi Bilioni 5.9 kujenga one stop center ya ununuzi wa madini katika Mji wa Mererani. Vile vile, tunaishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kupitia kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, mpaka sasa tayari tumeshapokea kiasi cha fedha cha Shilingi Bilioni 1.59 ambao ujenzi umeshaanza ghorofa la kisasa la soko liliwekwa pale katika Mji wa Mererani na sisi tumepata sehemu ya kuwa tunakwenda kupigia picha kwa sababu ni kazi nzuri ambayo imefanywa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi floor hizo nne tayari Serikali ya Mkoa imeshaanza kupata maombi ya wafanyabiashara, yaani jengo halijakamilika lakini wafanyabiashara tayari wamekuja wanahitaji kupangisha. Hakika hongera sana kwa Wizara ya Madini, ahsante sana Rais Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kupongeza jitihada zizo, tuendelee kumshukuru kwa namna ya kipekee, Watanzania wote kwa ujumla kwa sababu wanaochimba Mererani ni Watanzania kutoka pande zote za nchi yetu. Tuna kila sababu ya kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweza kuruhusu Kitalu C ambacho kilifungwa zaidi ya miaka minne huko nyuma na sasa vijana zaidi ya 100 wameshapata ajira na ajira zinaendelea kutoka, lakini pia kipato kinaendelea kuongezeka kwa wananchi mmoja mmoja, kwa wachimbaji, lakini pia pato kubwa kwa Serikali. Ahsante sana Rais Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuishukuru Serikali yetu Tukufu ya Chama cha Mapinduzi, niombe Serikali mambo yafuatayo katika Mji wa Merelani kwa maana ya machimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana, Mji wa Mererani ili kupata madini yale kupasua miamba kunatumia baruti na vumbi ni kubwa na wananchi wetu wanapata ugonjwa wa TB. Katika Mji wa Merelani TB ni kubwa sana na ukiangalia kwenye takwimu mara ya mwisho mwezi wa Nane mwaka 2022, watu waliojitokeza kupima ni watu 2,024, lakini watu waliokutwa na maambukizi kwa wale ambao walipima kwa hiari ni watu 382 na ambao wanapata dawa mpaka sasa ni watu 371.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi letu kwa Serikali, kwanza kabisa tunaomba wachimbaji hao wadogo matibabu yao na hasa vumbi hili na athari ya ugonjwa wa TB, matibabu wanaenda kupata katika Mkoa wa Kilimanjaro Hospitali ya Kibong’oto. Mheshimiwa Waziri tunalo eneo kubwa linaloweza kujengwa hospitali na kuweza kuwasaidia idadi kubwa ya wananchi walioko Mererani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia shift moja wanapoingia kufanya kazi kwenye ile migodi ni zaidi ya wananchi 2,000 mpaka 3,000 na idadi kubwa ni kundi la vijana. Kwa hiyo, ili tuweze kulinda rasilimali na nguvu kazi ya vijana wa Kitanzania, basi tuweze kupeleka huduma ya afya katika Mji wa Mererani kwa sababu ni idadi kubwa ya vijana wa Kitanzania wanafanya kazi pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo Mheshimiwa Rais nia yake ni njema, dhamira yake ni njema na lengo ni jema. Sambamba na kujengwa Mji wa One Stop Centre pale Mererani, tumuombe sasa Wizara ya Maji iende sambamba na ujenzi huu ili kukuza, kwa sababu mji ule sasa hivi una watu wengi, una wakazi wengi ambao ni Watanzania kutoka maeneo yote, lakini changamoto ya maji ni kubwa. Tuendelee kuomba japo tunamshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji anaendelea kupambana, lakini bado tuombe speed iongezeke ili kuweza kutatua changamoto hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunaomba ujenzi wa barabra. Barabara zilizopo ni mbovu, zimekuwa ni shida. kwa hiyo, tunaomba sana Wizara nyingine ziende sambamba na lengo la Mheshimiwa Rais la kuhakikisha One Stop Center hiyo inakuwa ni ya kisasa na Mji wa Mererani unafanana na kile ambacho kinatoka katika pato la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuiombe GST iweze kuja kuendelea kufanya utafiti, lakini pia kuleta vifaa. Ndani ya Mkoa wa Manyara hatutegemei tu madini ya tanzanite, yapo madini mengi mfano kule Simanjiro kuna green garnet lakini changamoto iliyopo ni umeme, barabara pamoja na maji. Kwa hiyo, tukipata umeme itasaidia sana wananchi wadogo wadogo kutokutumia gharama za kutumia jenereta na kununua diesel. Kwa hiyo, tunaomba sana ili kuendelea kukuza pato la wananchi na pato la Taifa, basi miundombinu kama umeme, maji yaweze kupelekwa pamoja na barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo madini mengine ya dhahabu kule Mbulu ambapo mashapo yapo ya kutosha, lakini wananchi hawa wa kawaida wadogo wadogo hawana sehemu rasmi ambapo wanaweza wakatoboa wakajua mwamba upo hapa. Kwa hiyo, tuiombe sana GST iweze kuja kufanya kazi ili kuwarahisishia wananchi wetu wadogo wadogo wafanye kazi si kwa muda mrefu, lakini kazi yenye faida na kulinda uchumi wao mdogo na mtaji wao mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo madini Kiteto, Mkoa wa Manyara karibu maeneo yote yana madini, lakini kwa namna ya kipekee niongelee Wilaya ninayotoka Wilaya ya Hanang. Hanang ukienda Gehandu, ukienda Mogitu, ukienda Gendabi, tuna madini ya chumvi wanakuja watu kutoka nchi zingine wananufaika, tunakuomba sana Mheshimiwa Waziri tunaomba mtoe support kwa wawekezaji wetu wadogowadogo wa ndani ili waweze kukuza uchumi na waweze kuvuna rasilimali hii kubwa katika nchi yetu na iweze kuleta mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao uwezo wa kuchimba simenti kule badala ya kuendelea kutumia simenti kwa kununua kwa bei ghali, tunaweza kuwaleta watu kule na wakaweza kutusaidia. Hali kadhalika ipo chumvi ya kutosha tunaomba sana Serikali yetu sikivu ituletee wawekezaji ili na sisi siku moja wananchi wa Hanang waweze kuona kuna kiwanda kiko kule na waweze kupata ajira na kusaidia wananchi wa chini na kusaidia pato la Taifa la nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana kwa heshima na taadhima Wizara ya Kazi, mwanzoni kulikuwa kuna kampuni ya Tanzanite ambayo ilikuwa na wafanyakazi wengi sana na kamapuni hiyo ilikuwa ina muunganiko na STAMICO lakini baada ya kampuni hiyo kuondoka ama kuacha kufanya kazi ya uchimbaji, zaidi ya Watanzania wafanyakazi 540 wanadai zaidi ya Bilioni 2.5 tunaiomba sana Wizara ya Kazi iendelee kuwasikiliza wananchi hawa itatue kero, maana imekuwa ni kero kwa viongozi wetu wa Chama cha Mapinduzi wanapokuja Mkoani wananchi hawa ndio wamekuwa ni kimbilio lakini tunaiomba sana Serikali kupitia Wizara ya Kazi iweze kuliangalia jambo hili na wananchi wale wajivunie kufanya kazi ndani ya nchi yao ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia mabadiliko ya Sheria ya Muundo wa Utumishi, tuombe sana Mheshimiwa Waziri mabadiliko haya hebu yamalizike mchakato wake ili kuweza kuwasaidia watumishi wako wa Wizara kuweza kupata kipato wanachostahili, kwa sababu kazi wanayoifanya ni kubwa wanaletea nchi yetu kipato kikubwa, lakini maslahi yao ukienda kuangalia watumishi hawa hakika hayastahili na tunahitaji kupata watu ambao watazidi kuwa waaminifu, kuwa wazalendo japo sasa hatuna shaka na uadilifu wao na uzalendo wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima na unyenyekevu mkubwa mimi binafsi na ninaamini na Watanzania wote na hasa Wabunge tuliomo huku ndani, ni nani kama Samia Suluhu Hassan, ni nani kama Samia Suluhu Hassan? Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia tunampongeza sana mama yetu kipenzi Rais Samia, Watanzania tumemuelewa Serikali ya Awamu ya Sita inafanya kazi, tunayaona wananchi huko chini, mimi kama kijana na vijana wenzangu tutasema mema yanayofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan. Ahsante sana Serikali ya Awamu ya Sita, ahsante sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Ahsante kwa kunipa nafasi. (Makofi)