Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi uliyonipa na nianze kabisa mwanzo niwaombe kabisa Waheshimiwa Wabunge na Mheshimiwa Naibu Spika kwamba Bunge hili tusikubali kutumika kama mahali pa kuhalalisha wahalifu na wabadhirifu wa fedha za umma, na kwamba la kuvunda halina ubani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuwashukuru sana na kuwapongeza sana mamlaka za ukaguzi pamoja na za uchunguzi, CAG, CPA Charles Kichere pamoja na CP Salum Hamdun, Mkurugenzi wa TAKUKURU, kwa kazi nzuri sana waliyoifanya ya ukaguzi wa fedha za umma mwaka huu. Taarifa zao walizozitoa pamoja na watendaji wao kule ofisini ni kielekezo kikubwa sana cha uzalendo wa Taifa lao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana kipekee Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kukataa katakata nchi yake kugeuzwa kuwa shamba la bibi. Na mimi nasema Mawaziri waliohusika, watendaji wote wa Serikali waliohusika mapema iwezekanavyo wakamatwe, washtakiwe na wafunguliwe makosa ya uhujumu uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii tunajadili hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, kuna mambo mawili tu ya kiujumla ninayotaka kuyasema; moja bajeti ya maendeleo tuliyopanga mwaka huu wa fedha, katika mpango wetu wa miaka mitano tulipanga iwe asilimia 37.1 lakini mpango wa maendeleo uliowasilishwa na Serikali, fedha za maendeleo ni asilimia 34.1 tu; nini kilichosababisha mpango wetu kushuka, nini kilichosababisha fedha za maendeleo kushuka tofauti na mpango wa maendeleo tuliouweka wa miaka mitano?

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni suala zima la Katiba; nimesoma mpango wa maendeleo na ukomo wa bajeti sijaliona suala hili; nimesoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu sijaliona suala hili, na suala hili Mheshimiwa Rais amelisisitiza sana, sikutegemea nilikose kwenye hotuba kubwa ya Mheshimiwa Waziri Mkuu au kwenye taarifa kubwa ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ikija Serikali hapa itueleze hili suala likoje, licha ya Mheshimiwa Rais wetu kulisema kwa msisitizo mkubwa kwamba ni lazima tufanye mabadiliko katika Katiba yetu na ikiwezekana tupate Katiba mpya inayohitajika kwa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tatu ni suala la vihatarishi au changamoto mahususi katika utekelezaji wa bajeti tunayoizungumza leo. Ukipitisha bajeti kukiwa na vihatarishi vingi ambavyo vinaashiria kwamba mpango wa bajeti tunaoupitisha unakwenda kukwamba tu, ni lazima ujishirikishe, ufanye tathmini ya kutosha juu ya tahadhari hizo, juu ya changamoto hizo, ufanye tathmini ya kina, uone ni namna gani unakwenda kuzitatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa Serikali kupitia mpango wa maendeleo ukurasa wa 89 kipengele cha 2.4.2 inakiri wazi kwamba kuna vihatarishi vingi vinavyopinga utekelezaji wa bajeti. Kwa kifupi tu kwamba kuna upungufu mkubwa wa rasilimali watu, kuchelewa kukamilisha taratibu za utoaji cheti cha msamaha wa kodi, usanifu duni, usimamizi usioridhisha katika utekelezaji wa miradi kwa mujibu wa mikataba na mipango kazi kwa baadhi ya watekelezaji wa miradi, kucheleshwa kwa malipo ya wakandarasi na sababu nyingine nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi sababu inasema Serikali yenyewe kwamba hizi ni changamoto. Moja, maana yake Waziri Mkuu atuambie kwamba Serikali imeshindwa kuzidhibiti hizi sababu? Lakini la pili; tunashindwaje kutoka pale? Na ukienda sasa kuzichambua hizi hoja ndizo hizi ambazo zinaturudisha nyuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutakaa hapa, tutaidhinisha bajeti ambayo mwisho wa siku inakwenda kutafunwa na watu wachache. Tunarudi hapa tena unatupa tena jukumu la kupitia bajeti inakwenda kuliwa na watu wachache. Ni lazima hizi nyufa tuzizibe leo. Tunapopitisha bajeti na nyufa zenyewe tumeziziba ili fedha za wananchi zisiende kuliwa tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, kushindwa kutekeleza mpango wa manunuzi ni jambo ambalo kwenye mpango wa maendeleo wamesema wao wenyewe Serikali na hapa imetokea, na CAG amelisema. Jumla ya trilioni 3.14 hazikutumika, zikiwemo fedha tulizozituma kwenda TANROADS.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania mwaka 2021/2022 waliahidiwa kujengewa barabara zao zaidi ya trilioni 2.9 za TANROADS hazikwenda kufanya kazi, hakuna mradi ulikuwa implemented. Leo tena tunarudi hapa kupitisha bajeti halafu pesa zikawekwe, Watanzania waendelee kuteseka bila kupata maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kutokufuata Sheria ya Manunuzi. Tunajua tunapitisha bajeti hapa, mwisho wa siku hizi pesa zinakwenda kutekeleza miradi ya maendeleo kupitia Sheria ya Manunuzi, halafu sheria hiyo inakiukwa kila leo, halafu tunaletewa tena bajeti inakiukwa na fedha za wananchi ziliwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilisimama hapa kwenye Bunge lako tukufu nikazungumzia juu la Lot No. 6, mradi wa SGR kutoka Tabora kwenda Kigoma kwamba TRC imeacha bei ya ushindani kwa kilometa moja ya standard gauge ya bilioni 9.1 imekwenda kumpa mkandarasi CCECC kwa bilioni 12.5, zaidi ya bilioni 3.4 kwa kilometa na kuisababisha Serikali hasara ya trilioni 1.7. Mkataba huu bado unaendelea, tusipofanya intervention utaendelea. Nchi imekula hasara ya bilioni 1.7.

Mheshimiwa Naibu Spika, Lot 3 na Lot 4 mkaguzi ame- confirm kwamba tumepunjwa trilioni 1.7; lakini pia na ununuzi wa mabehewa bilioni 503; jumla trilioni nne.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi fedha ni za Watanzania, Waziri wa Fedha alikwenda kukopa hizi fedha kwa sharti la kuvunja Sheria ya Manunuzi ambayo hana uwezo huo, hana uwezo huo mkubwa wa kisheria, hana uwezo mkubwa huo wa Kikatiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi Waziri wa Fedha, Waziri wa Uchukuzi na Mkurugenzi wa TRC kwa nini hawajakamatwa na kufunguliwa makosa ya uhujumu uchumi mpaka sasa hivi wako hapa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, tusicheke, shilingi trilioni nne za Watanzania zinakwenda kupotea kwenye mradi huu. Hata kama tungeenda kukopa mkopo sijui wa riba ngapi, tunalipa fedha kidogo sana katika mambo mengine haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hizo dakika tatu zilizobaki, nizungumzie mambo mawili ya mwisho; kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere hapa na kwenyewe tulisema sana hapa Bungeni ikiwemo mimi, kwamba jamani hawa watu tunawadai fedha zetu, kwa nini hawalipi? Majibu ambayo yanatolewa na Waziri wa Nishati hayaeleweki, kila leo tukiuliza hapa Bungeni. Mkaguzi amekwenda ku-confirm tunawadai bilioni 327 kwa mwaka mmoja wa 2022. Mwaka 2023 tunadai zingine, kwa hiyo ni jumla ya bilioni 655. Ukijumlisha na zile za CSR ni bilioni 270; jumla ni bilioni 926 tunazowadai. Na mkataba unakaribia kwenda mwisho, lakini fedha hizi hazidaiwi na hawa watu, Waziri wa Nishati yupo, Mkurugenzi wa TANESCO yupo, hawadai fedha hizi na bado wapo kwenye ofisi za Serikali. Mamlaka zinazotakiwa kuchukua hatua ziko wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho; leo tulikuwa tunalalamika hapa sisi tunawezaje kupitisha Bajeti, halafu mtu mwingine anakwenda kutumia matumizi nje ya bajeti, mtu mwingine anakwenda kukopa mikopo zaidi ya fedha tulizoidhinisha hapa. Kwa hiyo, fedha alizokopa hatujaidhinisha, matumizi ya hizo fedha zinakwenda kutumika kwenye nini, hatujaidhinisha. Leo mkaguzi amekwenda ku- confirm, mwaka wa 2021/2022 Waziri wa Fedha amekwenda kukopa trilioni 1.285 bila ridhaa ya Bunge, bila ridhaa ya mtu yeyote, fedha za Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatujui hizo trilioni 1.285 zimekwenda kufanya nini, hatujui alizikopa akazipeleka wapi, mpaka sasa hivi na jambo hili linaendelea kutunzwa kwa usiri mkubwa. Mambo haya inawezekanaje yakafanyika hivyo yanavyofanyika?

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tunawadai IPTL bilioni 342, fedha hizi tulishashinda kesi kihalali toka tarehe 1 Machi, 2021; kazi ni TANESCO na Waziri wa Nishati kwenda kuzidai, imeshindikana. Wanashindwa nini kwenda kudai; wana ubia gani na huyu IPTL, wananufaika nini na huyu IPTL fedha za Watanzania? Na kama jambo hilo limewashibda si wawaachie Watanzania wengine wazalendo ambao wanaweza kuzipigania fedha za Watanzania. Watanzania wanyonge hawa ambao wanateseka kwa kodi zinazowaumiza kila leo, fedha zao wanazoweza kuzichukua, ambazo zipo kwa mujibu wa sheria hazidaiwi na watu ambao walishapewa dhamana ya kuziomba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa summary tu hapa, ubadhirifu wote huu wa CAG ambao mimi nimeainisha na bado naendelea kuainisha ni zaidi ya trilioni 30. Sasa ukishakuwa na ubadhirifu wa trilioni 30 unakaa kwenye bajeti kufanya nini? Yaani unazipitisha hela zote zikagawanywe? Na hapa lazima tuchukue hatua kali dhidi ya watu hawa wanaofanya haya mambo. Kama Bunge lako litashindwa kuchukua hatua katika hili, basi hili Bunge liwajibike… [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)