Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Katiba na Sheria, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Spika, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Katiba na Sheria, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha kuwa mhimili wa Mahakama ni chombo kikuu cha kusimamia utolewaji wa haki nchini. Chombo hiki ni muhimu sana katika ustawi wa jamii na maendelo endelevu, na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa Ushindani wa Kimataifa (National Competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha Ofisi ya Mahakama imefanikiwa kuboresha mifumo ya teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) ikiwemo mfumo wa usimamazi wa mashauri na kupelekea kuongeza tija katika utatuzi wa mashauri ikiwemo yaliyodumu kwa kipindi kirefu. Ofisi ya Mahakama imeendelea kutekeleza mpango wa ujenzi na ukarabati wa majengo ya mahakama katika ngazi mbalimbali nchini ikiwemo jengo la Makao Makuu Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa majukumu yake, Ofisi ya Mahakama inaendelea kukabiliwa na upungufu wa watumishi wa kada mbalimbali na pia uchakavu wa majengo ya Mahakama za ngazi zote. Kama ilivyoshauriwa kwenye taarifa ya Kamati ya Bajeti, kuna haja kwa Ofisi ya Mahakama kuongeza watumishi katika mahakama zote nchini ili kuongeza tija na ufanisi. Pia napendekeza Serikali kuhakikisha inatenga fedha za maendeleo za kutosha ili kuendeleza ujenzi na ukarabati Mahakama za Mwanzo, Mahakama za Wilaya, Mahakama kuu pamoja na nyumba za Majaji ili kuboresha na kusogeza huduma hii muhimu kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mbeya bado ina changamoto za uhaba wa Mahakama za Mwanzo na inapelekea wananchi kusafiri umbali mrefu kupata huduma ya Mahakama ya Mwanzo. Mji Mdogo wa Mbalizi wenye idadi ya watu zaidi ya 100,000, ina Mahakama ya Mwanzo ambayo ni ndogo sana na chakavu ambayo ni hatarishi kwa usalama na afya ya watumishi na hata wananchi kwa ujumla. Napendekeza Serikali ijenge Mahakama ya Mwanzo katika eneo la Utengule Usongwe ambalo limetolewa na wananchi. Pia naomba kuwepo na kipaumbele cha ujenzi wa Mahakama za Mwanzo angalau mbili kwa kila Tarafa za Usongwe, Isangati na Tembela.

Mheshimiwa, Mwenyekiti, naunga mkono hoja.