Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uhai. Kwanza namshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Mambo anayoitendea Tanzania tangu ameingia madarakani ni makubwa, nasi wote ni mashaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya TAMISEMI, na kwenye hili nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Angellah Kairuki kwa kazi nzuri, na speed hii aliyoanza nayo naamini Halmashauri zetu sasa ziko salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia Naibu Waziri Mheshimiwa Festo Dugange na Mheshimiwa Deo Ndejembi kwa kweli wamekuwa wakizunguka kwenye halmashauri zetu wakikagua utekelezaji wa maono ya Mheshimiwa Rais namna fedha ambavyo amezipeleka. Hawa wanaendelea kufuatilia kwamba zinakwenda kufanya kazi sawa sawa na maelekezo ya Mheshimiwa Rais, tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo nimesema ni Mjumbe wa Kamati ya TAMISEMI. Kwenye ziara yetu tuliona miradi mingine ambayo imechelewa kukamilika na kati ya sababu wanasema ni mvutano wa wapi mradi utekelezwe. Wala haiingii akilini na kwenye jambo hili niiombe sana sana sana TAMISEMI hapa kubwa ni ushirikishwaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati miradi inakwenda wenzetu wataalamu kule site hawashirikishi wadau muhimu wanaohusika kwenye ile miradi wakiwemo Waheshimiwa Wabunge. Huku ndani tunafanya kazi ya kusemea Majimbo yetu sasa miradi ikiwa inakwenda ni vizuri tushirikishwe ili kwenda sawa sawa kutokwamisha hii miradi kwa sababu ya kuvutana ni wapi mradi ukajengwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe sana Wizara ielekeze wataalam wetu kule watushirikishe, washirikishe Waheshimiwa Wabunge, lakini pia na wadau wengine ili kwenda kutekeleza miradi hii kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mbunge wa Jimbo la Nachingwea na Makao Makuu ya Wilaya ya Nachingwea ni mamlaka ya Mji Mdogo zaidi ya miaka 10 sasa. Tumeshatuma maombi ya kuwa Mji kamili zaidi ya miaka saba iliyopita. Niiombe sana sana Wizara jambo hili ni jema na sisi litakwenda kutuongezea uwezo kama halmashauri. Niwaombe sana muone namna ambavyo mtaharakisha jambo hili jema ili Nachingwea sasa Mamlaka ya Mji Mdogo iwe Mji kamili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao upungufu kwenye Sekta ya Afya na kwenye Sekta ya Elimu. Kwenye eneo hili nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutoa sasa kibali kwa ajili ya kuajiri watumishi wapya kwenye eneo hili la elimu pamoja na afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwangu kwa mfano; tukiwa tunazungumzia habari ya kuboresha miundombinu kwa maana ya majengo, yako majengo chungu nzima ambayo bado wananchi walijitolea bado hayajakamilishwa. Tunashukuru kwa namna ambavyo Serikali imetuletea madarasa, imetuletea vituo vya afya ni jambo jema lakini ziko nguvu za wananchi ambazo zimelala na bado hazijulikani hatma yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana sana sana Wizara waende kumalizia yale maboma ambayo wananchi walijitolea na nguvu zao wanaziona. Tuna vituo vya afya, tuna shule lakini pia tunazo zahanati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kidogo kuzungumza kwa habari ya upungufu wa nyumba za waalimu. Mfano mdogo Nachingwea mahitaji nyumba ni 413; zilizoko ni 72. Sasa utaona hiyo walimu wa sekondari mahitaji ni 413, zilizopo ni hizo 72, upungufu ni 341. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa walimu wetu wanafanya kazi nzuri namimi nitumie nafasi hii kuwapongeza watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea kwa kazi kubwa wanayoifanya kwenye elimu, kwenye afya na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye elimu Nachingwea tunajivunia hata kwenye rekodi ya sasa tumekwenda sana na Lindi kiujumla kama Mkoa lakini kwa hali hii tuiombe sana Serikali ipeleke fedha kwa ajili ya kujenga nyumba za walimu ambazo kwa kweli upungufu ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matundu ya choo kwenye shule za sekondari. Mahitaji ni 564, yaliyoko ni 318; upungufu ni 246. Hebu angalia hiyo tofauti bado tuna kazi ya kufanya. Tunatambua na tunashukuru kwa kazi kubwa iliyofanyika lakini bado tunaomba zaidi kuendelea kutusaidia kwenye halmashauri hasa hasa hizi zilizoko vijijini kwa sababu zilisahaulika kwa muda mrefu. Sina mashaka na Mheshimiwa Waziri najua kazi hii utakwenda kuibeba vizuri na kazi hii itakwenda kufanyika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA. Wenzangu wamesema hapa kazi nzuri inayofanyika na TARURA hakuna asiyeiona. Waheshimiwa Wabunge wenzangu mtakubaliana kwamba TARURA wanafanya kazi nzuri chini ya Mtendaji Mkuu na Mkurugenzi wetu wa barabara Engineer Komba wanafanya kazi nzuri pamoja na watumishi wote wakiwemo wale wa Halmashauri yangu ya Wilaya ya Nachingwea. Wanafanya kazi nzuri. Basi tuiombe sana Wizara iendelee kuangalia namna ambavyo wataongeza fedha ili hawa watendaji wetu mahiri kabisa watuboreshee miundombinu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kabla Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kuingia; Nachingwea fedha ya matengenezo ya barabara tulikuwa tunapata shilingi bilioni moja. Baada ya kuingia Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imebadilika bajeti ya mwaka ni zaidi Shilingi bilioni tatu. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni jema na sisi kama Wabunge tunapaswa kuungana kwa kauli moja kuendelea kumtia moyo Mheshimiwa Rais, anatuheshimisha. Kazi inayofanyika kwenye Majimbo kwa kweli kila mmoja anajua na tunacho kitu cha kusema 2025 na kule Nachingwea wanasema wao 2025 na Mama Samia wala hawafichi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wao wanasema na Mama Samia. Wanajua haya yaliyobaki kama changamoto anakwenda kuyatatua kwa kipindi hiki ambacho kipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kidogo habari ya Shule ya Mchepuo wa Kiingereza, shule za msingi. Kuna utitiri huo wa halmashauri zetu kuanzisha hizo shule za mchepuo wa kiingereza, ni jambo jema lakini jambo hili linakwenda kuweka matabaka tena. Niiombe Wizara twende tukaboreshe shule zetu za msingi zillizoko kwenye vijiji vyetu. Tupeleke waalimu wa kutosha, tupeleke vitendea kazi vya muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja.