Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Waziri, Naibu Waziri na viongozi wote kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti,napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti,katika kipindi kinachoishia Aprili, 2022 Serikali kupitia Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji imesimamia kwa uadilifu na ufanisi mkubwa masuala yote ya viwanda na pia kuna mwelekeo mzuri wa kuboresha mazingira ya biashara (blueprint). Pia kwa kusimamia vizuri diplomasia ya uchumi, imejenga imani kubwa kwa wawekezaji ambao wameonesha nia ya kuwekeza kwenye maeneo muhimu ya uchumi wetu. Katika kipindi cha mwaka mmoja na miezi minne, Serikali kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara, imetekeleza miradi mingi ya viwanda na pia kuboresha mazingira ya biashara (blueprint) kwa kuondoa tozo, ada na kodi ambazo zimekuwa kikwazo katika shughuli za uchumi. Kupitia blueprint, Serikali inatambua umuhimu wa kuweka mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji ili kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi na kupunguza umaskini wa kipato. Pamoja na jitihada za Serikali, bado kuna mahitaji makubwa ya viwanda vya kuongeza thamani ya madini, kuongeza thamani ya mazao yetu vijijini na pia kuna changamoto za uhakika wa masoko ya mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Serikali iendelee na msukumo wa kujenga viwanda vya mazao ili tuweza kuongeza thamani hapa nchini na pia kuzalisha ajira. Kutokana na neema ya kijiografia, nchi yetu inazalisha mazao ya aina mbalimbali ikiwemo zao la pareto na Tanzania inaongoza Afrika, pia ni wa pili duniani kwa uzalishaji wa pareto. Uwekezaji zaidi kwenye Kiwanda cha Viuadudu cha Kibaha kuna fursa kubwa ya kuzalisha mbolea na hata viuatilifu kutokana na pareto inayolimwa hapa nchini. Serikali ichukue hatua za kutafuta wawekezaji wa viwanda vya viuatilifu ambavyo mahitaji yake ni makubwa hapa nchini na hata soko la nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti,pia nchi yetu ina neema ya madini ambayo ni malighafi ya kutengeza aina mbalimbali za mbolea. Madini aina ya calcium (chokaa ya kilimo) na phosphate inapatikana kwa wingi hapa nchini na malighafi muhimu kutengeneza mbolea aina ya CAN na DAP na hata NPK. Kuwepo kwa gesi asilimia ni fursa nyingine kwa viwanda vya mbolea aina ya Urea ambayo mahitaji yake ni makubwa sana Tanzania na duniani kote.

Mheshimiwa Mwenyekiti,pamoja na madini hayo kuna madini adimu duniani kama vile NIOBIUM ya Pandahill Mbeya ambayo kuna fursa ya kujenga kiwanda cha kuchakata hayo madini ili kutengeza FERRONIOBIUM ambayo mahitajika yake ni makubwa hapa nchini na pia nje ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mradi wa Liganga na Mchuchuma, napendekeza Serikali kuchukua hatua kuharakisha uwekezaji kwenye mradi wa madini ya NIOBIUM ikiwa ni pamoja na ujenzi wa kiwanda cha Ferroniobium (FeNb) ambacho kitakuwa cha kwanza Afrika na cha nne duniani. Kutokana na mahitaji makubwa ya ujenzi wa reli, madaraja na reli ya SGR, kuna mahitaji makubwa ya vifaa vya chuma ambavyo ni imara, lakini vyepesi na vyenye ubora wa kimataifa.

Kwa kutumia sheria zetu za uwekezaji, Serikali itumie fursa za kipindi hiki ili kuvutia wawekezaji kwenye madini ya viwandani ili yaongezwe thamani hapa kwetu na pia kuvutia malighafi ya madini toka nchi zingine ili yachakatwe hapa kwetu. Tanzania imebahatika kuwepo kwa madini ya NIOBIUM ambayo inapatikana milima ya Pandahill, Wilaya ya Mbeya na mahitaji ya Ferroniobium (FeNb end product) ni makubwa duniani na hapa kwetu pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti,Serikali inahitaji kujiwekekea mikakati ya haraka (quick wins) ili kuhakikisha inakabiliana na athari za kiuchumi kutokana Covid-19 na sasa vita vya Urusi na Ukraine. Kwa kutumia rasilimali zetu za madini, Serikali inaweza kutengeneza fursa nyingi na kupitia Mradi wa Niobium na Kiwanda cha Ferroniobium, ajira 2,000 zitakazozalishwa wakati wa ujenzi na pia kutakwepo ajira za kudumu zaidi ya 600 na indirect jobs 7,000. Mradi utazalisha mapato kila mwaka shilingi bilioni 500 (US$ 220 million) ambapo mapato kwa Serikali kila mwaka shilingi bilioni 50 (US$ 22 million) uhai wa mgodi ni zaidi ya miaka 30. Hiki kitakuwa kiwanda cha kisasa cha kwanza Afrika (Modern Manufacturing Plant and Smelter).

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuingiza teknolojia hii adimu na ujuzi (skills transfer) pia itakuwa itachangia huduma za kijamii (Corporate Social Investment in Community) na chanzo cha fedha ya kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana fursa za kijografia, napendekeza msukumo zaidi kwenye EPZ na industrial parks hasa kwenye bandari zetu na maeneo yanayozunguka viwanja vya ndege kikiwemo Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Songwe kilichopo Wilaya ya Mbeya. Napendekeza Serikali ichukue hatua za haraka kubadilisha matumizi ya eneo ya iliokuwa Tanganyika Packers litumike kwa EPZ na industrial parks hasa kwa mahitaji ya viwanda mbalimbali ikiwemo vya mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napongeza mkakati wa Serikali kwa kuanzisha soko la bidhaa (The Tanzania Mercantile Exchange - TMX). Wizara ya Viwanda na Biashara iwe mstari wa mbele kuimarisha hili soko la bidhaa ambapo wauzaji na wanunuzi wanakutana na kubadilishana bidhaa na fedha katika mtindo wenye mpangilio na utaratibu maalum. Kuanzishwa kwa soko la bidhaa kutamwezesha mkulima kuweza kuuza mazao yake katika utaratibu unaoeleweka bila kulanguliwa. Pia soko la bidhaa linatupa mwanga na mwanzo mzuri wa kuboresha soko la madini kuwa sehemu ya TMX.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.