Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Awali ya yote kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenijalia mpaka sasa kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyelwa. Kabla sijaanza kuchangia kwenye hotuba ya Waziri Mkuu nataka nisome neno la Mungu katika Zaburi 33:12; “Heri Taifa ambalo Bwana Mungu wao watu waliochaguliwa kuwa urithi wake.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme neno hili Taifa la Tanzania ni Taifa Maalum. Inawezekana watu wasijue lakini Taifa hili Mungu ameliweka kwa ajili ya kusudi maalum. Ni lazima kama Watanzania tutambue kusudi hili ambalo Mungu ameliweka katika Taifa hili na tulilinde kwa nguvu zote na gharama zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Mataifa machache ambayo Mungu ameyachagua na ameyaweka kwa ajili ya kusudi maalum. Kwa hiyo ndugu zangu haya mambo ya haki za binadamu ya kuliondoa kusudi la Mungu katika Taifa letu niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, niwaombe sana Watanzania tupambane nalo kwa nguvu zote. Haiwezekani tukaileta laana katika Taifa hili ambalo Mungu ameliweka kusudi lake. Niombe sana viongozi wetu wa kitaifa hili jambo walichukulie serious na ikiwezekana pawepo na kipindi maalum cha kutubu ili kuondoa dhambi hii katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuongea hayo sasa nichangie hotuba ya Waziri Mkuu. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Watanzania wanajua kazi kubwa anayoifanya ya kumsaidia Mheshimiwa Rais na aendelee hivyo hivyo, tunamtia moyo na naamini na Mungu atakuwa pamoja naye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuwaletea Watanzania fedha nyingi. Kila mahali Mheshimiwa Rais anakokwenda ameleta fedha na kwa kweli hakuna mahali ambapo hajagusa. Kwa hiyo, tunaendelea kumwombea Mheshimiwa Rais aendelee kuwatumikia Watanzania na naamini Watanzania wako pamoja naye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Vitambulisho vya NIDA. Ni haki ya Watanzania kupata vitambulisho vya NIDA kwa sababu ni muhimu, lakini jambo ambalo ni la kusikitisha, ni zaidi ya miaka 10 tangu waanze kutengeneza vitambulisho vya Taifa. Hata hivyo, katika maeneo mengi bado hatujaweza kuwafikia Watanzania wengi ili waweze kupata vitambulisho vya NIDA. Naamini vitambulisho hivi vya NIDA ni haki ya kila Mtanzania. Mtanzania ambaye hana kitambulisho hawezi kusajili simu yake, Mtanzania huyu hawezi hata kusajili biashara yoyote. Kwa hiyo, tunadumaza maendeleo ya Taifa. Hivyo, niiombe sana Serikali haya mambo ya kila siku wanakuja hapa na ngonjera za kutuambia sijui inaletwa mitambo gani, tuombe sasa waje na majibu yaliyo sahihi, Watanzania wapate vitambulisho ili tuondoe usumbufu uliopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile utaratibu wa kupata vitambulisho bado haujakaa vizuri. Kwa maeneo haya ambayo yapo pembezoni kama Mkoa wa Kagera na maeneo mengine, Watanzania wanapata shida sana. Haiwezekani umeenda kumtambua Mtanzania, wewe Afisa uhamiaji uliyetoka Dar es Salaam bila kushirikisha Viongozi wa Vijiji na Vitongoji, wewe unaanza kutambua unasema huyu ni mhamiaji haramu kwa sababu ana pua ndefu, kwa sababu ni mrefu. Niombe sana tushirikishe jamii inayozunguka maeneo hayo ili tuweze kuwatambua wale ambao hawastahili ili Watanzania wanaostahili waweze kupewa Vitambulisho vya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niongelee suala la umeme. Umeme ni maendeleo, umeme ni ajira, lakini pia umeme ni uchumi. Mheshimiwa Rais anapambana sana kuleta pesa kwa ajili ya kuwapa Watanzania umeme, lakini kasi ya kupeleka umeme ni ndogo. Mfano, upande wa Kyerwa, tuna vijiji 28 ambavyo bado havijapatiwa umeme, lakini vijiji hivi tayari Mkandarasi amekwishapewa. Niombe sana Serikali ifuatilie huyu Mkandarasi anayepeleka umeme Mkoa wa Kagera, kwa kweli speed yake ni ndogo. Haiwezekani ndani ya miaka miwili kwenye Wilaya ya Kyelwa ameshindwa hata vijiji vitatu, sasa hivi ni vijiji viwili tu. Kasi yake ni ndogo kwa kweli hairidhishi. Pesa ipo Serikali imetoa, lakini hawa wakandarasi wanaowapa wakati mwingine wawaangalie waone ni wakandarasi wa namna gani. Watanzania wanahitaji umeme kwa sababu ni muhimu sana. Kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu hili aliangalie kama Msimamizi Mkuu wa Shughuli za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niongelee kilimo. Serikali imeweka fedha nyingi kwenye kilimo na tunampongeza Mheshimiwa Waziri Bashe anafanya kazi nzuri. Tulishuhudia hapa wanagawa pikipiki za Maafisa Ugani, lakini niombe sana Mheshimiwa Waziri Bashe hili aliangalie Maafisa Ugani wake wanamwangusha. Hakuna kazi wanayoifanya. Hawa Maafisa Ugani kitu wanachokifanya kwa mfano Kyerwa, wanasubiri msimu wa kahawa, mkulima anaanza kuvuna kahawa ndipo wanakuja kukagua kama ile kahawa imekomaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzoni wakati anaanza kulima, anapalilia, anahudumia hili zao hatumwoni Afisa Ugani lakini ukifika wakati wa kuvuna wanakuja kwa kasi. Wakati mwingine wanakuja kutafuta fedha kwa wakulima, kuwaibia. Kwa hiyo, niombe sana, ni lazima tuweke nguvu kubwa ili mkulima aweze kupata zao ambalo ni zuri na lenye tija. Kwa hiyo, niombe hili Mheshimiwa Bashe aliangalie Maafisa Ugani wake kwa kweli wanamwangusha hawafanyi kazi, wamekaa tu na hizo pikipiki walizowapa sijui wanazifanyia nini? Kwa hiyo niombe sana hili waliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nilisemee ni suala la barabara. Barabara ni muhimu sana. Hizi barabara za Wilaya ya Kyerwa zimezungumziwa muda mrefu. Barabara ya Omurushaka kwenda mpaka Murongo, tenda imetangazwa mwaka 2022, Mkandarasi amekwishapatikana, lakini mpaka leo zaidi ya miezi sita hatujaona Mkandarasi. Tunaomba Mkandarasi aje asaini Mkataba, barabara hii ianze kujengwa kwani ni muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile barabara ya Mugakorongo kwenda mpaka Murongo, hii ni barabra muhimu, ni barabara inayounganisha Nchi ya Uganda na Tanzania. Ni lazima tufanye biashara na hawa wenzetu. Ukienda kwa wenzetu unaangalia ni kama Ulaya, lakini ukija huku kwetu ni kama uchochoro. Niombe sana kwa sababu barabara hii imeshatangazwa, tenda imeshafunguliwa, Mkandarasi apatikane na barabara hii ianze ili Wanakyerwa na wao waweze kujiona kama ni sehemu ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru. (Makofi)