Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na wataalamu wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya kulinda usalama wa raia.

Mheshimiwa Spika, mimi mchango wangu utalenga kwenye zoezi la kusitisha ubandikaji wa bima katika vioo vya magari ambayo ililetwa na kanuni ya mwaka 1979 ikiitwa The Display of Road License and Evidence of Motor Vehicle Insurance Regulation, GN 79 of 1979.

Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) ilielekeza kwamba kuanzia Aprili Mosi, 2021 ukataji wa bima kwa vyombo vya moto ufanyike bila mteja kubandika stika kwenye kioo cha gari kama ilivyozoeleka na badala yake mteja hupewa namba ya stika ya kielektroniki (e- sticker).

Mheshimiwa Spika, mteja anakapokata bima hupewa namba ya stika ya kielektroniki, risiti ya malipo EFD, hati ya bima pamoja na mkataba wa bima.

Mheshimiwa, lengo la uboreshaji huu ilikuwa na nia ya kupata huduma haraka, kudhibiti upotevu wa mapato na uhalifu unaoweza kufanywa na watu wasio waaminifu.

Mheshimiwa Spika, kabla ya mabadiliko haya, hapo zamani kabla ya mambo ya teknolojia, njia pekee ya kujua uhai wa bima ilikuwa ni kupitia hiyo sticker iliyokuwa inabandikwa kwenye kioo cha gari. Askari akisimamisha gari hukagua uwepo wa sticker iliyo hai na kumruhusu asiye na kosa kuendelea au kumkamata aliyevunja sheria.

Mheshimiwa Spika, ujio wa matumizi ya bima mtandao ilitokana na uwepo wa makampuni yaliyokuwa yanatengeneza sticker fake na kuikosesha Serikali mapato na kuhatarisha usalama wa raia.

Mheshimiwa Spika, sticker hizi ilikuwa zinarahisisha ukaguzi wa trafiki na kumsaidia kiurahisi mwenye gari kujua bima yake inamaliza muda wake lini.

Mheshimiwa Spika, katika matumizi ya njia hii mpya ya kimtandao, madereva katika maeneo mengi ya nchi wamepata changamoto kwa sababu trafiki wa barabarani na TIRA hawajapeana mwongozo wa kutosha juu ya utaratibu mpya wa kutokubandika sticker, na ndio maana wanaoendelea kuumia ni baadhi ya wateja wenye magari.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu ninaishauri Serikali chini ya Mamlaka ya Bima na Polisi Tanzania wakae na kufanya yafuatayo; kwanza warudishe utaratibu wa zamani wa kubandika sticker za Bima ya Taifa kwenye vioo vya magari. Maeneo ambayo mifumo ya ukaguzi ya kielektroniki haisomi, madereva hupata bughudha na kusimama barabarani muda mrefu. Mara nyingine wameandikiwa faini pamoja na kwamba wamelipia bima kwa mfumo mpya.

Mheshiiwa Spika, pili, sheria za nchi zitumike kutoa adhabu kali kwa makampuni au watu binafsi watakaojihusisha na utengenezaji wa sticker fake.

Tatu, busara itumike ili usajili wa kielektroniki uwepo na pia iruhusiwe anayetaka sticker apewe na abandike kwenye gari lake. Mfumo wa kielektroniki ni muhimu sana kwenye kuhifadhi kumbukumbu sahihi za walipa bima.

Mheshimiwa Spika, nne, mafunzo maalumu ya namna ya kutumia mifumo hii ifanyike ili mabadiliko yaliyotokea yaeleweke pande zote na mwisho wa siku watumiaji wa chombo kama kalipia bima yake asipate usumbufu wa aina yoyote barabarani.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.