Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Katiba na Sheria

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Daktari Jaji Feleshi kwa maelezo aliyoyatoa pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri Pauline Philipo Gekul kwa maelezo ambayo ametoa katika kujibu hoja mbalimbali za waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongee kidogo hoja aliyoizungumzia Mheshimiwa Agnesta kuhusiana na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora. Kwa mujibu wa Mkataba wa Paris umeweka viwango kwamba Tume za Haki za Binadamu zianzishwe ama kwa Sheria ama kwa Katiba, sisi Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuona umuhimu wa Tume hii tumeanzisha kwa nyaraka zote mbili Sheria pamoja na Katiba. Tumeiweka kwenye Katiba ili isiweze kuguswa na kuchezewa na mtu yeyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitendo cha kuweka Tume hii katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni dhamira wazi kabisa kwamba Serikali imeipa Tume hii heshima kubwa sana na kwamba haiwezi kuchezewa au kufutwa na mtu yeyote kirahisi. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Agnesta akubaliane nami kwamba Tume hii ni Tume ambayo sisi kama Serikali tunaiheshimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikiongeza Bajeti ya Tume kila mwaka. Mwaka 2021/2022, Bajeti ilikuwa ni bilioni 5.5, lakini leo nasimama hapa mapendekezo ya Bajeti endapo Bunge hili litaridhia na endapo Mheshimiwa Agnesta ataunga mkono ni Shilingi Bilioni 8.1 ongezeko takribani ya Shilingi Bilioni 2.6. Hiyo inaonyesha kwamba Serikali inaongeza kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya Mheshimiwa Agnesta ni Fedha ya Maendeleo. Fedha ya Maendeleo inatumika kujenga Miradi ya Miundombinu na Tume hii kwa sasa hivi haihitaji Miradi ya Miundombinu. Fedha za Operations ya Tume inatokana na OC na katika mwaka huu wa fedha mpaka kufika Machi, Tume imeishapata bilioni 2.2 na imetumia fedha hizo kufanya kazi za kutosha sana. Kwa hiyo kuna utofauti hapa Mheshimiwa Agnesta kati ya fedha za maendeleo na fedha za operations, fedha za operations ziko kwenye OC na tayari Tume hii imeishapokea asilimia 69.79, takribani asilimia 70 na hatujamaliza mwaka. Hii asilimia 30 iliyobaki itakamilika mpaka kufika Juni. Kwa hiyo Tume imepata fedha hizi za operations, maendeleo ni miradi ambayo Tume hii haina miradi kwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye hoja alizozitoa Mheshimiwa Luhaga Mpina. Hoja ya kwanza ameshajibu AG, nisingependa kurejea lakini niseme tu pale ambapo mtu ameshinda kesi, amemshinda mtu yeyote yule achilia mbali Serikali, kuna utaratibu wa kisheria wa kukazia hukumu. Sasa hawa watu wana haki ya kufuata utaratibu huo wa kukazia hukumu, iwe dhidi ya Serikali iwe dhidi ya mtu mwingine yeyote sheria zetu zimeweka utaratibu mzuri. Tukiaanza kulitumia Bunge kukazia hukumu za Mahakama, tutakuwa tunaingilia Mhimili wa Mahakama, kwa hiyo tusimame kwenye misingi ambayo tumejiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Mpina, ameongelea suala la Tume ya Haki Jinai. Tume ya Haki Jinai hii ni maono na maelekezo na matakwa ya Mheshimiwa Rais, ili kuboresha mfumo wa haki jinai ambao tuliurithi toka wakati wa ukoloni. Kwenye hili tunapaswa kumpongeza sana sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuja na wazo hili na sisi tunaamini matokeo ya Tume ya Haki Jinai yatasaidia kuboresha mifumo ambayo tunayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mpina, ameongelea suala la Azimio la Kufuta Hasara ya Fedha kama ambavyo liko kwenye taarifa zangu. Alichokisema yeye ni ni kwamba hili jambo lililetwa lakini halijajadiliwa. Sasa hili ni jambo la Ushahidi, niombe kiti chako kitoe mwongozo kwa sababu tunahitaji sasa kwenda kwenye Hansard na kupitia kumbukumbu zote, tujue kama anachokisema ni kweli au siyo kweli na hatuwezi kukimaliza hapa bila kuomba Mwongozo wa Kiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Mpina ameongea suala la Ofisi ya Mwendesha Mashtaka kushindwa kukusanya shilingi bilioni 170. Najaribu kutafuta nitumie maneno gani kwa sababu tayari kiti kilishatoa mwongozo kwamba mambo yote yaliyokuwemo kwenye Taarifa ya CAG tutayajadili kwa mujibu wa utaratibu na Kanuni za Bunge tulizojiwekea. Sasa akinitaka mimi na Serikali tujibu leo, wakati utaratibu huo haujafika, tunakiuka hata miongozo ya Bunge ambayo tumejiwekea sisi wenyewe. Kwa hiyo tumwambie Mheshimiwa Mpina, tukifika wakati wa kujadili Taarifa za CAG jambo hili tutaliongea na Serikali itatoa maelezo yake wakati huo ukifika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mpina, vile vile ameongelea suala la upekuzi wa Mikataba na akasema kwamba kuna Mikataba kwa mujibu wake yeye anaona haijafanyiwa kazi na AG. Jambo hilo liko kwenye aya ya 53 ya Taarifa ya Bajeti ambayo tumeileta leo. Kwenye hili tunapaswa kumpongeza sana Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kwa sababu katika mwaka huu wa fedha amepekua mikataba mingi zaidi kwa asilimia 11 kuliko ilivyokuwa mwaka jana. Kwa hiyo amefanya ufanisi zaidi, mtu ambaye amefanya ufanisi tunapaswa kumpigia makofi mengi na kumpongeza na kwa taarifa tu ni kwamba mikataba yote iliyosainiwa ndani ya kipindi husika imepekuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa aya hii ya 53, hakuna Mkataba ambao haujapekuliwa. Ameongelea Mikataba ambayo imethaminishwa ambayo kwa mujibu wa taarifa hii ukurasa wa 28 ni mikataba 567. Mikataba yote iliyopekuliwa ni 1,304. Sasa siyo kila mkataba una thamani ya fedha, kuna mikataba mingine ni memorandum of understanding au ni makubaliano ambayo hayataji fedha mle ndani ambayo ina thamani ya fedha milioni 567. Kwa hiyo niseme kwamba hoja hizo ambazo amezisema Mheshimiwa Mpina ni hoja ambazo sisi tumezifanyia kazi isipokuwa hili moja tu ambalo tutaomba Kiti kitupe mwongozo kwa kadri kitakavyoona inafaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.