Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa na mimi ya kuchangia kwenye hii Hotuba ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti,nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na timu yake kwa hotuba yake nzuri ambayo imeonesha ni kiasi gani kulikuwa na mafanikio makubwa ya utendaji wa Serikali hasa ukizingatia hiki kipindi tunachopitia. Tanzania si Kisiwa; sisi wenyewe tumeshuhudia kiasi gani ambavyo mtikisiko wa dunia umeathirika kutokana na UVIKO-19 pamoja na vita vya Urusi na Ukraine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mataifa makubwa yametikisika kikubwa. Wenzetu huko ukiangalia mfumuko wa bei ni zaidi ya tarakimu mbili na kuna wengine wanakaribia tarakimu tatu. Sasa, ukiangalia hotuba ya Waziri Mkuu inaonesha sisi tuko chini ya asilimia tano ambayo ni asilimia 4.7 kwa mwaka huu. Vilevile tunategemea hata hali itakuwa nzuri kwenye bajeti ijayo. Sasa utaona ni maajabu kiasi gani kwa nchi kama Tanzania tunafanya vizuri ukilinganisha na mataifa makubwa. Leo hii kuna benki kubwa za dunia ambazo tulikuwa tunaziamini, nazo zimetikisika. Kwa hiyo hili si jambo dogo, ni jambo la kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa aliyoifanya katika kuhakikisha kuwa Tanzania tunakuwa katika hali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia hata ukuaji katika repoti ya Waziri Mkuu inaonesha kuwa ukuaji wa uchumi kwa Tanzania bado ni mzuri ukilinganisha na wenzetu. Ukiangalia ukusanyaji wa mapato bado ni mzuri ukilinganisha na wenzetu. Kwa nini tunajilinganisha na wenzetu? Ni kwa vile mpango wetu ni wa ushindani kiuchumi, ambao unahitaji kuonesha kiasi gani Tanzania tufanye vizuri ukilinganisha na mataifa mengine. Nchi jirani hapa tumeona mtikisiko wa uchumi, ukuaji wa uchumi umekuwa hasi. Vilevile leo hii hata ukusanyaji wa mapato wenzetu majirani wameshindwa kukusanya kiasi ambacho umepelekea hata kushindwa kulipa mishahara ya wafanyakazi wao. Sisi tunajivunia kwa Mheshimiwa Rais wetu pamoja na timu yake nzima ambavyo wameendelea kufanya vizuri na hali inakuwa na matumaini mazuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti,namshukuru Mheshimiwa Rais vile vile kwa jimbo langu na Wilaya yangu ya Mbeya, ametutendea mengi mno. Kwenye maji kwa kweli hata nikiuliza swali hapa litakuwa ni swali la kupongeza kwa sababu miradi mingi ya maji imeenda vizuri na inaendelea kutekelezwa. Hivi juzi Serikali imesaini mkataba wa mradi mkubwa wa maji ambao ni kwa Wilaya nzima ya Mbeya, likiwemo jimbo langu, pamoja na Mkoa wa Songwe, Mradi wa Kiwila.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye barabara vilevile kilikuwa ni kilio kikubwa. Mheshimiwa Rais naye ameidhinisha ujenzi wa barabara ya njia nne kuanzia Nsalaga ambayo iko jimbo la Mbeya Mjini mpaka Songwe ambayo iko Jimbo la Mbeya Vijijini. Hii ni hatua kubwa kwa sababu pamoja na changamoto zote, lakini Watanzania wengi wamepoteza maisha kwa ajili ya ufinyu na barabara ilivyokuwa mbovu, hii barabara yetu ya TANZAM.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kumalizia ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Songwe, kwa kweli Mbeya ni ya kimkakati. Uwanja wa Ndege wa Songwe ambao ni mahsusi utakuwa wa kimataifa kwa ajili ya kusomba mizigo kupeleka nchi za kigeni. Mheshimiwa Rais amefanya jambo hili katika wakati mwafaka ambao tunategemea kuwa sasa Tanzania, badala ya mazao yetu kuoneshwa yanatoka nchi jirani, sasa hivi kwakweli tutakuwa hatuna sababu tena kuona maparachichi au kahawa zinatoka nchi jirani badala ya kwamba zinatokea Tanzania.

Mheshimiwa Spika, katika hili naomba Serikali, iangalie ni namna gani sasa ule uwanja uzungukwe na eneo maalumu la viwanda (industrial park) au EPZ, kama alivyozungumza mwenzangu. Pale tunahitaji tuwe na cold rooms za kutosha. Ule uwanja si kwa ajili ya Mbeya peke yake, ni kwa ajili ya Nyanda za Juu Kusini. Wenzetu wanalalamika kuhusu maparachichi yanaharibika; lakini huwezi kupeleka maparachichi, lazima yaandaliwe. Pia tunazalisha mazao mengi, matunda mengi na mboga mboga. Sasa tujiandae wakati huu ambao tumenunua ndege ya mizigo iweze kufanya kazi ya kusafirisha mizigo ambayo itakwenda kiushindani kwenye masoko ya nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Rais vilevile kwa miradi ya umeme. Tumeenda vizuri na sasa hivi tunamalizia vijiji 40 vya mwisho ambapo nategemea kabla ya mwaka huu vijiji vyote vitakuwa vimeguswa ili tuendelee na utekelezaji kwenye vitongoji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote hayo ili tuweze kustahimili na kukaa katika utulivu kwenye nchi yetu tunahitaji haya mambo yaweze kuendelea kama ilivyo sasa na yaboreshwe. Naomba Serikali iendelee kujenga barabara. Barabara ya TANZAM ni muhimu sana. Kipande cha kuanzia Igawa mpaka Tunduma kiko kwenye hali mbaya sana. Naomba Serikali ichukue hatua za haraka kwa sababu hii barabara inatuweka katika ushindani na Bandari yetu ya Dar Es Salaam ili iweze kushindana na bandari za nje. Kwa hiyo hili suala siyo la barabara ni suala la kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hiyo barabara napendekeza vilevile barabara ya Mbalizi-Shigamba, Mheshimiwa Waziri Mkuu uliahidi wewe mwenyewe hii barabara na ukasema hutaki tena usikie nauliza swali wala niongelee kuhusu hii barabara. Nakuomba mwaka huu kwenye bajeti hii, hii barabara iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Pia Barabara ya Isyonje-Ikondo nayo ni barabara muhimu kwa ajili ya kulisha uwanja wa Songwe. Vilevile barabara ya Mbalizi-Gadula naomba nayo ikamilishwe haraka kwenye bajeti ya mwaka huu. Pia by pass ambayo inaanzia Uyole mpaka Songwe nayo ni muhimu ikakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yote haya tunahitaji Serikali iboreshe reli ya TAZARA. Reli ya TAZARA ni muhimu; na mimi naweza kusema uboreshaji wake ni quick wins, haiitaji mambo makubwa. Nina imani Serikali ikitenga angalau bilioni 300 ile reli inaweza kuboreshwa. Kwa sababu ukiboresha reli ya TAZARA unakuwa umeweka mizigo asilimia zaidi ya 70 ambayo inapita Bandari ya Dar es Salaam kwa ajili ya soko la nje itapitia kwenye Reli ya TAZARA na bandari yetu itakuwa competitive.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bandari yetu sasa hivi iko kwenye ushindani mkubwa na inawezekana tukashindwa kushindana kwa vile kuna Lobito ambazo ziko Angola. Wale wenzetu wametengeneza mpaka barabara za kuja kwenye masoko yetu. Vilevile kuna bandari za Afrika…

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, inatoka wapi taarifa.

T A A R I F A

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe taarifa kuhusu hoja inayozungumzwa sasa. Shirika la Reli la TAZARA ni shirika ambalo lilianzishwa kwa ubia wa Tanzania na Zambia sasa katika mgawanyo wa hisa ilikuwa ni kwamba Tanzania ina hisa 50 na Zambia asilimia 50. Sasa kuna changamoto ya kisheria, kwamba hakuna yeyote anayeweza kuongeza mtaji au akaboresha hiyo Reli akaongeza gharama kwa sababu bado atabaki na asilimia ile ile asilimia 50. Kwa hiyo namuunga mkono mzungumzaji ahsante sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa unapokea taarifa hiyo?

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa mwenyekiti, naipokea hiyo taarifa, hayo ni mojawapo ya maboresha ambayo yanatakiwa yafanyike kwenye reli ya TAZARA. Ni kweli inahitaji maboresho kwenye mkataba na nina imani kwa vile Mheshimiwa Rais pamoja na Rais wa Zambia walikutana hivi karibuni na katika ajenda yao ilikuwa ni namna gani wanaweza kuboresha reli ya TAZARA kwa hiyo nina imani kwamba kwenye kipande cha Tanzania sisi tuchukue hatua zaidi ili twende mbele zaidi kwa sababu hili ni suala la ushindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwenye suala la umeme ninaomba Serikali ikamilishe haraka Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, lakini kwenye suala la kilimo ninaomba Serikali iangalie ni namna gani tukitumie kilimo kuleta fedha nyingi za kigeni, hasa kwa kuongeza uzalishaji tija ili bidhaa zetu ziweze kufika kwenye masoko ya kigeni. Leo bidhaa zetu nyingi zikiwemo kahawa na maparachichi zinauzwa kwa label za mataifa mengine. Huo ni upotevu wa fedha za kigeni. Na tunahitaji pesa za kigeni kwa sababu sasa hivi tuna matatizo ya urali wa biashara. Urali wa biashara sisi hatuko vizuri sana, bidhaa tunazoagiza nje ni kubwa kuliko bidhaa tunazopeleka nje. Hii maana yake nini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umemalizika.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti,nashukuru sana naunga mkono hoja.