Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo ipo mbele yetu. Nitumie nafasi hii pia kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kuweza kusimama nikiwa na afya tele kuchangia hoja ambayo ipo mbele yetu katika uwakilishi wangu kwa wananchi wangu waliopo katika Jimbo la Morogoro Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kukupongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yako nzuri ambayo umeitoa hapa Bungeni ikionesha yale ambayo yalifanyika katika kipindi kilichopita lakini mwelekeo wa Wizara yako katika kuyafanyia yale yanayotakiwa kufanywa na Serikali katika mwaka huu wa fedha unaokuja. Nitumie nafasi hii vilevile kumpongeza Mama yetu Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi kubwa ambayo anaifanya katika kuwaletea maendeleo Watanzania. Wabunge wa Bunge hili la Jamhuri ya Muungano ni mashahidi, mambo ambayo yanafanyika katika Majimbo yetu ni historia ambayo kwa kweli kila Mbunge anashangaa maana ndani ya miaka miwili kuna mambo makubwa ambayo yamefanyika. Tuna kila sababu ya kumpongeza, kumpa moyo lakini kuwa sambamba na yeye katika kufanya yale ambayo anayahitaji yafanyike kwa maendeleo ya Taifa hili la Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuchangia kwenye suala la barabara. Ninaipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo ameifanya katika ujenzi wa barabara ya Bigwa - Kisaki. Barabara ya Bigwa - Kisaki ni barabara muhimu ambayo inakwenda kwenye Hifadhi ya Mwalimu Nyerere pia inakwenda kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere. Toka tumepata uhuru ilikuwa ni historia lakini kwa mwaka huuu wa fedha Serikali yetu imetenga fedha kujenga kwa kiwango cha lami kilometa 78, tender hiyo ilitangazwa tarehe 20 Januari na juzi tarehe 5 Aprili tenda imefunguliwa wako Wakandarasi ambao wanachujwa ili kazi ianze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kila sababu ya kuipongeza Serikali lakini kubwa zaidi niiombe Serikali hasa Wizara ya Ujenzi na TANROADS waharakaishe mchakato wa kupata Mkandarasi ili kazi ianze mara moja na Watanzania ambao wako kule Morogoro Kusini, Morogoro Kusini Mashariki na Wilaya ya Morogoro na wao waone matunda ya uhuru kwa kuweza kupita kwenye barabara ya lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba vilevile niishauri Serikali yangu na kuiomba Serikali tufanye upembuzi yakinifu wa barabara ya Ngerengere kwenda Mvua na Mvua kwenda Kisaki ili nayo ijengwe kwa kiwango cha lami, kwa sababu barabara zote hizi ni muhimu, ni barabara ambazo zinakwenda kwenye Hifadhi ya Mwalimu Nyerere na Bwawa la Mwalimu Nyerere, tukiweza kukamilisha kufika huko kwa kiwango cha lami tuna uhakika watalii watakwenda, tutaongeza pesa nyingi za kigeni kwenye Serikali ambazo zitasaidia kuleta maendeleo Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la barabara niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi kikubwa ambayo wameifanya katika kuleta fedha za maendeleo katika upasuaji wa barabara kwenye eneo la TARURA. Katika mwaka wa fedha uliokwisha tumepata takribani bilioni 4.13 katika utengenezaji wa barabara kazi inaendelea. Ombi langu kwa Serikali kiuhalisia jiografia ya Jimbo la Morogoro Kusini ni Jimbo ambalo liko milimani fedha hii ambayo imekwenda imetosheleza kwa kiasi lakini bado kuna uhitaji mkubwa, ninaiomba Serikali yangu ikiwezekana katika bajeti inayokuja hii kupitia TAMISEMI, TARURA waongezewe bajeti, ikiwezekana ifike hata bilioni saba tuweze kwenda kupasua barabara za milimani kama vile Singisa, Kasanga, Kolero, Bwakila Juu, Kibogwa ili barabara zifikike maendeleo yapatikane kwa urahisi. Vilevile ninaomba Serikali kuna bajeti tumeomba ombi maalum la billioni moja kwa ajili ya barabara ya Bwakila Juu - Dakawa niombe Serikali itusaidie fedha hizo ili walau tuweze kufanikisha katika hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwenye suala la elimu tumefanya kazi kubwa sana. Kwa mara ya kwanza nadhani Wabunge mtakuwa ni mashahidi miaka yote kila tunapofika mwishoni mwa mwaka huwa tunakuwa na operation maalum kwa ajili ya kuwachangisha wazazi ili watoto waende shule form one inapofunguliwa, ndani ya miaka miwili hii chini ya Mama Samia Suluhu Hassan hakuna mzazi ambae amebughudhiwa. Madarasa yalipelekwa na watoto wote walianza kwa mara ya kwanza wote hakukuwa na walioingia awamu ya kwanza, hakukutokea na walioingia awamu ya pili wote waliingia kwa awamu moja, tuna kila sababu ya kumpongeza Mama katika haya na tupo nyuma yake tunamuunga mkono katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Serikali ni kwamba pamoja na mafanikio haya bado kuna changamoto, bado maboma mengi ya nguvu za wananchi ambayo yamejengwa yanahitaji kumaliziwa. Vilevile bado kuna uhitaji wa vyumba vya madarasa, ninaiomba Serikali yangu ihakikishe kwamba mambo haya yanafanyika ili watoto wetu waweze kusoma kwa nafasi na kuweza kupata elimu iliyo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika maeneo ya pembezoni kama vile kwangu Jimboni Kata ya Kolero, Kata ya Kasanga, Kata ya Kibogwa, Kata ya Singisa na Bwakila Juu, kuna uhitaji mkubwa wa mabweni kutoka katikati ya Kata kwenye shule ya sekondari mpaka kwenda kwenye vijiji kuna mwenda ambao unatumika pengine zaidi ya masaa matatu, manne watoto wetu wanashindwa kwenda na kurudi, matokeo yake nini? Wanakwenda kujipangisha kwenye vijumba ambavyo hakuna ulinzi wa watoto. Kama hivi tunavyopiga kelele maadili na nini, kwa hiyo ninaiomba Serikali ihakikishe kwamba inatutengea mabweni walau mawili mawili kwenye kila shule za sekondari katika bajeti ili watoto wetu wapate utulivu wa kusoma na kukaa katika usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala afya Serikali imefanya kazi kubwa. Ninaipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, kwenye Wilaya yangu hospitali ya Wilaya tumekamilisha, tuna kila sababu ya kupongeza katika hili. Pia Vituo vya Afya Sita vimekamiliaka, maboma Kumi yamemalizwa ya zahanati ambayo ilikuwa nguvu za wananchi zilikuwa zimetumika kulikuwa kuna uhitaji wa Serikali kuongeza, tuna kila sababu ya kupongeza Serikali katika hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna changamoto ambayo ninaiomba Serikali yangu ya vifaatiba vya upasuaji,majengo ya OPD kwa Kituo cha Afya cha Kisemu, Kisaki, na Mikese, vilevile Watumishi bado ni wachache, kuna hela ambazo tuliahidiwa Halmashauri ya Morogoro Vijijini milioni 500 kwa ajili ya vifaatiba kwenye Hospitali ya Wilaya, milioni 300 kwa ajili ya vifaatiba kwenye vituo hivyo nilivyovitaja vya afya na shilingi milioni 150 kwa ajili ya zahanati. Ninaiomba Serikali tuleteeni fedha hizo tukamilishe haya yanayotakiwa kupata ili Watanzania dhamira ya Serikali ya kuwapatia afya inayostahili ikamilike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kwenye suala la utawala…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa muda wako umekwisha.

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)