Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi jioni ya leo kuwa mmoja wa wachangiaji. Ni kweli muda wa kupongeza unakula muda wa kuchangia lakini ni hakika kabisa katika Bunge hili kwa namna ambavyo Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano anatekeleza majukumu yake tunazo kila sababu ya kutumia dakika chache za kuchangia tunazopewa kumshukuru yeye na Serikali yake kwa mambo mbalimbali makubwa anayoyafanya kwenye nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kuchangia hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu, nami nitachangia eneo moja dogo sana la kukuza uchumi kwenye nchi hii. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ametuonyesha namna ya hali ya ukuaji wa uchumi duniani na katika nchi yetu, amejaribu kutaasa na kutuambia kwamba inakadiriwa itakapofika 2023 uchumi wa dunia utashuka kwa asilimia 2.9 kutoka asilimia 3.4 ya mwaka 2022. Ameweza kutueleza pia kama nchi mwaka 2022 uchumi ulikuwa asilimia 5.2 na unakusudiwa kuongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, ongezeko hili la kiuchumi ambalo linaonesha katika taarifa ya nchi yetu na ukiangalia ongezeko la kidunia linaloonesha kwamba uchumi unakadiriwa kushuka isitupe faraja kwa sababu katika nchi yetu zipo changamoto mbalimbali ambazo zinaashiria kwamba tunakoelekea hali ya kiuchumi pia inaweza ikawa mbaya sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya jambo ambalo nina wasiwasi nalo, leo hii katika Majimbo mbalimbali nchini idadi ya tegemezi nchini inakuwa kubwa sana na utegemezi huu unasababishwa na mambo mbalimbali, moja hali ya hewa katika maeneo mengi ambayo kilimo kilikuwa kinachukua nafasi hali ya hewa imebadilika wakulima wengi hawalimi, kwa hiyo inatokea sasa wananchi wengi wanaelekeza nguvu zao kuwategemea ndugu zao wachache wenye kipato kidogo.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa kukataa maelekezo ya Kiti ni utovu wa nidhamu, Kanuni ya 84 na inaweza ikampotezesha mtu mambo magumu sana, endelea Mheshimiwa Michael.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, nilikuwa nasema kwamba pamoja na takwimu ambazo tumezipata za kuongezeka kwa hali ya uchumi nchini lakini hali halisi kwenye Majimbo na kwenye nchi yetu tegemezi wanaongezeka kwa kiasi kikubwa sana, utegemezi huu unasababishwa nimesema na mabadiliko ya hali hewa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mikoa mingi ambayo wakulima walikuwa wanatumia kilimo kama moja ya chanzo cha kujipatia mapato na kukuza uchumi wao, hali ya hewa imepelekea kubadilisha hali hiyo na watekelezaji na mavuno yanakuwa machache kitendo ambacho kinapelekea sasa watu wengi kuwategemea ndungu zao wachache wanaoingiza vipato kwa njia nyingine ambazo zinaweza zikapatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni moja ya athari zinazopelekea kuona kwamba hata wizi kwenye taasisi mbalimbali unaongezeka, watumishi wengi wa umma kwenye taasisi mbalimbali wanawategemezi wengi nyuma yao na yote yanasababishwa kwamba hao wanaowategemea wengi hawana shughuli za kufanya, kama alikuwa mkulima ameshindwa kulima kutokana na hali ya hewa, ameshindwa kulima kutkana ana mogogoro ya wakulima na wafugaji, ameshindwa kulima kutokana na sheria nyingi za matumizi ya mabonde kutokutumia maji ya umwagiliaji, ameshindwa kulima kwa sababu ya kukosekana miundombinu ya kilimo kwenye maeneo mbalimbali nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninashauri Serikali ijielekeze kuangalia ni namna gani italiondoa hili wimbi kubwa la watu kuwa tegemezi na njia pekee ya kuliondoa wimbi kubwa la watu kuwa tegemezi ni kufungua miundombinu ya kuwafanya watu hawa waweze kuwa wazalishaji na wanaweza kuwa wazalishaji kwenye sekta ya kilimo na kwenye taasisi mbalimbali ambazo wanaweza wakapata ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, sote hapa ni mashahidi nchi yetu leo inaongoza kwa ujenzi wa viwanda, Mkoa wa Pwani ambao natokea ni moja ya Mikoa ambayo ina viwanda vingi vya kutosha. Tujiulize viwanda hivi ambavyo vimejengwa katika maeneo mbalimbali nchini vinalipa kiwango gani cha mishahara kwa Watanzania. Sasa kama wananchi ambao wanapata nafasi wachache kuajiriwa kwenye viwanda hivi ambavyo vimejengwa mshahara wao hauendani kabisa na hali ya uchumi mtaani, nini kitatokea? Ni lazima wapo watakaoshindwa kumudu kufanyakazi, matokeo yake wataachakazi na wataendelea kuwa tegemezi kwa ndugu zao wachache wenye kipato kwa njia moja au nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tunaona tuna maeneo mengi na mabonde mengi ambayo yanastahili kwa kilimo. Tujiulize mabonde haya yamewekezwa kwa kiwango gani na Serikali ili wananchi wengi wanaoyazunguka mabonde hayo watumie hayo mabonde na maji yaliyoko kwenye maeneo hayo kufanya uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishauri sana Serikali ijielekeze kwenye kuwaongezea wananchi uchumi ili hii takwimu ambayo wana wasiwasi nayo ya kuongezeka au kushuka kwa uchumi na Pato la Taifa kushuka isiwe katika mazingira ambayo tunayazungumza.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo bado tunaona kwamba mfumko wa bei wa bidhaa mbalimbali nchini unapelekea wananchi kushindwa kumudu kugharamia maisha yao ya kawaida. Watumishi wa kawaida ndiyo pale tunaposababisha sasa pesa za Serikali zinakwenda kwenye maeneo hayo kusimamia miradi, matokeo yake wanatokea watu wanaiba! Wanaiba kwa sababu hali ya mtaani ya bei haifanani na kipato chake cha mwezi anachofanya yeye na wale tegemezi alionao. Ni vema Serikali ikajielekeza kwenye namna bora ambayo inaweza ikawaondolea watu wake hali ngumu ya kiuchumi ili waweze kuhakikisha kwamba mambo mbalimbali yanakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumefanya ziara Wajumbe wako wiki moja, wiki tatu zilizopita wengi walikuwa kwenye Kamati zao, tumetembea kwenye maeneo mbalimbali kukagua miradi mbalimbali. Kwa kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu ndio inasimamia utekelezaji wa majukumu ya Serikali katika nchi hii tuifahamishe tu kwamba hali ya miradi mingi nchini ni tete. Usimamizi wa miradi katika maeneo ambayo watu wengine tumeyakagua haiko vizuri, haiko vizuri kwa sababu pesa za miradi zilizopelekwa hazikufanya kazi za tija na ndiyo hii ambayo leo watu wanashindwa kujizuia hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii kila mtu anaesimama anajaribu kupata nafasi ya kuijadili hotuba ya CAG na hii inafanana na mtu mwenye kikohozi, kikihozi huwezi kukizuia kinakuja kutokana na hali uliyonayo kwa wakati husika. Wabunge wanapata hamu ya kuichangia hiyo ripoti wakati wakifahamu muda bado kutokana na hali ya taarifa ilivyo na inasababishwa na hali ambayo inaonekana, wameiona kwa macho kwenye ziara, wameiona kwenye taarifa za CAG, kwamba usimamizi wa miradi kule hauko vizuri, miradi imepigwa, unakuta mradi una-phase mbili mpaka ya tatu lakini phase ya kwanza haijaisha, yote hii inasababishwa na usimamizi mbovu, inasababishwa na wizi ambao umefanywa na wasimamizi ambao wapo kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, inasemekana ni vibaya kuwaaambia wizi leo kwa sababu wakati bado lakini lazima tuseme kwamba hali ni mbaya lakini katika sehemu mbalimbali inaonekana hali mbaya hii inasababishwa na huu utaratibu wetu wa force account. Tuiangalie hii force account.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona kama ni njia mojawapo nzuri ya kupunguza gharama za miradi lakini kiukweli hali halisi gharama za miradi hazipungui kwa sababu kila sehemu ambako pesa zimepelekwa bado Wakurugenzi, Wasimamizi wa miradi hiyo wanaomba pesa za ziada.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mbunge ahsante.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.