Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kuweza kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nitumie fursa hii kuwapa pole sana wananchi wa Jimbo la Kijini pamoja na wananchi wa Jimbo la Nungwi, hasa katika Vijiji vya Kidoti, Tazari na Kilimani kutokana na athari za upepo mkali ulioharibu nyumba na mali zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali yangu tukufu ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuona namna ya kuweza kuwafariji wananchi wale waliopata majanga yale ikizingatiwa kwamba upepo ule ni miongoni mwa athari za mabadiliko ya tabia nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, mchango wangu ninapenda kuuelekeza moja kwa moja katika suala zima la maadili, mila, sinka na taratibu za Kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, duniani muda huu tuliokuwa nao nchi zote zimeweza kugawika katika makundi mawili; zipo nchi zinaokubaliana na masuala ya ushoga, ndoa za jinsia moja, lakini zipo nchi pia ambazo zinapinga vitendo hivi. Hofu yangu ipo kwa Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutokana na hatua tunazochukua juu ya kukabiliana na suala hili. Kusema kweli bado hatujachukua hatua za kuridhisha na kuonesha u-serious wetu kama tunavyokuwa serious katika kupambana na majanga mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano; yakitokea maradhi ya kuambukiza nchi za jirani utakuta ghafla Serikali inaanza kuchukua jitihada za kufunga mipaka kuzuia wageni kuingia katika nchi hizi ambazo wageni wanatoka katika nchi ambazo zinasadikika kuwa na maradhi hayo. Lakini hali iko tofauti katika suala hili la ushoga. Changamoto tunazozikuta kutokana na suala hili, sisi tuliopitiwa na majimbo ambayo yamezungukwa na utalii ni kubwa mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani, na ni muumini wa kila siku; Tanzania tumekuwa na sheria nyingi zinazoweza kutosheleza kukabiliana na hali hii ya ushoga. Lakini changamoto inakuja katika suala zima la usimamiaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili ninapenda nitoe mfano, Jimbo langu la Nungwi ni jimbo la kitalii na ilivyojengeka au ilivyoaminika ni kwamba sehemu kubwa zinazoendesha biashara hizi za ushoga, za ndoa za kiume, ni sehemu ambazo zimepitiwa na sekta ya utalii. Kinachonihuzunisha, unaweza kuwakuta maaskari wanatoka nje ya Nungwi, wanatoka sehemu tofauti na Zanzibar kukiwa kuna sherehe au hali yoyote katika mazingira ya Nungwi unaweza ukakuta maaskari wapo wengi wanakuja kwa ajili ya kutunza mazingira ya pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini cha kusikitisha ni kwamba badala ya kwenda kufanya doria katika matukio waliopangiwa wale maaskari unaweza kuwakuta maaskari wamekwenda kuzongea na kuwanyang’anya waendesha bodaboda bodaboda zao na kuzipeleka kituo cha polisi kwa ajili ya mazungumzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachonisikitisha maana ya hiki ninachokizungumza kinatuweka na masuala mawili mazito. Inawezekana kwa Tanzania yetu ya kileo suala la waendesha bodaboda kukosa helmet likaonekana kwamba lina athari kubwa zaidi kuliko suala la ushoga.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi.

T A A R I F A

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, nilikusudia nieleze kuhusiana na hatua ambazo Serikali kwa ujumla wake imechukua kuhusiana na changamoto hii ambayo Waheshimiwa Wabunge wameizungumza kwenye hotuba ya bajeti yangu kwa kirefu, lakini naona huu ni mchango takribani wa pili umekuwa ukiishutumu Serikali juu ya hii kadhia ambayo inaendelea duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ambayo nataka kutoa ni kwamba kwanza, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali kupitia kauli mbalimbali za viongozi wetu kuanzia Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu, mara kadhaa wamelizungumzia na wameonesha hisia zao na hasira juu ya matatizo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna hatua ambazo tunachukua kama Serikali, zinaratibiwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu, atakuja kueleza mwenyewe. Lakini kwa upande wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ikiwa kama Wizara ambayo inasimamia usalama wa nchi hii na utekelezaji wa sheria hizo, kuna mambo mengi ambayo tumeyafanya ya kimkakati. Hofu yangu ni kwamba Waheshimiwa Wabunge wasidhani kwamba Serikali haichukui hatua kwenye jambo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo mengi; kuna masuala ambayo yanahusu usimamizi wa sheria kwa upande wa Jeshi la Polisi, kuna watu wengi ambao wanahusika katika mambo kama haya wameshachukuliwa hatua mbalimbali, na wengine wapo katika uchunguzi. Kuna hatua za kiuhamiaji kwa wale ambao wanajihusisha na masuala haya wanaotoka nje ya nchi kupitia taasisi mbalimbali, hatua hizo za kiuhamiaji vilevile zimeshachukuliwa za kiuhamiaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hatua za kitaasisi kupitia taasisi mbalimbali ama jumuiya zinazojishughulisha na mambo haya, tunashirikiana vizuri na Mheshimiwa Waziri, Dkt. Gwajima, ambaye anasimamia NGOs na mimi nasimamia jumuiya za kiraia, kushughulika na taasisi na jumuiya hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hatua ziko nyingi sana. Niombe Waheshimiwa Wabunge pale ambapo nitakuja kusoma hotuba ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi tutaeleza kwa kina.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, waelewe tu kwamba Serikali iko very serious na tatizo hili na hatua nyingi zinachukuliwa na pongezi kwa jitihada zao ambazo wanaendelea.

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kuchangia hoja yangu; naipokea taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuendelea, maaskari wamekuwa waki-deal zaidi na waendesha bodaboda, kitu ambacho kinawapa hofu Watanzania juu ya ukubwa wa waendesha bodaboda kukosa helmet na suala la ushoga. Kitu kinachotia hofu zaidi ni kwamba hivi kuna ugomvi gani baina ya vijana wetu wa bodaboda na maaskari polisi? Lakini hivi kuna uswahiba gani uliopo kati ya baadhi ya maaskari na wale wanaojihusisha na vitendo vya ushoga? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa ni maisha, tuwasome kisha tuwasomeshe kwa vizazi vyetu. Mwanadamu amekuwa akinywa pombe zaidi kuliko maji safi na salama kwa afya yake. Mwanadamu amekuwa akiwatupa na kuwatelekeza viumbe ambao amevizaa yeye mwenyewe wakati kuku na bata wanaendelea na utaratibu wao uleule wa kuwalea na kuwa na mapenzi kwa watoto wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanadamu wamekuwa na tabia ya kutaka kuzaa na wale waliowazaa au watakaowazaa lakini simba wanaendelea na utaratibu wa kuwafukuza watoto wao wanapofikia umri wa balehe na kuwataka waende wakajitegemee ili kuepusha tu kuzaa na wazazi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi sote hapa ni wazazi, sote ni walezi na sote tuna familia. Mzazi na mlezi wa kweli ni yule anayeguswa na changamoto za mtoto wa mwenzake. Katika hili wanyama tangu walipoumbwa hawajawahi kubadilisha tabia zao lakini binadamu tumebadilika na kuwa na tabia za kinyama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mashekhe, mapadre, wanaendelea kupaza sauti kukemea ushoga na vitendo hivi vinavyoambatana na mambo hayo, Serikali iko bize zaidi katika kukusanya mapato na tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukijifanya hatuyaoni haya, tunayafumbia macho, badala yake tukiacha kudumisha mila na kuendekeza nguvu zaidi katika kukusanya mapato kwa wahisani na wawekezaji ambao baadhi yao hawana tija.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya miaka michache tutakuwa na chanzo kipya cha kukusanya mapato kupitia mashoga.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, taarifa hiyo iwe fupi tafadhali.

T A A R I F A

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba tumekuwa tukipigana vita kubwa sana katika kuhakikisha tunatunza maadili ya nchi hii na vizazi vyetu; tumekuwa tukiongea sana. Jambo ambalo nimeliona ni kwamba ufuatiliaji wa nini Serikali inafanya kwa Watanzania wengi na wawakilishi wao siyo mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeimba mpaka nyimbo za don’t touch here, here and there kama vile tunachekesha, ni kupeleka hamasa hiyo, tumetengeneza SMAUJATA, Jeshi la

Jamii la Wazalendo, wako kule wanafanya maandamano… Kilimanjaro jana…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, yote hiyo ni kuamsha, na Ofisi ya Rais, TAMISEMI imepeleka barua kwamba agenda hii iwe ya kudumu kwenye mabaraza yetu ya halmashauri ya Madiwani na Kata.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachangia.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Simai, endelea na mchango wako.

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningelipenda niendelee na hoja yangu nakusisitiza kwamba kama tutaendelea kuwa busy zaidi katika masuala ya kukusanya mapato kuliko ku-deal na mila na desturi za Kitanzania basi tujiandae Watanzania kuwa na chanzo kipya cha kukusanya mapato kupitia mashoga kwa sababu kasi ya ushoga inaongezeka kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile maana ya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)