Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana nami kupata nafasi leo ya kuchangia katika hotuba hii ya Waziri Mkuu. Nina machache tu ya kusema. Siku ya leo nitazungumzia mambo mawili, na muda ukiruhusu nitakwenda kwenye la tatu. Nitazungumzia suala la uzalendo kwa vijana, suala la maadili kwenye nchi yetu na muda ukiruhusu nitazungumzia utaratibu wa ujazaji wa nafasi za ajira zinazotangazwa Serikalini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala zima la uzalendo kwa vijana; kwanza kabisa, naomba kwa niaba ya vijana wote Watanzania, tufikishe salamu zetu za pongezi na shukrani za kutosha kabisa kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Kwa sababu tangu ameingia madarakani Mheshimiwa Rais amekuwa nasi bega kwa bega, changamoto zetu amezivaa, amekuwa anazi-address kila siku na kuwasisitizia watendaji wake pia kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano. Tumekuwa na malalamiko ya muda mrefu sana sisi vijana kwamba tukianza biashara tunakuwa na msururu wa taratibu nyingi na urasimu mkubwa sana kabla ya kuja kusimama kwenye biashara zetu. Mheshimiwa Rais ameliona hili, na siku za hivi karibuni kupitia Waziri Viwanda na Biashara, ameondoa malipo ya kodi kwa kipindi cha mwaka mmoja kwa kijana aneyeanza biashara. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi hizi za Mheshimiwa Rais, tangu alipoingia katika kiti chake, kahakikisha anatulea sisi vijana na kutuaminisha kwamba tunaye mtu anayetuunga mkono katika juhudi zetu za kuchangia katika kujenga Taifa letu. Hata hivyo, bado tuna changamoto moja kubwa sana ambayo inatishia moyo wa uzalendo kwa vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha pale ambapo vijana tunakuwa tunajifunga mikanda, shime kujenga nchi yetu pamoja na mazingira na changamoto zote tunazokutana nazo, halafu tunaona kuna baadhi ya watendaji ambao sisi vijana tumewaamini kupitia nafasi mbalimbali Serikalini, kufanya kazi yao kutuletea maendeleo kwa kodi tunazolipa, wanaiba pesa hizo na badala yake tunashindwa kupata maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata neno la Mungu limesema kwamba “toa boriti katika jicho lako, ndipo utoe boriti katika jicho la mwingine.” Tunapataje nguvu au Serikali itapata wapi legality ya kumwambia kijana uwe mzalendo, ukipewa nafasi fanya kazi na ujenge nchi yako ilhali kuna baadhi wamepewa nafasi hizo na wanayoyafanya tunayaona.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii vijana wanaohitimu tunawalaumu, kwamba kijana anahitimu, anataka ndani ya mwaka mmoja ama miwili aendeshe Range, ajenge ghorofa. Tunawalaumu, lakini haya hatujayatoa from no where, tunawaona. Kuna vijana wadogo, leo hii unamwona kapata kazi TRA, kapata kazi bandarini, mwaka mmoja ana ghorofa. Unaniambiaje mimi nisifanye yale kama anayoyafanya yule? Tunaua Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana sio Taifa la kesho tu, ni Taifa la leo. Kama tunataka vijana waendelee kuwa wazalendo, waendelee kuijenga nchi hii, tujenge nchi ambayo miaka 100, miaka 200 itasimama ikiwa na uchumi imara, tunahitaji mabadiliko makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishauri katika Bunge lililopita kwamba Serikali ituletee mabadiliko ya sheria ili tukuze uwajibikaji katika utumishi wa umma. Hawa wanaofanya mambo haya, tuwawajibishe. Leo hii kijana akiona kwamba mwizi au anayefanya ubadhilifu amewajibishwa, hata yeye kesho anazidi kuona kwamba Taifa linamlinda, Taifa linam- support. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wahenga walisema, “mtoto wa mhunzi asiposana, hufukuta.” Maana yake ni nini? Maji hufuata mkondo. Sasa kama Serikali inatuonesha mkondo huu, kesho vijana watafuata mkondo upi? Tunaomba, tunaomba, tunaomba; haya yanayoendelea kule nje hayana afya kwa vijana, hayana afya kwa Taifa, hayana afya kwa kesho yetu iliyo salama. Tunahitaji mabadiliko ya sheria na tunahitaji hatua za haraka zichukuliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala zima la maadili, wamezungumza Wabunge wenzangu hapa waliotangulia. Kuna kitu ambacho kinaendelea kwenye jamii yetu kinatushtua. Kimsingi kinatishia hata kesho ya nchi yetu na kinahusu bara zima kwa ujumla. Mapenzi ya jinsia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunajua kwamba kujihusisha na mambo haya, moja ya effect yake kubwa zaidi ni kukosekana kwa uendelevu wa vizazi. Hakuna kizazi kinachoweza kuendelea kwa mapenzi kati ya mwanaume na mwanaume au mwanamke na mwanamke. Mimi nitawarudisha nyuma kwenye historia. Karne ya 19, moja ya vitu vilivyoisaidia Europe ku-develop kwa kasi ilikuwa ni kitu kinachoitwa demographic revolution. Ongezeko kubwa la idadi ya watu, lakini ripoti za IMF na World Bank zinatuonesha nchi ya China imefika hapa ilipofika sababu kuu, ikiwa ni wingi wa watu walionao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii mambo haya yanaletwa, siyo kwamba wenzetu hawaoni juhudi za ukombozi ambao Bara la Afrika linajitahidi kufanya ili kufika mbele na kujiondoa katika lindi la umasikini tulionao, ni wazi. Pia ripoti ya World Bank inaonesha, Africa is the youngest continent. Maana yake ni nini? Afrika ndiyo bara pekee lenye nguvu kazi kubwa zaidi kuliko mabara mengine yote duniani. Afrika ndiyo ina vijana wadogo zaidi kuliko mabara mengine huko duniani. Maana yake miaka 10, 20, 30 ijayo Afrika leo haitakuwa hapa ilipo. Tuna vijana wenye nguvu na wenye uweledi wa kufanya kazi. Uchumi wetu utakuwa umeimarika, umeimarika, umeimarika zaidi. Kimsingi hicho ni tishio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi wamechangia kwa maana ya kwamba hii ni tishio tu kwa maadili yetu, lakini mimi naenda mbele nasema, hili ni tishio dhidi ya ukombozi wa kiuchumi ambao Afrika na Tanzania inajaribu kufanya. Ni ukweli usiopingika kwamba sisi Watanzania zaidi ya asilimia 80 tunategemea kufanya kazi za ngumu ili kujipatia kipato, lakini tafiti zinaonesha kwamba kibiolojia, watu wanaojihusisha na mambo hayo, hasa wanaume wanapungukiwa na nguvu ya kufanya kazi kwa zaidi ya asilimia 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipoziba ufa, tutajenga ukuta. Miaka 20 ijayo tutapata wapi vijana wa kufanya kazi za nguvu za nchi hii, kuijenga nchi hii? Tunahitaji hatua za haraka zichukuliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nashangaa kwa sababu Mheshimiwa Rais amezungumza, Mheshimiwa Makamu wa Rais amezungumza, Mheshimiwa Waziri Mkuu amezungumza, Wabunge mbalimbali wamezungumza, viongozi wetu wa dini wamezungumza, Watanzania kila sehemu wanazungumza, kwa nini hatua hazichukuliwi? Sheria ipo wazi, hiki kitu ni criminal offence. Mheshimiwa Saashisha alisoma hapa sheria ndani ya Bunge hili, kwamba ni miaka 30 ukionekana umefanya mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii siyo kesi ya nani atamfunga paka kengele? Kwa nini? Kwa sababu watu hawa wanajinasibu, na wako wazi hata kwenye mitandao ya kijamii. Kwa nini hatuoni hatua zikichukuliwa? Tunahitaji kuona hatua za haraka zinachukuliwa kunusuru vizazi vyetu, kunusuru nchi yetu lakini kunusuru uchumi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, lakini siyo kwa umuhimu mdogo, nitaongelea suala la utaratibu wa ujazaji wa nafasi za ajira kwenye nchi yetu. Tunashukuru sana tangu Mheshimiwa Rais ameingia madarakani, ametangaza nafasi nyingi sana za ajira na vijana wengi wamejipatia ajira. Kwenye hilo tunashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo tuna walakini kidogo katika utaratibu unaotumiaka kujaza nafasi hizi. Kwanza kabisa, tukiangalia ratio ya applicants kwa nafasi zile ambazo zinazozatangazwa, inaonesha namna gani tuna tatizo kubwa sana la ajira kwenye nchi yetu. Tunaipongeza Wizara kwa sababu tulitoa maoni nayo ikapokea, ikaanzisha vituo mbalimbali ambapo watu sasa wanaweza kwenda kufanya interview tofauti na zamani ambapo lazima waje sehemu moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto inayokuja ni kwamba, unakuta zinahitajika nafasi 100, lakini idadi ya watu wanaoitwa kwenye interview unakuta ratio yake ni hata 50:1. Unajiuliza, kama hawa watu kwenye ku-apply walitoa vyeti vyao, wali-submit vielelezo vyote vilivyotakiwa. Kwa nini waitwe watu wengi kiasi hiki kwa nafasi chache ilhali tunajua fika kwamba hawa vijana wana changamoto huko waliko? Wengi hata akiitwa hata kwenye kufanya interview wanakwambia hata nauli sina, sijui nitafikia wapi? Sijui nitakula nini kwa hizi siku ninazoenda kufanya interview?

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta nafasi moja wanaigombania vijana 50. Kuna haja ya kufanya hayo? Pili, vijana hawa wakifika kwenye interview, kumekuwa na tendency; unaambiwa interview inaanza saa 3.00, lakini vijana watakaa pale mpaka saa 8.00 hamna interview iliyofanyika. Hawajui wala hawajapewa utaratibu wowote. Kwa nini kama Serikali inakuwa imejiaandaa kufanya interview na kusaili vijana hawa, kwa nini wasijipange, utaratibu ufanyike, vijana wafanye interview warudi majumbani? Inakuwa ni kama hawajajipanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine, tumeambiwa kwamba mnafanya interview, kuna baadhi yenu wanawekwa kwenye kanzidata ili nafasi nyingine zikija, wasifanye tena usaili wachukuliwe kwenye kanzidata. Hilo ni jambo zuri, lakini lazima tuwe na transparency. Vijana watajiuliza kwamba tuna uhakika gani kwamba hawa waliowekwa sasa hivi ndiyo wale waliokuwa kwenye kanzidata? Tuna uhakika gani kwamba hawa hawajachukuliwa kutoka mifukoni mwa watu wakawekwa kwenye nafasi zile? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali. Naomba, kama kuna kanzidata, iwe wazi, kila mtu ajue kwamba mimi kwenye kanzidata ni Na. 3, zikitangazwa nafasi 10 maana yake na mimi nimo; zikitangazwa nafasi 20 nami nimo, au simo nasubiri kipindi kijacho, ili kuondoa sintofahamau kwa vijana kwenye suala hili la ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)