Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi

Hon. Christopher Olonyokie Ole-Sendeka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi ya kwanza kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuungana na Wabunge wenzangu katika azimio hili muhimu sana ambalo Bunge hili limeiamua katika siku yetu ya leo ya mkutano huu.

Mheshimiwa Spika, Waswahili wanasema, “chanda chema, huvishwa pete.” Nachukua nafasi hii kuwapongeza waliowaza na kuleta pendekezo hili la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa aliyoifanyia nchi yetu Afrika na dunia katika muda mfupi wa uongozi wake.

Mheshimiwa Spika, natoa azimio la kumpongeza Rais kutokana na kazi kubwa aliyoifanya kuimarisha demokrasia nchini. Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Awamu ya Sita anafanya haya tukijua dhahiri kwamba amesimama katika mabega ya mafanikio makubwa ya waliomtangulia kuanzia Baba wa Taifa hadi Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, kwa maana ya awamu zote zilizomtangulia.

Mheshimiwa Spika, awamu zilizotangulia ziliweka rekodi ya Tanzania katika hali ya juu sana katika suala zima la demokrasia na diplomasia. Hakuna asiyejua kazi nzuri iliyofanywa na Mheshimiwa Dkt. Salim Ahmed Salim na kuiweka Tanzania katika ramani ya dunia; na hakuna asiyejua kazi nzuri iliyofanywa na Mheshimiwa Asha Rose Migiro akiiwakilisha nchi hii na kuwa mwanamke wa kwanza na Mtanzania wa kwanza kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kwamba kazi nzuri inayofanywa na mwanadiplomasia namba moja Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuendeleza kazi nzuri iliyoasisiwa na waasisi wa Taifa hili na ameifanya kwa kasi ambayo hakuna mfano wake. Katika muda mfupi wa kazi aliyoifanya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameimarisha demokrasia, demokrasia ambayo inazingatia misingi ya utu, misingi ya usawa, misingi ya haki katika nchi hii, bara hili na hata alipokwenda kuhutubia Umoja wa Mataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amethibitisha hayo alipozungukia mataifa ya jirani kuweka mahusiano mema kati ya Tanzania na nchi zinazotuzunguka, yeye mwenyewe kwa kutembelea mataifa hayo. Leo Tanzania katika nchi zinazituzunguka, watu wanatuzungumza vizuri.

Mheshimiwa Spika, Rais pia kwa kujua diplomasia ya kimataifa inahitaji wawakilishi wa nchi wenye weledi na uelewa mkubwa, amehakikisha kwamba anawateua mabalozi ambao wana ufahamu juu ya sera, juu ya mipango ya nchi yetu, juu ya fursa zilizoko duniani, na hii imewezesha mabalozi hao kutekeleza na kuendeleza kazi nzuri aliyoianzisha katika filamu yake ya Royal Tour na tumeshuhudia wawekezaji wengi wakija katika nchi yetu, tumeshuhudia pia wafanyabiashara wetu wakiungana na dunia nzima katika tasnia ya biashara. Waswahili wanasema, “Ukiona vyaelea, ujue vimeundwa.” Haya yamefanikiwa kutokana na kazi nzuri aliyoianzisha, siyo mwingine bali ni Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi Watanzania na hasa tukiongozwa na Bunge lako Tukufu na wewe mwenyewe kutuongoza, tuna kila sababu ya kusimama kifua mbele na kwa hakika kutoa matamko ya dhahiri ya kumuunga mkono Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa sababu ameirudisha Tanzania mahali tulikokuwa tunaijua huko, na ndiyo maana hata katika kipindi hiki ambacho dunia imetikisika kutokana na tatizo la Uviko, Tanzania tumeendelea kuwa na uwezo wa kuendeleza miradi ya kimkakati, tumeendelea kuwa na uwezo wa kuweza kujenga shule zetu, zahanati zetu katika sekta zote; barabara na miundombiu mbalimbali. Hii ni matokeo ya kazi nzuri ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, haya anayafanya kwa kuzingatia mahitaji ya pande zote za Muungano; na kwa sababu yeye mwenyewe ni mtu wa haki, Waswahili wanasema, “Haki na usawa vinaposhamiri katika jamii yoyote, undugu hujengeka na maovu hujitenga.” Ukiona hilo la maridhiano leo linaloendelea, limetufanya tuwe wamoja na wenzetu wa vyama vingine vya siasa.

Mheshimiwa Spika, na haya anayoyafanya kwa kuzingatia mahitaji ya pande zote za Muungano na kwa sababu yeye mwenyewe ni mtu wa haki, na waswahili wanasema haki na usawa vinaposhamiri katika jamii yoyote undugu hujengeka na maovu hujitenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiona hili la maridhiano leo jinsi linavyoendelea limetufanya tuwe wamoja na wenzetu wa vyama vingine vya siasa. Na hii haishangazi kwa sababu

Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ni tunda la CCM, chama kinachoamini kwamba, binadamu wote ni sawa, chama kinachotambua kwamba, kila mtu anastahili kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake, chama kinachoamini katika misingi ya ujamaa na utu na ujamaa maana yake ni misingi ya utu, haki na usawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ni tuda halisi la CCM. Kwa kweli, ni tunda la Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ni tunda la hayati Abeid Amani Karume, ni tunda la Mzee Mwinyi, ni tunda la Hayati Benjamin Mkapa, ni tunda la Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ni tunda la Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, ni tunda la CCM na ni tunda la Tanzania. Hii ni tunu ambayo tunayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunamzungumzia mtu ambaye ameweka bayana kwamba, sauti yake na uwezo aliopewa na Mungu na nafasi aliyopewa ya kuwa Rais wa nchi yetu hapendi kumfokea wala kumkemea mtu, yeye mwenyewe anasema na tunamuona kutoka usoni. Matendo yake, kama ulivyoona juzi akipokea Ripoti ya CAG, katika mambo ya hovyo uliona uso wake; kwa mara ya kwanza ametoa maneno mazito kwa sababu amelazimika, ameona kuna watu hawatembeinae, hawatembei katika mapito ya njia anayoionesha. Wanafisadi uchumi wa nchi hii wakati yeye anahangaika halali kutafuta fedha kwa ajili ya ustawi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wachache wameamua kutumia fursa walizopewa katika uhujumu wa uchumi wa nchi. Katika jambo hili la msingi mama hakuweza kuficha sura yake ya ndani, ililazimika atoe kauli ambayo inawafanya wale wengine wote ambao wamepewa dhamana na Dkt. Samia Suluhu Hassan wajue kwamba, mama hafanyi masihara katika kuleta ustawi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ndio maana natumia nafasi hii kuwataka wale ambao wamepewa dhamana na Dkt. Samia Suluhu Hassan, baada ya tamko lake alipopokea Ripoti ya CAG na Ripoti ya TAKUKURU wachukue hatua kumsaidia Dkt. Samia Suluhu Hassan kutoa adhabu ambayo Watanzania wataiona. Hasira ya Mama Samia haiwezi kwenda bure, Bunge lako Tukufu lazima katika siku zinazokuja kwenye mkutano huu tutoe msimamo ambao utahakikisha kwamba, Hasira ya mama kwa wale waliofisadi uchumi wa nchi hii wanachukuliwa hatua bila kutizama sura zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, muoneeni huruma, amekwenda Marekani amemleta Makamu wa Rais, amekwenda Falme za Kiarabu ameleta maendeleo, amekwenda Ufaransa ameleta maendeleo katika nchi yetu. Leo watu wachache tu waliopewa dhamana wanatumia nafasi hiyo kujineemesha wenyewe halafu bado mpaka leo imeshaisha wiki tangu ripoti imetajwa hatujasikia wakubwa wanachukuliwa hatua; tunataka wachukuliwe hatua, hatuwezi kumuunga mkono Rais kwa maneno, lazima tumuunge mkono Rais kwa vitendo. Na kama hamtachukua hatua tukiwa kwenye Bunge hili tutakuja na hoja nyingine dhidi ya wale ambao wamekabidhiwa dhamana na Rais ya kuwashughulikia hawa ambao bado hawajashughulikiwa. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, Mwalimu Nyerere alisema uhuru bila demokrasia ni udikteta, lakini demokrasia bila nidhamu ni fujo. Uhuru bila demokrasia ni udikteta na ndio maana mama amesema hataki kwamba, uhuru wetu ugeuke kuwa ni udikteta kwa watu wengine, amehakikisha kwamba, haki inashamiri katika nchi, misingi ya utu inasimamiwa, heshima ya mtu inathaminiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tunasema pamoja na uhuru tuliopewa, lakini Mwalimu anasema uhuru bila demokrasia ni udikteta, lakini demokrasia bila ya nidhamu ni fujo; sasa

tutumie nafasi yetu ya uhuru tuliopewa kuhakikisha pia kwamba, hatufanyi fujo kwa kutumia uhuru huo bila mipaka, tujiongoze wenyewe ili tujenge Taifa ambalo lina ustawi, umoja na mshikamano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naona umekaa mkao wa kuniashiria, lakini nitoe rai tu kwetu Watanzania wote na vyama ambavyo tunavyo vya siasa; kwanza nawapongeza viongozi wa vyama vya upinzani kwa kuendelea kufanya maridhiano na Rais wetu, kwa kutanguliza maslahi ya Tanzania mbele. Sasa tumeanza vizuri, tumalize vizuri, tusiachane njiani, hii nchi inahitaji umoja na kila mtu na kila mmoja aweke tofali, nchi hii iendelee kusonga.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja hii. Na Mungu aibariki Tanzania, Mungu ambariki Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Ahsante sana. (Makofi)