Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi hii ambayo umenipa ili nami niweze kuchangia hii Hotuba muhimu sana ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimepitia Hotuba, nimesoma hotuba yote ya Mheshimiwa Waziri ambayo ina kurasa zipatazo 201. Napenda nikiri kabisa kwamba taarifa hii ya Mheshimiwa Waziri imesheheni mambo mengi muhimu sana katika ujenzi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimeangalia Taasisi zetu zinavyofanya kazi vizuri. Taasisi ya CAMARTEC, TIRDO, TIMDO na SIDO. Kazi nzuri waliyoifanya ya taknolojia ya kisasa ya kuandaa mashine ambazo zinaongeza thamani ya bidhaa zinazozalishwa kwa ajili ya usindikaji wa mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi. Hii ni kazi nzuri sana ambayo inafanywa na taasisi zetu hizi na mimi nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Ma-CEO wa taasisi hizo pamoja na watumishi wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, kazi kubwa hapa ni kuzisaidia hizi taasisi sasa ziweze kufanya kazi vizuri zaidi. Utakuta taasisi kama hizi zinafanya kazi kubwa kama hiyo, lakini nenda kaangalie bajeti zao, utasikitika sana. Serikali itenge fedha nzuri, nyingi za kutosha kuziwezesha hizi Taasisi. Tuna vijana wetu waliobobea vizuri na ndio wanaoyafanya haya mambo makubwa. Kwa hiyo, ni muhimu sana wakaweza kupewa fursa ya kuweza kufanya kazi vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu uwekezaji wa Serikali pamoja na sekta binafsi. Waheshiwa Wabunge hili suala la uwekezaji wa Serikali na sekta binafsi linahitaji kuangaliwa kwa makini sana. Mikataba mingi tuliyoingia inanyonya mapato ya nchi. Mikataba mingi tuliyoingia katika uwekezaji wa Serikali na sekta binafsi inanyonya uchumi wa nchi, inahamisha rasilimali za nchi na inahamisha ajira za Watanzania. Lakini vilevile katika mikabata hii mingi tunayoingia inapora ajira za Watanzania, kwa hiyo unajikuta kwamba mkataba unaingiwa wa Watanzania hawa ambazo fedha za Watanzania zinaenda kulipa ajira kwa watu wengine wakati tunao vijana ambao wanaweza kufanya kazi nzuri sana hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo mikataba mingi ambayo tunayoingia ambayo ni questionable na mingine imetuletea madhara makubwa sana. Tunayo mikataba, sasa hivi TPA naye ameanza kutafuta mdau, ameanza kutafuta mbia. Mikataba ya namna hii; lakini ipo mikataba inayotusumbua mpaka sasa hivi ya TRA na SISPA Company ambayo nayo inahamisha fedha za Watanzania. Lakini ipo mikataba mingine tumeingia majuzi hapa ya India Tech Mahindra na TANESCO ya ziadi ya bilioni 70 kwa ajili ya kuendeleza mifumo ya TEHAMA wakati wataalam wa TEHAMA tunao hapa wa kila aina wanaoweza ku-develop mifumo ya TEMAHA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wetu wameandaa mifumo mizuri kama GePG, POS na hata MaxMalipo, mifumo mizuri tu. Leo unaenda kutafuta mfumo India kwa ajili ya kufanya nini? Sasa mikataba ya namna hii imekuwa ikituletea madhara makubwa sana. Na hivi sasa hivi nasikia Symbion inapigiwa chapua hapa tuilipe bilioni 356, bilioni 356 lakini inapigiwa hili chapuo wakati huo huo hatuambiwi aliyeingia mkataba huo na kutusababisha tuwe na mkataba ambao hatuwezi ku-exit hata kama mkataba ule unatuingizia hasara, amechukuliwa hatua gani? Tunaambiwa na chapuo hilo linapigwa bila kuambiwa kwamba huyu Symbion malimbikizo yake ya kodi ni shilingi ngani na anapaswa kutulipa shilingi ngapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, linapigwa hilo chapuo hatuambiwi ukaguzi gani uliofanyika juu ya mambo yaliyojificha nyuma ya pazia hili. Wabunge tukataeni mikataba ya namna hii lakini tukataeni hata kulipa hizi fedha. Uchunguzi ufanyike, ukaguzi wa kina ufanyike kilichojificha nyuma ya Symbion tuweze kuyajua yote mazagazaga yaliyopo na tuweze kuzijua haki zetu zilizopo katika hilo eneo. Lakini mikataba yote ambayo tunaitambulisha kwamba ni mikataba mibovu iitishwe hapa Bungeni tuweze kuifuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni hili suala la mfumuko wa bei. Suala la mfumuko wa bei. Ni kweli imeelezwa hapa kwamba mfumuko wa bei umesababishwa na UVIKO 19 pamoja na vita vya Urusi na Ukraine, tumeelezwa hapa. Ni kweli sababu hizi zinachangia mfumuko wa bei, lakini zipo sababu zingine ambazo zimechangiwa na ukosefu wa uadilifu wa viongozi wetu na watendaji wetu. Ziko sababu zilizosababishwa na uzembe na usimamizi dhaifu wa maeneo mbalimbali ambao tunaufanya sisi wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachosema na kuliambia Bunge lako hili ni kwamba mfumuko wa bei huu unaoendeelea hivi sasa umesababishwa na umetengenezwa na tumeutengeneza sisi wenyewe tuliomo humu ndani. Mateso haya ya mfumuko wa bei ambayo wanayapata wananchi sasa hivi tumeyatengeneza hapa kwa kukosekana kwa uadilifu, kwa kukosekana kwa usimamizi makini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la upangaji holela wa bei. Upangaji holela wa bei sisi wote tunashuhudia hapa, bidhaa zote zimepanda bei, kila siku zinatangazwa bidhaa kupanda bei. Lakini ukweli ni kwamba pamoja na sababu zingine, sababu ya upangaji holela wa bei, mtu anaamua tu kupandisha bei hili suala limekuwa likiturudisha nyuma sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri hapa ametueleza kwamba kuna upandaji holela wa bei lakini tunachoshangaa ni kwamba kama kuna upandaji holela wa bei, na yeye Waziri anajua na anayo mamlaka yake ya FCC inayosimamia ushindani, na Sheria ya Ushindani Namba Nane ya Mwaka 2003, hawa watu wanaopandisha bei kiholela kwa nini hawajachukuliwa hatua? Kwa nini hawajachukuliwa hatua? Waziri anawajua waagizaji wa mafuta nje ya nchi, anawajua waagizaji wa ngano nje ya nchi, anawajua wazalishaji wa ndani na amefanya tathmini na akagundua watu wamepandisha bei kiholela. Hao waliopandisha bei kiholela kwa nini hawajarudishwa kwenye mstari ili wananchi waweze kupata bei nafuu? Waziri kwa nini anawaogopa hawa? Au anataka kutuambia kwamba watu hawa wana nguvu zaidi kuliko Serikali? Au Waziri anaubia nao? Na kuwaacha Watanzania waendelee kuteseka na mfumuko huu mkubwa wa bei wa kuamuliwa na watu waliokaa na kukubaliana tu tupandishe bei? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni suala la uhaba wa nishati ya umeme. Kuhusu suala la uhaba wa nishati ya umeme, Kamati imetueleza hapa imesema ilipotembelea viwanda viwili ikaenda kugundua kwamba kuna viwanda umeme ulikuwa unakatika mara 10 ndani ya masaa manne. Ni maneno ya Kamati siyo maneno ya Mpina. Umeme ulikuwa unakatika zaidi ya mara 10 ndani ya masaa manne. Pale unategemea kuna uzalishaji gani? Uzalishaji viwandani unashuka na kama uzalishaji viwandani ukishuka wafanyabiashara wataamua kupandisha bei, kwasababu uzalishaji wao utakauwa umeshuka, ili waweze kufidia gharama ya uzalishaji na kupata faida, na ndiyo lazima upate mfumuko wa bei.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja.

MWENYEKITI: Haya malizia.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ni mafuta. Mafuta, Mbunge mwenzetu hapa Mheshimiwa Hamis Tabasam, Mbunge wa Sengerema alitueleza kuna wizi mkubwa unaofanywa kwenye Petroleum Bulk Procurement Agency kuna wizi mkubwa unafanyika kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa hivi hoja ya wizi unaofanyika kule kwenye agency ya kununua mafuta tulitegemea ingeweza kuwekewa ukaguzi wa haraka, CAG na PCCB wakavamia wakafanya ukaguzi na kuujua ukweli kama Watanzania wamepandishiwa bei na mafisadi wachache na wezi wachache tukaujua ukweli lakini sasa hivi hoja inaondolewa kwenye wezi waliofanya wizi inapelekwa kwenye tozo ambazo hizi tunapata shughuli za maendeleo nyingi kutokana na hizo tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi seriousness yetu iko wapi? Watanzania wanalia, wanapandishiwa bei za mafuta, watu wanatangazwa kufanya njama za manunuzi, wanafanya wizi kwenye manunuzi, wanapandisha bei makusudi, tunaletewa taarifa hapa Bungeni ukaguzi haufanyiki na uchunguzi haufanyiki. Ni lazima mambo haya tuyakatae na lazima tuwahurumie Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.