Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi ili nami niweze kuchangia hii hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana na kuwapongeza wananchi wangu wa Jimbo la Kisesa kwa namna ambavyo wanavyoendelea kuchapa kazi kule, nami nipo hapa Bungeni kuhakikisha kwamba nawawakilisha kikamilifu kwa mujibu wa Ibara ya 63(2) na (3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wananchi wa Jimbo la Kisesa kama tulivyokubaliana kwamba masaa ni namba, na hakuna kupumzika mpaka kazi ikamilike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza, suala la mambo ya kiujumla. Moja, Serikali imeshindwa kurudisha mifugo ya wafugaji 6,000 ambao wameshashinda kesi Mahakamani. Mheshimiwa Waziri suala hili ni la muda mrefu sana. Kwa sababu ni la muda mrefu, sasa Serikali itekeleze. Wapiga kura wangu mimi wa Jimbo la Kisesa ambao wanadai mifugo hii zaidi ya ng’ombe 400, sasa hivi wapo njiani kuja kuchukua mifugo yao. Akina Sai Maduhu, Masunga Muhamari, Ndaturu Muhororo, Zengo Kusekelwa, Dandika Kamasaga, Sambai Deke, hata akina Mzee Rerina kule kwa ndugu yangu hapa Mbunge, nao wote wako njiani kuja kuchukua mifugo yao. Sasa ni muhimu Serikali ikabidhi hao mifugo kwa hao wananchi ambao wameshinda kesi kihalali Mahakamani, warudishiwe mifugo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kwa haraka haraka…

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Rais ya Haki za Binadamu…

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Mpina.

TAARIFA

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa tu mzungumzaji, mimi pia Ushetu nina wananchi wangu walishinda kesi mwaka 2019, wako watatu, ng’ombe 500 na documents zote nimeshawapelekea. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina, unaipokea hiyo taarifa?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa yake na kwamba hawa wafugaji wote wa ng’ombe 6,000 wapo njiani kuja kuchukua mifugo yao hapa Dodoma kwa Waziri wa Katiba na Sheria. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Tume ya Rais ya Haki za Jinai, mimi ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa maono yake haya makubwa ya kuamua kuangalia kasoro na dosari zilizopo katika suala la ukamataji, upelelezi, uchunguzi na uendeshaji wa mashtaka na kuinda hii Tume. Pia naipongeza Tume sasa hivi inavyoendelea. Changamoto moja tu ni kwamba wanapopata maoni hadharani ya watu wanaowapa maoni: Moja, wanasababisha watu wengine ule uhuru wa kutoa mawazo unapungua, lakini pia inaweza ikafanyika kampeni ya upotoshaji ili mwisho wa siku wakatoka na results ambazo hazikutarajiwa, ambazo Mheshimiwa Rais hakuzitarajia wala wananchi hawakuzitarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, ni Maazimio ya Bunge kuhusu kufuta hasara na upotevu wa fedha na vifaa vya Serikali. Imesema, taarifa ya Mheshimiwa ya Waziri Kiambitisho B, ukurasa wa 146 anasema, Bunge liliazimia kuridhia kufuta hasara ya upotevu wa fedha na vifaa vya Serikali kwa kipindi kinachoishia tarehe 30 Juni, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwepo hapa, taarifa hii ililetwa hapa Bungeni kwa Order Paper tarehe 19 Septemba, 2022 lakini haikujadiliwa hapa Bungeni na madai yaliyokuwa ya Waziri wa Fedha yalikuwa ni shilingi bilioni 19.75 zisamehewe, zifutwe kwenye vitabu vya Serikali, lakini Bunge hili halikujadili taarifa hiyo. Bunge liliahirishwa siku hiyo saa 4.39, hatukujadili wala hatukuridhia. Sasa haya mambo ya kuridhia, Waziri wa Katiba na Sheria ameyatoa wapi? Nani amemletea taarifa za kuridhia? Kwa nini anataka kulidanganya Bunge? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipengele cha pili, eneo hilo hilo la Azimio la Bunge, ni kufutwa kwa madai ya malimbikizo ya kodi. Nilisema kipindi kile; nililalamika sana huko nyuma kuhusu kufutwa kwa madai ya Shilingi trilioni 5.59, na kama maelezo ya Waziri ya Fedha alivyokuwa akiyatoa hapa, lakini Taarifa za Mthibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Mwaka 2021/2022 zinasema kwamba haya mahesabu hayajaoneshwa kwenye vitabu hivyo, na hivyo inamaanisha kwamba yamefutwa. Kama yamefutwa, basi itakuwa amekiuka sheria Waziri wa Fedha anayehusika, na TRA watakuwa wamekiuka sheria kwa sababu hawana mamlaka hiyo kwa mujibu wa sheria, kifungu cha 34(1) ambacho kinataka lazima yapite hapa Bungeni na tuamue kwa njia ya azimio. Kwa hiyo, ukifuta tu kienyeji, maana yake unaingia kwenye makosa ya uhujumu uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni uendeshaji wa mashtaka. Hapa, DPP ameshindwa kukusanya Shilingi bilioni 170.61 ambazo tayari Mahakama imehukumu kwamba Washitakiwa wanatakiwa kutoa, hizi ni fedha za plea bargaining. Sasa ameshindwa kukusanya hizo fedha bila sababu zozote za msingi, na alikuwa na uwezo wa kukata rufaa upya, alikuwa na uwezo wa kutaifisha mali za washitakiwa wanaodaiwa, lakini mpaka sasa hivi DPP wetu ameshindwa kukusanya fedha hizo, na sababu za kutokukusanya hazieleweki. Namwelewa vizuri sana uwezo wake Sylvester Mwakitalu, huyu DPP wetu, ni Mwanasheria mzuri, nini kilichomkwazwa ashindwe kukusanya mapato halali ya Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hapa zinaletwa mbwembwe nyingi, mara unajua walionewa, mara unajua hawa... Kama ulinionewa, maamuzi haya hayakufanywa kwa DPP wakati huo. Maamuzi haya yalifanywa na Mahakama. Kama ulionewa, ulikata rufaa? Kwa nini hizi fedha hazijakusanywa? Suala la kutokukusanya fedha hizi limefanyika, Waziri wa Katiba na Sheria yupo, Waziri wa Fedha yupo, lakini naye DPP yupo. Kama DPP anashindwa kukusanya mpaka fedha ambazo zipo kwa mujibu wa sheria: Je, anapopokea mashtaka mengine kutoka kwa DCI, anapopokea mashauri mengine kutoka kwa TAKUKURU, anayafanyaje? Kama hawezi kukusanya, hata yale haya ambayo yako kwa mujibu wa sheria, Shilingi bilioni 170 Watanzania wanateseka fedha zao zipo tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni hili suala la usimamizi wa mikataba. Tumeelezwa kwenye hotuba ya Waziri kwamba Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameweza kufanya upekuzi mikataba 1,304 na katika mikataba hiyo, mikataba 567 ina thamani ya Shilingi trilioni 91. Maana yake kuna mikataba 737 nayo haijafanyiwa uthamini katika mwaka mmoja wa fedha. Sasa kama Serikali imeenda kuingia mikataba ya trilioni moja, Bajeti ya maendeleo tulinayoipitisha iko around Shilingi trilioni 15. Sasa hii mikataba ni ipi? Kwa nini haijawekwa kwenye majedwali? Ukienda kwenye viambatisho vyake kule, ameweka vitu vingine tu. Kilichoshindikana nini kuweka jedwali linaloonesha mikataba hii ya trilioni 91 ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, tusipofanya hivyo, Serikali inaweza ikaingia mikataba ambayo haimo kwenye bajeti, haipo kwenye mpango wa maendeleo na sisi kama wasimamizi wa rasilimali za Taifa tukawa hatujalitendea haki Taifa hili kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa nini Waziri ameshindwa kuweka kiambatisho hapa kama Wabunge tujue mikataba hiyo ni ya nini? Miradi hiyo ni ya jambo gani? Sasa hivi tumeona mikataba 737 haijafanyiwa uthaminishwaji; na kwa nini haijafanyiwa uthaminishwaji? Mingine imefanyiwa uthamanishwaji, kwa nini hii haijafanyiwa? Hii ambayo imefanyiwa uthamanishwaji ni 567 tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tutende haki. Waziri huyu, hakuna kupitisha bajeti yake, nanyi Wabunge nawaomba mpaka alete hili jedwali ili tujiridhishe na hicho ambacho kilichomo kwenye Hotuba yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la karibia mwisho, ni mashauri na madai ya usuluhishi; mashauri na madai ya usuluhishi hapa, jambo zuri hapa limetajwa kwamba tumeokoa hasa kwenye usuluhishi kwenye madai tumeokoa kama shilingi bilioni 165. Kwenye usuluhishi ni shilingi trilioni 13.33 na nasema; dakika moja tu namalizia.

MWENYEKITI: Malizia.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi trilioni 13.33 wanasheria wetu wameshinda kesi mahakamani na tukaokoa shilingi trilioni 13.33 ni jambo zuri. Mwezi wa 12 niliomba hapa jedwali lile liletwe tumeshinda kwenye mambo gani? Ni kesi zilihusu nini? Kwanini unatuletea tu idadi ya kesi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la mwisho kama tusipofanya hivyo, tutaendelea kuingia kwenye matatizo. Hapa Waziri amesema tu kesi tulizoshinda lakini tulizoshindwa ameshindwa kusema na ndiyo maana hapa tuna ile kesi….

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina muda wako umeisha.

MHE. LUHAGA J. MPINA:… ya Standard Chartered Bank ya Hong Kong shilingi bilioni 342 ambayo nayo tulishindwa. Sasa haya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)