Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Aleksia Asia Kamguna

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetuwezesha sote kuwa hai. Nakushukuru pia kwa nafasi uliyonipatia. Nawapongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na Makamu wa Rais, kwa majukumu yote ambayo wanatupigania Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais, ni Amiri Jeshi wetu Mkuu ana majukumu makubwa anatupambania Tanzania. Tunamshukuru kwa yote. Nawapongeza pia Mawaziri kwa kazi wanayoifanya na pia naipongeza Wizara yote ya Kilimo na watendaji wote, nawapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 65 ya Watanzania ni wakulima, lakini walio wengi ni wakulima wadogo wadogo ambao sehemu kubwa ya wakulima hao wana changamoto. Changamoto hizo ni kama ukosefu wa wataalam, wana changamoto za mitaji midogo kadha wa kadha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia Mkoa wa Morogoro, wenzetu wana changamoto hizo nyingine, lakini sisi tuna changamoto kubwa zaidi. Jamani Mkoa wa Morogoro ni mkoa ambao Mungu ametupendelea, ametupa fursa ya ardhi nzuri, lakini ardhi ile sisi inatutesa. Ardhi inatutesa sasa hivi imekuwa ni shubiri, lakini watu wa nje wanaona kama vile sisi ile ardhi inatusaidia, haitusaidii hasa kwa akinamama. Kwa nini nasema hivyo? Kwa sababu mwanamke anatoka nyumbani kwake anaenda shambani kwenda kulima, lakini mwanamke yule hawezi kulima kwa sababu anaogopa wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, akifika shambani, wafugaji wakimwona kwenye shamba lake ambalo ameshalilimia, ameshalipalilia, ameshalifanyia huduma zote, mfugaji yule anakuja kulishia kwenye lile shamba hatimaye yule mama akiuliza kwa nini unalilishia, yule mfugaji anaweza akampiga, wanawafanyia vitendo vya udhalilishaji, hatimaye wakati mwingine hata kuwapotezea maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ni mbaya, hivi ninavyoongea hapa, asubuhi nimepigiwa simu kwamba mfugaji ameenda kupeleka mifugo yake kwenye shamba la mtu amekula heka 30, asubuhi ya leo. Sasa jamani tunajenga Tanzania ya aina gani? Mtu akienda shambani kwake nina mfano halisi, mtu ameenda, maskini, mkulima yule, ameenda amekodi shamba la 150,000, ameenda amelimwagilia mpunga umefika mkubwa anataka kuvuna, mwenye ng’ombe akapeleka kwenda kulishia wafugaji, kujitetea kwa nini unaenda kulishia shamba langu akampotezea maisha. Nafikiri hata kwenye vyombo vya habari mlisikia, ilikuwa ni tarehe 27/12/2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo hali haijatokea sehemu moja, imetokea sehemu nyingi, imetokea katika Jimbo la Mlimba, Jimbo la Kilosa, Mvomero na Wilaya ya Morogoro Vijiji, Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki tarehe 8/5/2022. Serikali kwa nini kuwe na matatizo ya wakulima na wafugaji miaka nenda rudi, kwa nini kusiwe na amani? Yule mtu wa Morogoro alizoweya yeye anaenda shambani analima, lakini sasa hivi nini matokeo ya hiyo hali, matokeo yake ni kwamba wale watu umaskini tuliokuwa nao umekithiri, njaa inazidi kuwa kali na kipato kimekuwa duni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali, chonde watuangalie ili tukomeshe hii hali ya wakulima na wafugaji. Nchi yetu ya Tanzania ni nchi ya amani, lakini kwa nini tufikie hapo kwenye kugombana. Watu wa Morogoro ni rahimu, wanawakaribisha wageni wote wanaokuja Morogoro hakuna ubaguzi, lakini tunapofika tushirikiane tuishi kwa amani. Akinamama wanadharaulika, wanadhalilika hasa, hawawezi kwenda mashambani, wajawazito wanawafanyia vitendo vya ovyo. Sasa naiuliza Serikali je, hii hali itaendelea hivyo mpaka lini? Tunasema kwamba vijana wanakimbilia mjini, mtu anaenda analima, shamba lake linaliwa, ataacha kwenda mjini, atakaa kijijini anafanya nini? Naomba Serikali waliangalie hilo kwa macho ya huruma, chonde chonde. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema kwamba, sasa hivi tunataka maendeleo, ardhi tunayo, lakini maendeleo hatutapata, huwezi kupata maendeleo bila kufanya kazi. Unafanyaje kazi mtu, unalima lakini unachokipata hakuna na kwa vyovyote vile lazima kama mfugaji anakula mazao ya mkulima amani inakuwa haipo. Wale watu watakuwa hawafanyi kazi. Naomba majibu ya Serikali, waniambie kwamba je, wana mpango gani au wana mkakati gani kwa hatua hii iliyofikia ili tuweze kuwa na amani? Kwa maana tusipofanya hivi, tutazidi kukaribisha umaskini, tutazidi kuwa na vijana ambao Serikali imepanga mipango mizuri sana ya kuwawezesha, lakini watawawezesha kupitia nini na wakati sisi tunasema tunategemea kilimo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ikomeshe hiyo migogoro, nafikiri itafika mahali itaonekana kwamba hawa wafugaji ina maana wana nguvu kuliko Serikali. La hasha siamini hilo, naamini Serikali ina nguvu kuliko wafugaji. Sasa inatosha, kama tulikuwa nyuma hatujaliona hilo tatizo, hilo tatizo lipo, Serikali tuamke sasa tulifanyie kazi, tulimalize, hatimaye wale watu waweze kufanya kazi turejeshe amani ambayo Tanzania tumeizoweya.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Aleksia Asia Kamguna kwa mchango wako.

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)