Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo ipo Mezani pako ambayo ni hoja ya Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nami nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya kwa Watanzania ambayo ni kazi tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya, lakini kwa kutuletea hotuba ambayo ina matumaini kwa Watanzania. Amegusa kila sekta. Pia tunamwona Waziri Mkuu jinsi anavyohangaika kuisimamia Serikali, tunamwona anavyosimamia miradi mbalimbali ya Serikali, na anavyofanya ziara kufuatilia maagizo ya viongozi wengine. Kwa hiyo, tunampongeza sana Waziri Mkuu kwa kazi tukufu anayoifanya. Tunamwombea kwa Mwenyezi Mungu ampe afya njema, aendelee kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza pia Mheshimiwa Jenista Mhagama na Mheshimiwa Profesa Ndalichako kwa kazi nzuri anayoifanya, pamoja na Naibu Waziri. Kipekee nawapongeza kwa jinsi walivyoratibu shughuli za Mwenge katika Mkoa wetu wa Mtwara. Wametoa usaidizi wa kutosha na shughuli zilifana. Nachukua nafasi hii kumpongeza Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mheshimiwa Kanali Abbas kwa jinsi alivyosimamia zoezi hili, na uzinduzi ulifanyika kwa kufana sana. Nampongeza yeye pamoja na Kamati mbalimbali ambazo zimehusika katika shughuli ile ya Mbio za Mwenge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utaanza kujikita kwenye Hotuba ya Waziri Mkuu, Ukurasa wa 30 ambao unazungumzia kwamba, Serikali itaendelea kuratibu upatikanaji wa pembejeo, viuatilifu na mbegu. Kipekee naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kazi kubwa ambayo inaifanya katika kuwekeza katika tasnia ya korosho. Tumeona kwa muda wa miaka mitatu mfululizo Serikali ikitoa pembejeo bure kwa wakulima wa korosho. Tunaendelea kuishukuru Serikali na mwaka huu kuna mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 340 ambayo imetolewa. Nina matumaini pembejeo hizi zitafika kwa wakati na wakulima wa korosho watanufaika na pembejeo hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ushauri ufuatao: Pamoja na uwekezaji huu ambao umefanywa kwenye tasnia ya korosho, bado kuna anguko la uzalishaji wa korosho katika nchi yetu. Msimu wa mwaka 2017/2018 Tanzania tulifikisha tani 320,000, lakini kwa masikitiko makubwa msimu huu uliopita uzalishaji umepungua hadi tani 160,000 pamoja na uwekezaji mkubwa uliofanywa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiuliza Bodi ya Korosho, hawana majibu ya uhakika, ukiuliza TARI Naliendele, hawana majibu ya kutosheleza. Napendekeza iundwe tume huru ya kufuatilia nini kimeikumba tasnia ya korosho mpaka kukawa na anguko kubwa kiasi hiki? Kwa sababu haiwezekani mikoa ya uzalishaji wa zao la korosho imeongezeka, Serikali inawekeza vya kutosha, lakini tumetoka kwenye tani 340,000 hadi tani 120,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi ndogo tu, Ivory Coast, kila mwaka wanaongeza zaidi ya tani 100,000 na mwaka huu wamefikisha tani 1,000,000. Malengo ya Bodi ya Korosho mwaka huu ilikuwa ni kufikisha tani 400,000, lakini tumeishia kupata tani 160,000. Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi inasema tutakapofika msimu wa 2025 tufikishe tani 700,000. Kwa anguko hili tuna kazi kubwa sana ya kufanya ili kufikia malengo ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba uunde tume huru ili kuchunguza nini kimejiri? Ninapendekeza tupate wataalamu kutoka nje; kuna wataalam kutoka SUA; tusiendelee kuwatumia wale wale wa TARI na wa Bodi ya Korosho kwa sababu watatuletea majibu yale yale ambayo tumeyazoea. Tupate timu mpya, ikiwezekana twende hata nchi nyingine tuchukue wajumbe, kwa mfano, Ivory Coast ambao wamezalisha vizuri. Msumbiji wanafanya vizuri, tuchukue uzoefu kutoka huko, kwa sababu, tukileta TARI au watu wa Bodi ya Korosho watatupa majibu yaleyale ambayo kila mwaka bado uzalishaji unapungua.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza hadidu za rejea ya tume hiyo vile vile iangalie mfumo wetu wa uagizaji na udhibiti wa pembejeo. Kuna malalamiko kwamba pembejeo ambazo zinaingia kwenye tasnia ya korosho hazina ubora unaotakiwa. Kwa hiyo, Tume hii tutaipa na kazi hiyo, waangalie; je, hizi pembejeo ambazo zinaingia kwenye tasnia ya korosho zina ubora unaotakiwa? Zinatoa matokeo ambayo tunayatarajia? Kwa sababu haiwezekani tukaambiwa kuna mabadiliko ya tabia ya nchi wakati Mtwara na Msumbiji tunapakana na Mto Ruvuma; Msumbiji wanafanya vizuri, lakini Mtwara haifanyi vizuri. Kuna kitu ambacho hakiko vizuri katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili utajikita katika kuifungua Mtwara. Naipongeza Serikali kwa kazi kubwa sana ambayo imeifanya katika kuufungua Mkoa wetu wa Mtwara. Kuna uwekezaji mkubwa kwenye Bandari yetu ya Mtwara, kuna uwekezaji mkubwa katika kiwanja cha ndege na maboresho katika barabara, lakini kuna kazi ambayo ninatakiwa ifanyike ili Mtwara yetu iweze kufunguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya Mnivata – Newala – Tandahimba mpaka Mbamba Bay, kipande cha kilometa 160. Tumekuwa tukibadilisha tarehe ya kuanza utekelezaji. Tulikutana na Katibu Mkuu akatuambia Machi tutaanza utekelezaji, lakini jana tumesikia jibu hapa kwamba ni mpaka Juni. Changamoto ni nini? Hii barabara ianze kujengwa. Barabara hii ni kiunganishi kizuri na kitakamilisha Mtwara Corridor ambayo itafungua mikoa ya Mtwara, Ruvuma, Njombe mpaka Mbamba Bay. Kwa hiyo, naomba huo mchakato wa ununuzi uendeshwe haraka, ili barabara hii iweze kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya Masasi – Nachingwea, ni ya muda mrefu, kwa nini haitengewi fedha za kutosha ikajengwa? Vilevile kuna suala ambalo ukichukua vitabu vya bajeti miaka mitano, tutakuwa tunazungumzia reli kutoka Mtwara hadi Mbamba Bay na Tawi la Mchuchuma na Liganga. Kila mwaka tunataja, lakini utekelezaji haupo. Naomba Serikali yangu sikivu tuanze kuutekelea huu mradi. Mradi huu kama nilivyosema, utaifungua mikoa ya Mtwara, Lindi, Ruvuma, Njombe na hivyo tutafungua ushoroba wa kusini.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Chikota kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kuchauka.

T A A R I F A

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwongezee taarifa Mheshimiwa anayeongea. Ametaja Mtwara Corridor; kwa ufahamu wangu, naona Mtwara Corridor imeshakufa. Kwa sababu, Mtwara Corridor ilitegemewa kuifungua, kama route aliyoisema; lakini kwa miaka saba niliyokaa Bunge hili sijawahi kuona mradi wa barabara Mtwara wala barabara Lindi, zaidi ya barabara iliyotajwa Mnivata, kila mwaka inatajwa, na hii barabara ya Nachingwea – Masasi. Hakuna barabara yoyote Mkoa wa Lindi iliyotekelezwa kwa muda wa miaka saba yote niliyokaa hapa. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Chikota, taarifa unaipokea?

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea. Niongezee kwamba, ile barabara inaitwa barabara ya Masasi – Nachingwea mpaka Liwale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna mradi wa maji kutoka Mto Ruvuma kupeleka maji Mtwara Manispaa. Mradi huu ni mkubwa na mradi huu una mwaka wa saba sasa. Kwenye kitabu cha Wizara kunabadilika maneno tu, tunatafuta fedha, tunafanya usanifu, tunafanya mazungumzo. Mradi huu ni muhimu sana kwa Manispaa ya Mtwara. Mradi huu siyo kwa Manispaa ya Mtwara tu, utanufaisha Wilaya ya Mtwara, lakini vilevile na Halmashauri ya Mji wa Nanyamba kwa sababu, chanzo cha maji kipo Maembechini; lakini wananchi wamesitisha kufanya shughuli zao za maendeleo kwa kupisha mradi huu. Fidia haijalipwa bado, lakini vilevile hakuna kinachoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba mradi huu ambao ni muhimu kwa upatikanaji wa maji kwa uwekezaji wa Mji wa Mtwara, kwa sababu, hata Kiwanda cha Dangote kina mahitaji makubwa sana ya maji. Mradi huu ukitekelezwa, basi hata na Kiwanda cha Dangote kitapata maji ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mradi huu utekelezwe na ninaunga mkono hoja. Ahsante sana.